Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi na mimi nichangie hoja hii iliyoko mble yetu.
Kwanza kabisa, napenda kuanza kutoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Joseph Pombe Magufuli kwa imani kubwa kabisa aliyoonyesha kwangu kwa kuniteua kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania na kuniteua kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Rais kwamba nitaifanya kazi aliyonipa kwa moyo wa dhati kabisa na nitawatumikia wananchi, Watanzania wenzangu katika sekta hii ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingi zimezungumzwa katika Wizara yangu, lakini kwa sababu ya muda nitazungumzia tu chache. Napenda kuanza kuzungumzia suala la elimu bila malipo ambalo mwenzangu wa TAMISEMI amelizungumzia, lakini ningependa kuongezea tu jambo dogo katika kutoa ufafanuzi kwa sababu umejitokeza mkanganyiko kwamba Serikali inabagua baadhi ya watoto; wengine wanapewa chakula na wengine hawapewi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kusema kwamba usajili wa shule uko wa aina mbili na Wizara yangu ndiyo inayofanya usajili wa shule. Tuna shule za kutwa na shule za bweni. Shule za bweni zina vigezo vyake. Tunatambua kama alivyosema Waziri wa TAMISEMI kwamba kuna baadhi ya shule za kutwa ambazo zimewekewa hostel kwa sababu maalumu. Sasa zile haziko katika utaratibu wa sasa wa wanafunzi kupatiwa chakula kwa sababu usajili wake ni shule za kutwa na sio shule za bweni. (Makofi)
Kwa hiyo, nami narudia kuwaomba Wakurugenzi wote wa Halmashauri, kama kuna shule ambayo ilisajiliwa kama shule ya kutwa lakini inakidhi vigezo; kwa sababu vigezo vipo ili shule iweze kuwa ya bweni. Ina vitu vingi ambavyo wanapaswa kuzingatia. Basi kama wamekidhi vile vigezo, waje Wizarani tuwabadilishie usajili. Ili waweze kupata chakula, lazima iwe ni shule ya bweni na siyo vinginevyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa shule ya kutwa kwa sababu inahesabika kwamba mwanafuni anakuja shuleni na kurudi nyumbani, kwa hiyo, lile jukumu la chakula bado ni jukumu la mzazi kwa sababu mwanafunzi anaishi nyumbani kwa mujibu wa usajili shule husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimeona hilo jambo pamoja na maelezo mazuri ambayo aliyasema, nizungumzie kwa sababu ni suala la kisera.
Kwa hiyo, shule iliyosajiliwa kama shule ya bweni inapata chakula, shule iliyosajiliwa kama ya kutwa katika mwongozo ambao tumeutoa mzazi ataendelea kuchangia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia kidogo suala ambalo limejitokeza kuhusiana na malalamiko kwamba ada kubwa. Hii imejitokeza hata katika hotuba ya Mheshimiwa Rais kwamba mojawapo ya kero ni ada kubwa zinazotozwa na shule binafsi. Naomba tu niseme kwamba Wizara yangu tayari inalifanyia kazi suala hilo na tunajaribu kuja na ada elekezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba hili suala la ada elekezi linahitaji kufanyiwa kazi kwa kina na kuangalia vizuri shule zetu, kwa sababu shule ziko katika makundi mbalimbali. Unaweza kukuta zile huduma au facilities ambazo zinapatikana shuleni zinatofautiana sana. Kuna shule nyingine mpaka zina swimming pool, zimejengwa kwa terazo, nyingine zimejengwa kwa tiles au kwa marble, sasa unapokuwa unatoa ada elekezi, ni lazima pia uzingatie kwamba mwanafunzi anasoma katika aina gani ya shule.
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo shule nyingine za binafsi ambazo hazina hata sakafu. Kwa hiyo, huwezi kuja na ada elekezi ukasema tu kwamba ni shilingi kadhaa. Ni lazima haya mambo yote uyaangalie. Hata chakula wanachopewa wanafunzi kinatofautiana. Baadhi ya shule wanapewa mpaka sausage, wanakula pilau na wengine wanakula ugali na maharage kila siku. Huwezi ukaja na ada elekezi ambayo ni uniform. (Makofi)
Kwa hiyo, Wizara yangu lazima iliangalie hili jambo kwa umakini mkubwa sana. Tutaangalia mpaka mishahara wanayolipwa walimu. Kuna baadhi ya shule zinawaonea walimu inawapa mishahara kidogo.
Kwa hiyo, naomba Watanzania tuwe na subira, Wizara yangu inalifanyia kazi hili jambo, lakini siyo jambo ambalo linahitaji kufanya kazi kwa haraka. Tutakapokuwa tayari, tutakuja kuwapa majibu. Tutakapokubaliana, kwa sababu tunafanya kwa kina na tuna mtaalam mshauri, tutaweka class za shule kwa vigezo mbalimbali ambavyo tutavitambua, basi tutakapokuwa tumekamilisha, naomba tukubaliane na hiyo ada. Nashukuru sana. (Makofi)