Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nami nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wote watatu wa Kamati zote tatu kwa ripoti nzuri ambayo ameweka hapa mezani. Pia nawapongeza Wajumbe wa Kamati hizo.

Kamati ya Sheria Ndogo ninawapongeza sana kwani wamekuwa ni msaada mkubwa sana katika maboresho na marekebisho ya makosa ya namna moja ama nyingine ambayo yamekuwa yakijitokeza kwenye sheria ndogo ambazo zimekuwa zikitungwa kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa lakini vilevile kwenye Serikali Kuu, Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mwenyekiti Andrew Chenge kwamba tutaendelea kushauriana na Kamati yake na Wajumbe ili tuweze kuboresha. Kama walivyosema, kwa kweli tumeanza kwenda vizuri ndani ya Serikali, wametupongeza, tunapokea pongezi hizo tutajitahidi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Kamati ya Tawala za Mikoa, Waheshimiwa Wabunge wamesema mengi, ninawashukuru pia. Kipekee nampongeza ndugu yangu Mheshimiwa Mchengerwa na Kamati ya Katiba na Sheria. Kamati hiyo nayo imekuwa ni msaada mkubwa sana kwetu kwenye maeneo mbalimbali na hasa Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa kweli wametusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisiti kusema, hata wewe uliyekalia kiti kama Makamu Mwenyekiti mmesaidiana sana na Kamati katika kuhakikisha tunafanya kazi zetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Wajumbe wote ama Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja hizi, lakini hasa niungane na wale Wabunge ambao wameanza kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri zinazofanywa na Serikali yetu. Vilevile nami bila kusita, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi anazozifanya. Niwathibitishie tu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote, Mheshimiwa Rais wetu amedhamiria kuleta mabadiliko makubwa katika nchi yetu nasi wote tunayashuhudia kwa macho. Tumemshuhudia Mheshimiwa Rais pamoja na utendaji mbalimbali wa kazi ndani ya Serikali na Taasisi amefanya ziara za kikazi katika mikoa yote bila kubagua hata kwenye Majimbo ya Upinzani Mheshimwa Rais amefika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesikiliza kero za Watanzania, amezitafutia ufumbuzi, amefanya hivyo kwa mapenzi makubwa na dhamira ya dhati kabisa, tuna kila sababu ya kumpongeza na kumshukuru Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Makamu wa Rais na hata Waziri Mkuu mmeona, sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu tunaratibu kazi za Mheshimiwa Waziri Mkuu, mmemwona Waziri Mkuu kwa kweli naye amefanya kazi nyingi na kubwa katika mikoa yote na katika nchi nzima ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye baadhi ya hoja. Nawashukuru Wajumbe wa Kamati na Taarifa za Kamati nikiacha ile ya Sheria Ndogo nimeshasema, lakini Kamati ya Katiba na Sheria tunawashukuru, mmeendelea kuboresha katika maeneo ya Mfuko wa Vijana; naomba niwahakikishie kwamba mmetupongeza, tunataendelea kuongeza bidii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeamua Mfuko wa Vijana sasa hivi kwa Ofisi ya Waziri Mkuu ubadilishe mwelekeo, kutoka katika kutoa mikoa midogo midogo kwa wajasiriamali wadogo wadogo, ile tutaicha TAMISEMI. Sisi sasa tunataka ku-concentrate na vijana ambao ni graduates, wana certificate, walioanzisha makampuni ili wakopeshwe fedha hizo, wafungue makapuni na miradi mikubwa ambayo itatoa ajira kwa vijana wenzao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tumeli-present kwenye Kamati na Kamati mmeshuhudia, tumeshafanya mageuzi makubwa sana kupitia Mfuko wa Vijana; tunawahakikisha vijana na Waheshimiwa Wabunge, tunataka kuutumia mfuko huu tofauti na 10% ya Halmashauri twende sasa kwenye mitazamo ya ajira ambazo zinahusika na miradi mikubwa itakayofanywa kupitia kwenye mifuko wa vijana. Tutafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, tunajitahidi sasa hivi ili kuondoa gap ya ujuzi nchini. Tunazo program na mkakati wa Taifa wa kukuza ujuzi, kuhakikisha kwamba tunaondoa tatizo la ujuzi katika uwekezaji ndani ya Taifa letu. Kwa hiyo, tayari kazi hiyo inafanyika vizuri, Kamati mmeona na mmsema, nasi tutaendelea kufanya hivyo. Ili kutatua tatizo la ajira kwa vijana, tumekuja na program ya internship ambayo sasa tunawachukua vijana wetu graduates tunawapeleka kwenye private sector, wanakwenda kufanya mafunzo ya uzoefu na wengi wamekuwa sasa wakiajiriwa huko kwenye private sector. Kwa hiyo, Kamati imetushauri mambo mengi na tunaipongeza tunawashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamesemwa sana pia ndani ya Bunge na hasa Wabunge wa Upinzani kwamba Serikali hii haijali Wizara ya Kilimo na sekta ya kilimo. Naomba tu niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge, kwenye utaratibu wa kupitia bajeti; bajeti za Serikali ni bajeti zinazochukua sura ya kisekta. Ukichukua bajeti ya Wizara ya Kilimo utaikuta kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara, utaikuta kwenye Wizara Ofisi ya Rais, TAMISEMI imekuwa budgeted huko na kwenye Wizara nyingine. Hata kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu hata sisi pia tuna bajeti ya kilimo ambayo inaenda kutekeleza miradi ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawapa mfano, tulikuwa na programu ya MIVARAF ya kuongeza thamani ya mazao na miundombinu ya masoko. Mradi huo peke yake kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda kwenye sekta ya kilimo tumetumia bilioni 282.16 na hizo zote zimetoka tena programu hii imewanufaisha Bara na Visiwani pande zote mbili za Muungano. Tumeweza kujenga masoko mapya, masoko mapya peke yake 16 na nyie Wajumbe wa Kamati ni mashahidi, tumekarabati masoko matano, tumejenga maghala mapya 29 katika hiyo programu.

Lakini tumeweza kujenga miundombinu ya barabara na mpaka sasa programu hiyo imeweza kusaidia sana usafirishaji wa mazao kutoka shambani kwa sababu ya kuboresha miundombinu ya barabara kwa sasa tani za usafirishaji wa mazao kwenye programu hii zimetoka tani 230 mpaka 808 kwa sababu ya programu hiyo.

Sasa tunashangaa kama kuna wenzetu wanasimama hapa ndani halafu wanabeza kazi nzuri hii inayofanywa na Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli. Haiwezekani. (Makofi)

Ninaomba tunapokuwa tunachangia humu ndani tupingane kwa facts sasa mtu anaenda anachukua kipande kidogo tu, akichukua hicho kipande kidogo ndiyo anatangaza kama ni jambo zito kweli kweli. Naomba niwaambie Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na mpango wa bajeti za kiwizara tunao mpango na mfumo wa bajeti za kisekta, bajeti ya maafa haiwekwi kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu peke yake, itawekwa miundombinu barabara watawekewa, madarasa wataweka TAMISEMI, wataweka Wizara ya Elimu, vituo vya afya watapeleka Wizara ya Afya huo ndiyo utaratibu tunaenda kileo zaidi na tunawaambia kwamba Serikali hii imejipanga kweli kweli mtatutafuta hamtatupata, lakini sisi tunasonga mbele na vitu vyetu vinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaendelea programu hii pia imepunguza muda wa kusafirisha mazao. Kusafirisha mazao kabla ya programu hii ni ya kilimo tumebeza sana hapa fedha za kilimo, wakulima walikuwa wanatumia masaa matatu sasa wanatumia chini ya nusu saa moja na nusu kusafirisha mazao yao.

Kwa hiyo naona kwamba tumeboresha sana sana. Lakini naomba nikubaliane na ninyi yako maeneo mengine bado tunatakiwa kuyafanyia kazi zaidi, kwa mfano kwenye suala la uwekezaji na biashara tunalo Baraza la Biashara la Taifa wanafanya kazi nzuri lakini sisi sasa ndani ya Serikali tumeamua kutengeneza mifumo, mfumo wa ki-TEHAMA wa utoaji wa vibali vya ajira kwa wageni ili mfumo uwe wazi, usiwe na usumbufu wa kusababisha kero na mlolongo mkubwa kwa wawekezaji wanapotaka kupata vibali vya wageni kama ni TIC ama kwenye sekta nyingine kazi hiyo tunaifanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa masuala ya local content na local content ipo pia ndani ya ofisi yetu na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, ambalo linasimamia sheria ya mwaka 2004 na sera ya mwaka 2004 imeendelea kufanya kazi zake vizuri. Tulichokifanya Waziri Mkuu amezindua Mkakati wa Taifa wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile tumezindua muongozo wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na baada ya kuyafanya hayo matokeo chanya yamepatikana, kwa mfano wakati wa ujenzi wa Daraja la Mfugale, Daraja la Mfugale lilikuwa linahitaji wafanyakazi 616 lakini wafanyakazi waliofanyakazi katika ujenzi wa daraja la Mfugale, 589 ni Watanzania na 27 ndiyo walikuwa wafanyakazi wa kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, manunuzi kwenye sekta ya manunuzi tulikuwa tunataka makampuni 15 lakini kwenye manunuzi makampuni 14 yalikuwa ya Kitanzania na kampuni moja tu ndiyo lilikuwa kutoka nje ya nchi ya Tanzania. Kwa hiyo, miradi hii ya kimkakati inafanyakazi vizuri sana kwenye dhana ya local content, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge muendelee kutuunga mkono, tutayasimamia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaenda kwenye suala la mwisho na lenyewe ni kuhusu uchaguzi sasa hapa naomba Waheshimiwa Wabunge mnisikilize vizuri. Kwenye suala la uchaguzi tumeshaanza kuboresha daftari la mpiga kura awamu ya kwanza na kwenye kuboresha daftari la mpiga kura awamu ya kwanza, umeshafanya route 13 kati ya route 14 imebakia route moja tu mikoa miwili Pwani na Dar es Salaam, na tukishamaliza route ya 14 tunaanza uboreshaji awamu ya pili kwa mujibu wa sheria, kwa hiyo siyo kweli kwamba eti hatujajipanga, tumejipanga vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini namuomba tu Halima atulie, ninachotaka kusema tulikadiria kuandikisha, kuboresha daftari kama ni kuandikisha wapiga kura wapya, kama nikubadilisha maeneo ya kupigia kura, kama ni jambo lolote linalohusiana na uboreshaji, tulitarajia uboreshaji huo uwe wa asilimia 17 lakini ajabu wananchi wamejitokeza wengi wamekuja kuboresha, wengi wamekuja kujiandikisha uboreshaji mpaka sasa umefika 29% ya wapiga kura wa mwaka 2015. Maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba wanaimani na Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli, na wanajiandaa kuhakikisha kwamba wanaingia kwenye uchaguzi. Sasa tunaambiwa kwamba hapa hii tume sijui ya uchaguzi siyo huru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-quote tu Katiba ya Jamhuri ya Muungano kifungu cha 74 (7) kifungu hicho cha 7 kinasema, kwa madhumuni ...

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu jamani.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima naomba tumwachie amalize

MHE. HALIMA J. MDEE: Sasa hizi hoja ni za Wenyeviti sasa huyu hoja siyo yake anajibu kama hoja ya kwake?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jenista naomba umalizie endelea, naomba uendelee.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaanza upya eneo hili. (Makofi/Kicheko)

Kwa utaratibu wa shughuli zetu za Bunge...

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naomba mtulie amalizie, Mheshimiwa Jenista naomba umalize.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo heshima sana ya kiti chako na ninaomba niendelee kusema, Ibara ya 74(7), (11) na (12) labda nisome ile ya 11 katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii Tume ya Uchaguzi haitalazimika kufuata amri ama maagizo ya mtu yeyote, au idara yoyote ya Serikali au maoni ya chama chochote cha siasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo mifano dhahiri tu na ninaomba Waheshimiwa Wabunge Tume hii imefanya kazi toka ilipoundwa kwa mujibu wa sheria na mfano mzuri mwaka 2010 tulipofanya uchaguzi kwa sababu Tume hii ni huru hata kama kunatokea mashtaka ya matokeo ya uchaguzi, tulijifunza kwa mfano wananchi wa Jimbo la Arusha walikwenda kupinga ushindi wa Godbless Lema mahakamani, lakini Tume ya Uchaguzi kwa sababu ni huru ilisimama na ilimpasa Mwanasheria Mkuu wa Serikali aungane na Tume kumtetea Godbless Lema na akabaki kuwa Mbunge ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine mwaka 2015 Mheshimiwa Mbunge Chief Whip Ester Bulaya, Mheshimiwa Wasira alipinga matokeo ya Ester Bulaya, lakini kwa sababu Tume hii ni huru Mwanasheria wa Serikali alisimama na Tume ya Uchaguzi na walimtetea Ester Bulaya na leo ni Mbunge mpaka leo ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Ninataka kusema nini, nataka kusema hivi kifungu cha 74(7), (11), (12) kimeeleza kabisa tume yetu ni tume huru labda tu kama tunataka kuibadilisha jina, lakini kwa mujibu wa Katiba tume hii ni huru na inafanyakazi zake kwa uhuru bila kuagizwa na chama chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuingie kwenye uchaguzi tukapambane kwa hoja chama ambacho kitakuwa na hoja za msingi kitashinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)