Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

Hon. Mboni Mohamed Mhita

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia katika Wizara hizi nyeti. Naomba nitumie fursa hii kwanza nikiwa Mbunge mwanamke, kumshukuru sana Mheshimiwa Rais na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna ya kipekee na jinsi ambavyo amejitoa kuweza kuimarisha na kudumisha sekta ya afya nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza sana dada yangu Mheshimiwa Ummy na kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile kwa namna ya kipekee kwa jinsi ambavyo wanatumikia Wizara hii kwa weledi wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amechukua initiatives za kipekee kabisa katika kuhakikisha kwamba, anamaliza changamoto kwenye Sekta ya Afya. Ushahidi wa kwanza ambao wengi ulituonyesha dhahiri kwamba Mheshimiwa ameamua kujitoa ili kuweza kumaliza changamoto hizi, ni pale alipoelekeza gawio la fedha zinazopatikana kutoka kwenye Kampuni ya Simu ya Airtel kuja na kujenga hospitali katika Makao Makuu ya Nchi hapa Dodoma. Ni Rais wa kizalendo sana anayeweza kufanya maamuzi hayo ya kishujaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tumeshuhudia katika kipindi hiki cha miaka minne ya utekelezaji Vituo vya Afya 352 vimejengwa Tanzania. Nasi wananchi wa Handeni Vijijini tulibahatika kupata shilingi milioni 800 ambazo tukazigawa kwenye Kituo cha Afya cha Kabuku pamoja na Kituo cha Afya cha Mkata. Hakuishia hapo, tumeshuhudia Hospitali za Wilaya 67 zikijengwa katika kipindi cha miaka minne tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu kwa haraka haraka mtu anaweza akaona ni chache, lakini tujikumbushe huko nyuma; toka tumepata uhuru tulikuwa na Hospitali za Wilaya 77 tu. Sasa sisi wenyewe tufanye hesabu hiyo, yaani toka tumepata uhuru tuna hospitali 77 dhidi ya miaka minne tu ambayo zimeongezeka hospitali za ziada 67. Kwa hesabu za haraka haraka hapo mtu unaweza ukajiongeza na ukaona. Hospitali 77 kwa miaka yote tangu uhuru versus miaka minne na upatikanaji wa Hospitali za Wilaya 67. Hiyo ni takriban amepiga jiwe kwa asilimia 70 ndani ya miaka minne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, naendelea hapo. Katika kipindi hiki cha miaka minne tumeshuhudia ujenzi wa hospitali tano za mikoa; Njombe, Songwe, Katavi, Simiyu, Geita na Hospitali ya Kikanda Mtwara. Nadhani habari hii itamfurahisha sana mama yetu Mheshimiwa Riziki Lulida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii pia kugusia kidogo kwenye mpango wa kidunia wa 90, 90, 90, ambapo mpango huu unasema asilimia 90 ya wale ambao ni suspects wa maambukizi ya UKIMWI wafikike na wapimwe. Asilimia 90 ya wale waliopimwa waweze kuanza kupata huduma ya dawa, lakini 90 ya mwisho ni wale ambao wameanza dawa, zile dawa ziweze ku-suppress yale maambukizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwapongeza sana Wizara ya Afya. Dada yangu Mheshimiwa Ummy na kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Faustine, Tanzania tuko mbali. Katika 90 ya mwanzo tuko kwenye 85% tunakwenda juu; 90 ya pili tuko kwenye asilimia 90; na tisini ya tatu tuko kwenye asilimia 90. Pongezi nyingi sana kwa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sehemu ambako kunakosekana changamoto. Changamoto ambayo tunaipata na ninaamini kwamba Wizara iko katika hatua za mwisho kabisa kutatua changamoto hii ni changamoto ya watumishi. Naomba nigusie Jimbo la Handeni Vijijini. Handeni Vijijini tuna changamoto kubwa ya watumishi kwenye Sekta ya Afya. Katika hitaji la watumishi asilimia 100, sisi tuna access ya watumishi asilimia 25 tu. Kwa lugha nyingine ni kwamba, tuna uhaba wa asilimia 75, yaani katika hitaji la watumishi 896 sisi tuna watumishi 226.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutumia fursa hii kushauri Wizara, naelewa wazi kwamba Wizara iko kwenye hatua za mwisho kabisa kuweza kutatua changamoto hii ya kuajiri. Ushauri wangu na wito wangu, namwomba sana dada yangu na kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Faustine basi mpango huu waweze kuufanya kwa uharaka, ili kuweza kumaliza changamoto hii ya uhaba wa watumishi kwenye Sekta ya Afya katika maeneo mbalimbali, hususan Jimbo la Handeni Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.