Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

MHE. JASSON S. RWEIKIZA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi kuja kuhitimisha hoja yangu ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa.

Niwashukuru pia Wabunge wote waliochangia na kutoa mawazo mbalimbali kwenye hoja hii, ambayo yamekuwa ni ya msaada mkubwa lakini pia niwashukuru sana Mawaziri na Naibu Mawaziri ambao wamejibu nyingi ya hoja hizo na kwahiyo kwenye majumuisho yangu sitagusia yale ambayo wameshajibu Mawaziri nitasema tu yale ambayo nataka kuweka msisitizo kidogo.

Mheshimiwa Lolesia Bukwimba alisisitiza sana kuhusu suala la TARURA. TARURA inapata pesa kidogo sana 30% ya hela ya road fund. Road Fund ina fedha za kutosha kujenga barabara za nchi hii lakini hela nyingi inaenda TANROADS, TANROADS barabara nyingi zimekwisha kamilika zimejengwa kwa lami madaraja yapo TARURA ina barabara nyingi sana za vijijini ambazo ni mpya ambazo zinapeleka pembejeo, zinatoa mazao mashambani huko.

Kwa hiyo kwa kweli nisisitize tu kwamba mchango wa Mheshimiwa Lolesia Bukwimba umekuwa ni wa msaada kuonesha umuhimu wa jinsi ambavyo tumekuwa tukisema mara nyingi kwamba TARURA iongezewe fedha kusudi iweze kumudu majukumu yake, inakwama kwasababu fedha zake ni ndogo sana, lakini pia ameongelea sekta ya afya ambayo Waheshimiwa Mawaziri wamejibu kwa kina na kwa ukamilifu. Kuhusu kuajiri watumishi na mambo mengine.

Mheshimiwa Pauline Gekul naye amezungumza suala la TARURA kupewa 50% amependekeza kwamba ipewe 50% maana yake na TANROADS ipewe 50% ya fedha za road fund hili ni jambo zuri, tunaliunga mkono sisi kama Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini amesema pia Mheshimiwa Gekul mafunzo kwa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ni jambo zuri sana, wamechaguliwa juzi hapa mwaka jana mwishoni, na kwa kweli hawana ujuzi ule unaotakiwa kumudu majukumu yao, ni vizuri waende kwenye mafunzo niseme tu kwamba mafunzo haya yako tayari, kile Chuo cha Hombolo kina kozi hizo za muda mfupi, za muda wa kati na muda mrefu. Halmashauri zijipange zipeleke hawa wenyeviti na viongozi wengine kwenye mafunzo hayo ili kuweza kupata mafunzo na kumudu shughuli hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia wazee iwekwe kwenye mpango wa 10% ni jambo zuri, ni wazo zuri kwa sababu wazee hao kwa kweli wengine hawana uwezo wa kujimudu maisha yao, ni vizuri wakapewa asilimia hizo angalau mbili kwenye hiyo 10 waweze kujisaidia katika maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi kama kamati tumekuwa wakali sana kwenye halmashauri hizi kwamba wahakikishe wanatenga asilimia 10 na kuzipeleka kwa wanawake na vijana na mwaka 2017 tuliwagomea hata bajeti zao, hatukupitisha bajeti zao kwamba yeyote ambaye hakutoa 10% asipewe fedha za bajeti, mwaka uliofuata wakawa wamefanya maboresho makubwa sana na fedha zikawa zimeongezeka. Kwa hiyo nazipongeza Halmashauri hizo ambazo zimeboresha matoleo hayo kwa walemavu, akinamama na vijana. Sasa pendekezo la Mheshimiwa Gekul ni zuri kwamba hata wazee wafikiriwe kuingizwa huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ruth Mollel ameongelea mambo kadhaa mambo mengi lakini mojawapo kubwa ni kwamba DART haijahama kutoka pale Jangwani kwenye mafuriko. Ni kweli na sisi tumeshatoa maagizo kwa DART kwamba wahame toka pale Jangwani waende sehemu ambayo ni ya juu haina mafuriko ya mara kwa mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Godbless Lema ameongelea mambo mengi pia, moja amesema ushindi ni kwa mtutu badala ya kutumia kura, jambo hili siyo la kweli kwa sababu kama ni kweli hata yeye amegombea na ameshinda, ina maana ameshinda kwa mtutu pia, ameingia humu kwa mtutu ambayo siyo kweli hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Vedasto Ngombale amepongeza TASAF, ndugu Mussa Mbarouk amezungumzia mambo mengi amesema uchaguzi haukuwa huru na haki, siyo kweli CCM ilishinda kwa haki kwa kura nyingi, kwa sababu haki ni pamoja na kujitoa, waliojitoa walikuwa na haki ya kujitoa, walijitoa wenyewe CCM ikaendelea na uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jacqueline Msongozi amezungumza mambo kadhaa mengi, Mheshimiwa Mwanne Mchemba TARURA, MKURABITA, TAGLA na eGA, Mheshimiwa Joram Hongoli wote wamezungumzia mambo ya TARURA hii inaonesha kwamba TARURA kwa kweli inastahili kuongezewa fedha. Kwa hiyo ni msisitizo mzuri ambao na sisi Kamati tunasisitiza kwamba TARURA iongezewe mgao wa fedha za road fund.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuaajiri walimu Waheshimiwa Mawaziri wamejibu hiyo. Suala la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga kwamba uraia pacha uruhusiwe. Sisi tunaunga mkono kama kamati uraia pacha uruhusiwe kwa sababu hawa wanaokwenda kule nje kwanza hawajaasi uraia wa nchi hii, lakini hawajakimbia nchi pia wameenda kutafuta tu wanatafuta fedha wanarudi wapewe uraia pacha na waweze kuleta fedha Tanzania, tunaunga mkono, TARURA amezungumzia Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Lucy Mlowe uchaguzi mdogo amesema Wenyeviti hawakubaliki, uchaguzi haukuwa huru na haki, lakini hawakutuambia huo utafiti amefanya kwa njia gani, utafiti wake amefanyaje huo, hakutuambia ametumia mfumo gani wa utafiti, hakutuambia amehoji wananchi wangapi ambao wamesema hawawataki Wenyeviti hao. Kwa hiyo utafiti huo kwa kweli hauna mashiko.

Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia mambo mbalimbali ambayo kama nilivyosema mengi yamejibiwa na Waheshimiwa Mawaziri.

Nimalizie kwa kusema kwamba Mheshimiwa Rais Magufuli amefanya mambo mengi sana mazuri, makubwa ya kujenga nchi hii kwa weledi na uadilifu mkubwa sana. Moja ambalo halijasemwa sana ni la kudhibiti ongezeko la maeneo ya utawala, huko nyuma ilikuwa ikikaribia uchaguzi au mdogo au uchaguzi wa mitaa, uchaguzi mkuu inatengwa kata, inatengwa wilaya yanatengwa majimbo, Mikoa, Wilaya sasa hivi hiyo imekoma kupunguza gharama za utawala na hizo fedha zinatumika kujenga hospitali, kujenga barabara, kujenga madarasa na kadhalika.

Kwa hiyo nahitimisha hoja yangu kwa kuwashukuru Wabunge wote waliochangia na nakushukuru mwenyekiti kwa nafasi hii ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.