Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja hizi mbili zilizopo mezani kwa siku ya leo. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa fursa ya kuendelea kuwa uhai, lakini pia niwapongeze sana wenyeviti wote wawili Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii lakini pia Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Masuala ya UKIMWI Dkt. Tiisekwa; nawapongeza sana kwa kazi nzuri waliyofanya. Kwanza wanatusimamia vizuri kwenye Kamati zetu lakini leo wamewasilisha vizuri sana Taarifa za Kamati mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze na jambo moja, nianze na suala la elimu. Kwenye elimu tunahangaika sana juu ya suala la walimu, hali ya walimu ni mbaya sana, na sielewi kabisa kwamba sasa Serikali inajipangaje kwa sababu shule zetu hazina walimu, ni tatizo la Kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi pia ni mjumbe wa Kamati ya LAAC ukiangalia Taarifa za Mkaguzi wa Mahesabu ya Serikali unaona kabisa kwamba anaonesha mapungufu kwamba katika kila Halmashauri kuna upungufu mkubwa sana wa walimu na tatizo likishakuwa kubwa sana halafu ukawa huwezi kulitatua inafika mahali unaliona hili huliwezi unaamua kuliacha tu liendelee kama lilivyo na unalizoea unaona kama ni hali ya kawaida. Ni hali mbaya sana. Kwa mfano tu kwenye Halmashauri yangu ya Mji Njombe ina upungufu wa walimu mia nne. Niombe sana Serikali iangalie ni kwa namna gani itafanya iajiri walimu wa kutosha ili kusudi shule zetu pamoja na kwamba wananchi wanachangia ujenzi wa shule, Serikali inachangia nguvu za wananchi pia lakini kama hakuna walimu katika shule za msingi kama hakuna walimu wa sayansi itakuwa ni tatizo kubwa sana kwa maana watoto hawa hawatapa elimu iliyokusudiwa (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine tunahitaji vijana wetu wapate ujuzi; hawa vijana hawawezi kupata ujuzi kwa namna yoyote ile kwa sababu leo hii katika nchi yetu hakuna chuo kinachotoa walimu wa ufundi; hatuna chuo hata kimoja kinachotoa walimu wa ufundi. Watu wengi tunapenda vijana wapate elimu ya ufundi lakini ni ukweli usifichika kwamba hakuna chuo hata kimoja. Kuna chuo kidogo sana cha VETA pale Morogoro na hakina uwezo hata kidogo wa kutoa walimu wa ufundi; lakini vilevile mitaala ya ufundi inayofundishwa ni mitaala ya zamani sana. Mimi ni fundi, kwa hiyo ninajua nini kinafundishwa huko. Kwa kweli ufundi ulipofikia leo na ufundi wanaofundishwa vijana ni vitu viwili tofauti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niishauri Serikali ijitahidi sana kuhakikisha kwamba sasa inajenga vyuo na inafundisha walimu wa ufundi wa kutosha ili kusudi tutakapotaka kuwa na mafundi walimu wa kuwafundisha wawepo. Tutakaa tunasema tunahitaji ufundi VETA zianzishwe lakini walimu wako wapi? Walimu hakuna. Nchi hii hakuna vitabu vya ufundi vinavyoandikwa, havipo. Sisi tunataka mafundi lakini nchi hii vilevile hakuna mitaala ya ufundi ya kisasa, yaani hakuna; mitaala iliyopo ni ya kizamani sana. Kwa hiyo niombe sana Serikali iangalie kadri inavyowezekana na hasa hasa Wizara ya Elimu ijikite kuliona hilo; ni jambo gumu zito lakini ni la muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na wasaidizi wake Mama Jenista, Mheshimiwa Mavunde na Mheshimiwa Ikupa. Katika Wizara yao wameweka utaratibu wa kutoa ujuzi; ni utaratibu mzuri na vijana wengi wanapelekwa maeneo mbalimbali ili kupata ujuzi. Wengi hatuyajui hayo lakini kwa kweli ukiuona ule mpango umeinua vijana wengi na umewawezesha vijana wengi kupata ujuzi. Ni mpango mzuri unaosaidia sana katika kuhakikisha kwamba sasa Vijana wengi wanapata fursa kupata ujuzi. Niwaombe muendelee na kazi hiyo muimarishe zaidi lakini mpanue, msiende tu kwenye fani zile zile za useremala, ujenzi, ushonaji. Haiwezekani nchi nzima ikawa ya mafundi seremala na washonaji, tuweke na fani nyingine, twende kwenye fani za kilimo, uvuvi na mifugo ili sasa vijana hawa watawanyike sehemu pana zaidi ili wakatumie ujuzi huu na hivyo uweze kuwasaidia kuweza kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la elimu liko jambo moja baya sana. Serikali imetoa mitaala mipya, Serikali ina ruzuku ambazo zinatakiwa ziende shuleni; haipeleki zile ruzuku badala yake inapeleka ku-print vitabu Taasisi ya Elimu iki-print vile vitabu inaviandika kitabu hiki hakiuzwi na vile vitabu vinapelekwa moja kwa moja shuleni na kwa hiyo shule zisizo za Serikali zote hazipati vitabu. Sasa unajiuliza, hivi hawa wanaosoma shule zisizo za Serikali ni watoto wa nani? Hawa si Watanzania? Hakuna fursa hata chembe ya shule isiyo ya umma kupata kitabu kilichoko kwenye mtaala wa kisasa. Kwa hiyo niombe sana hilo Serikali ilione na ilitatue hilo tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tulipitisha hapa Sheria ya fedha, kwamba tozo kwenye shule zisizo za umma inayofanana ya fire isiwepo; lakini mpaka leo fire bado wanatoza; hivi mimi najiuliza sheria na waraka ni nini kikubwa? Maana wao wanadai hawajapelekewa waraka. Niwaombe wahusika, watu wa Wizara ya Elimu, wati wa Wizara ya Mambo ya Ndani waambieni hawa Askari wa Zimamoto sheria inasema usitoze fire kwenye Shule zisizo za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie suala la UKIMWI. Tunalo tatizo kubwa la UKIMWI katika nchi yetu lakini tatizo tunavyoliendelea ni kama vile si letu. Hatuna mfuko imara kama nchi kwa ajili ya kukabiliana na UKIMWI tunategemea fedha za wafadhili; na fedha hizi za wafadhili zina masharti mengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, MheshimiwaWaziri wa Fedha yupo, niombe sana sasa hivi ndiyo tunaandaa bajeti kwa ajili ya mwaka ujao tuhakikishe tunaweka kifungu cha Mfuko kwa ajili ya UKIMWI ili kusudi kama nchi tuweze kuwa na fedha yetu kwa ajili ya matatizo ya suala la UKIMWI; vinginevyo hawa wafadhili wakiondoka, na wanavyotuyumbisha itafika mahala tutashindwa kabisa kuhudumia wagonjwa wa UKIMWI. Hawa wafadhili muda wanaokatiza shughuli, kwa mfano kuna taasisi moja ilikuwa inafanya huduma ya UKIMWI katika Mkoa wa Njombe JHPIEGO mkataba umekwisha.

Sasa katika kipindi kile ambacho mkataba umeisha na wenyewe hawana fedha za kuendelea kuhudumia, wale wanufaika wa ile huduma sasa hawapati; na kwa sababu hakuna fedha ya Serikali ya kufidia pale kwa hiyo wale watu wanakuwa hawapati huduma inayostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa Serikali, kwa kuwa sasa tunakwenda kwenye kikao kijacho ambacho kitakuwa ni cha bajeti; na sasa hivi ndiyo maandalizi yanafanyika tuanzishe Mfuko wa Nchi kwa ajili ya huduma ya UKIMWI kwa wananchi. Vilevile niombe sana wananchi wote wajitahidi kupima na Serikali ihamasishe upimaji. Watu wengi wanaogopa kupima ni uoga tu lakini tuhamasishane tupime ili kusudi tuweze kupata tiba ya UKIMWI kwa maana ya kupata tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)