Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa siku ya leo kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na uwezo wa kuchangia leo. Naomba kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri ya kuleta maendeleo anayofanya na hasa katika masuala ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Pia kwa nia yake ya dhati ya kuleta mabadiliko na pia kuleta ndege za shirika letu la ndani ya usafiri wa anga (ATCL) kuboresha na kutangaza utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wataalam wote Wizarani na pia taasisi zilizo chini ya Wizara hii. Pia Wakurugenzi wa TANAPA na NCCA kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri katika maeneo machache ili kuboresha Sekta hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza naomba Wizara hii ifuatilie kwa karibu kutatua migogoro baina ya hifadhi, jamii na watumiaji mbalimbali wa ardhi. Babati tuna hifadhi mbili ambazo tuna tatizo la mipaka, Tarangire ikiwa na Vijiji vya Ayawayo, Gedamar na Gidejabung. Wananchi walipewa fidia ya majengo yao (au maendelezo) kabla ya miaka zaidi ya kumi na waliahidiwa ardhi mbadala sababu hao wananchi walipelekwa hapo na operation vijijini ekari 17,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni la miaka mingi sana, tunashauri eneo hilo wapewe wananchi kwa ajili ya ufugaji jambo ambalo litaendana na uhifadhi. Pia tuna eneo la Ziwa Manyara (hifadhi) ambapo pia kuna mgogoro na Vijiji vya Mayoka, Moya na Manyara.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni eneo kubwa la Babati, Monduli, Kondoa, lipo kwenye eneo la hifadhi ya wanyamapori (game controlled area) ambapo zamani shughuli za kibinadamu zilikuwa zinawezekana. Kwa marekebisho ya Sheria ya 2009, shughuli zote za kibinadamu ilikuwa makazi, kilimo, uvuvi, ufugaji haziruhusiwi kufanyika tena ila sheria ilitaka Waziri ndani ya miezi 12 atangaze maeneo ya game controlled area na nyingine zitolewe kwa wananchi. Tuna mkinzano wa Sheria ya Ardhi, ya Wanyamapori, WMA, Madini na nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye game controlled area ya eneo la Babati na wilaya za jirani pia tuna WMA ya Burunge. Sheria ya Madini inamruhusu Waziri wa madini kutoa leseni ya kuchimba madini ndani ya hifadhi ambayo ni tatizo.

Tunaomba Wizara itusaidie kutatua mgogoro wa WMA Burunge na jamii ya kifugaji wameondolewa kwa nguvu katika maeneo yao na kupewa maeneo ya makazi tu ya ekari tatu kila mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nishauri Serikali itekeleze suala la Blueprint. Utalii wetu haukui sababu kubwa ikiwa ni ada, tozo, kodi na ushuru mkubwa ambao unafanya utalii wetu kuwa ghali (expensive destination) na pia uongozi wa masuala ya utalii. Binafsi TATO wameomba pawe na one stop centre kulipia leseni, tozo, ada na ushuru pamoja wakati mmoja kupunguza gharama. Nashauri Serikali iwekeze kupeleka nishati katika geti la Tarangire, Sangaiwe na Mamire pamoja na barabara ya lami ili kupunguza gharama za ukarabati wa kila wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri kila hifadhi ilipe fidia au kifuta machozi na kifuta jasho badala ya Wizara ambayo inachelewesha kutokana na bajeti ndogo na hizo hifadhi zikilipa hiyo fidia watafanya kazi ya kuhakikisha wanyama hawatoki nje ya hifadhi kila wakati. Naomba Wizara iharakishe kulipa deni hilo kuanzia 2011 hadi sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara iwekeze zaidi katika TFS, Kitengo cha Nyuki na pia Wakala wa Miti Taifa. Tukiwekeza hapo zaidi kwa rasilimali watu, fedha na elimu kwa uma, sekta hii inaweza kuchangia zaidi katika pato la Taifa na pia uchumi wa wananchi. Naomba pia nishauri Serikali ibaki na msimamo wake wa kutoruhusu biashara ya wanyama hai. Nashauri tuwe na marufuku ya kudumu (total ban).

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri pawe na uratibu ndani ya Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji kuangalia namna ya kila Wizara kuwekeza kuboresha maeneo muhimu ya miundombinu, nishati, maji, mawasiliano, uwekezaji ili kukuza utalii katika maeneo mbalimbali nchini, utalii wa ndani na nje. Pia Wizara ya Fedha na Wizara nyingine kupunguza kodi, tozo, ada na ushuru kulingana na kukuza biashara ya utalii (coordinate efforts).

Mheshimiwa Naibu Spika, utalii pekee unaweza kufanya Serikali yetu ipate kipato kikubwa bila kugusa rasilimali zetu nyingine kama madini. Bidhaa za misitu kama mbao na magogo hadi tutakapokuwa tayari kama nchi kuvuna wenyewe. Hongereni kwa kazi nzuri na tunawatakia kila la kheri.