Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nakushukuru na namshukuru Mwenyezi Mungu pia kwa kuniwezesha kusimama hapa. Awali ya yote ninaunga mkono Kamati zote mbili Kamati ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wangu nitaanza moja kwa moja na Kamati Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa kuzungumzia kutoa ushauri kwa Shirika la Utangazaji Tanzania TBC.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni-decrare interest kwamba mimi ni Mwanahabari na kabla ya hapo pia nilikuwa TBC. Kwa hiyo ninapozungumzia TBC naizungumzia TBC kwa upendo kwa kutambua changamoto zilizopo katika Shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitakuwa mchoyo wa fadhili endapo sitaipongeza Serikali yangu kwa kazi kubwa wanayoifanya; Mheshimiwa Rais pamoja na Baraza lote la Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Mwakyembe ninakupongeza sana hasa baada ya kuona jitihada kubwa unazozifanya katika kukagua mitambo ya TBC na kuweza kuiboresha pale ambapo ina changamoto. Kwa kiasi kikubwa sana Mheshimiwa Waziri hii itasaidia katika kutatua changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yoyote ile inajivunia Chombo chake cha Habari na TBC ndilo Shirika la Umma. Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inazungumzia uhuru wa kupata habari, lakini vilevile inaendelea mpaka kuzungumzia katika uhuru wa kutoa mawazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo hakuna uhuru usiokuwa na mipaka; hivyo nipongeze sana Serikali pale ambapo inasimamia kikamilifu kuhakikisha kwamba Vyombo vya habari vinafuata maadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC ni Shirika kongwe, na tunafahamu Shirika hili la Utangazaji Tanzania (TBC) liliendelea kutumia majengo ambayo yalikuwa ni majengo ya filamu kwa miaka hiyo; na kwa muda mrefu kwa kweli limekuwa likihitaji marekebisho na mabadiliko makubwa hasa katika mitambo pamoja na mazingira yenyewe kwa ujumla, lakini hasa mitambo. TBC bado inahitaji uboreshwaji mkubwa wa mitambo ili basi kiweze kuwafikia wananchi kwa ukaribu zaidi pasipo kuwa na hizo changamoto, na hata kama zitakuwepo basi changamoto ziwe ni chache.

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi najivunia Shirika hili la Utangazaji Tanzania na pamoja Mkurugenzi wa TBC, Bwana Ayoub Ryoba kwa jitihada kubwa wanazozifanya. Wafanyakazi hawa wa TBC ni Wafanyakazi ambao kwa kweli wanahitaji pongezi hasa kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli ulio wazi maeneo yote katika ziara zote za Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Jemedari Dkt. John Joseph Pombe Magufuli TBC tumekuwa tukiwaona wakituhabarisha kile kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kweli nimpongeze aliyekuwa Msemaji wa Serikali Dkt. Hassan Abass kwa kazi kubwa aliyokuwa anaifanya katika kuwahabarisha wananchi nini ambacho Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Serikali, inayoongozwa na Dkt. John Joseph Pombe Magufuli inachokifanya na tumeshuhudia kwa kweli hata wananchi sasa hivi wanamwelewa vizuri sana Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kutokana na kazi kubwa ya Dkt. Abass.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii basi wanasema pengine ndiyo ambayo imempendezesha Rais na kumpa nafasi hiyo. Mimi ninampongeza akaendeleze jitihada hizo hizo katika kuhakikisha kwamba anasimamia misingi ya taaluma hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Serikali, na nimpongeze Spika wetu kwa sababu hivi sasa katika Bunge letu kipindi cha maswali na majibu watu wanafatilia, hata wenzangu viziwi wanafatilia kwa sababu wapo Wakalimali wanaotafsiri lugha ya alama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hao tu, tumeanza vizuri katika taarifa zetu za habari televisheni mbalimbali nazo pia wanafanya kazi hiyo kuhakikisha kwamba hakuna anayeachwa nyuma. Mheshimiwa Waziri na Naibu wako nakupongeza sana kwa hili jambo unalolifanya katika kuhakikisha kwamba tunazingatia na mikataba yote ambayo nchi yetu imeiridhia.

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC hivi sasa wana channel ambayo inatangaza utalii ninaiomba Serikali kuhakikisha kwamba inawawezesha TBC kwa kiasi kikubwa na hata ikibidi kuongeza bajeti ili basi wao ndio wawe wa kwanza katika kutangaza utalii wetu hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi pia ni mjumbe wa Kamati ya Masuala ya UKIMWI, TB bado ni tatizo kubwa hapa nchini; kwa mwaka watu zaidi ya 75,000 wanakufa kutokana na ugonjwa huu wa kifuu kikuu. Niiombe Serikali kuhakikisha kwamba jitihada zinaongezwa ili kuweza kunusuru wananchi wa Tanzania wengi wasiangamie na ugonjwa huu wa TB.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia elimu iendelee kutolewa na tulishirikishe Shirika letu la Utangazaji Tanzania (TBC) kutoa elimu juu ya madhara gani au nini basi hasa chanzo cha ugonjwa huu ili wananchi waweze kufahamu na vilevile kuchukua tahadhari.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tulipitisha sheria kuhusiana na upimaji kwa watoto chini ya miaka kumi na nane mpaka kumi tano; ninaiomba Wizara iharakishe kanuni na pia kutoa elimu ili wazazi watambue umuhimu wa kuwapima watoto wao hasa chini ya miaka kumi na nane mpaka kumi na tano ili basi malengo ya 90 90 90 yaweze kukamilika na kufanyiwa kazi kwa jitihada kubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumekuwa tukitegemea sana vyanzo au wafadhili kuhusiana na ugonjwa wa UKIMWI; sasa ni wakati wa Serikali; naishauri Serikali kuhakikisha kwamba tunapata vyanzo vya uhakika vya kuweza kutunisha mfuko wa UKIMWI ili basi tuweze kujitegemea angalau kupunguza misaada mikubwa ambayo kwa wakati mwingine kwa kweli tunapata misaada hiyo kutokana na masharti magumu. Kwa hali ilivyo kwa sasa hivi kwa kweli tuharakishe mfuko huu na kwa kupata vyanzo katika bajeti ya mwaka huu ili basi tuweze kupunguza misaada kutoka kwa wafadhili wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda umekwisha ninakushukuru sana kwa kweli, naipongeza Serikali tena Mheshimiwa Harisson Mwakyembe na Naibu wako hongereni sana. Vilevile Mheshimiwa Ummy Mwalimu Mungu akubariki sana, A luta continua mapambano yanaendelea, ahsante sana. (Makofi)