Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri. Napenda kuchangia katika suala zima la nyumba za Walimu hasa wale wanaoishi vijijini.
Pia ujenzi wa vyumba vya madarasa ya sekondari na msingi hasa ukizingatia katika Wilaya ya Lushoto kuna maeneo mengi vijijini hayana shule kabisa. Watoto wanatoka zaidi ya Kilometa 20 hadi 25. Wakati wa mvua nyingi watoto hawa hawaendi shule mpaka mvua itakapopungua.
Naiomba Serikali yangu Tukufu ijenge shule kwenye maeneo hayo, mfano Lushoto Makanya Kagambe, Mazumbai, Ngindoi, Muheza na Mlola.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Walimu wetu wanapata mishahara midogo sana ambayo haikidhi haja zao. Naiomba Serikali yangu Tukufu iangalie jinsi gani ya kuwaongezea mishahara Walimu wetu hawa. Pamoja na stahiki zao, walipwe kwa wakati hasa hizi za uhamisho. Sambamba na hayo, makato ya Walimu yamekuwa mengi. Naiomba Serikali yangu ipunguze makato hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la vitabu mashuleni pamoja na miundombinu kwa ujumla. Pia Walimu hawa wapandishwe madaraja kwa wale wote wanaostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala la VETA ni suala ambalo lipo kwenye ilani, kila Wilaya iwe na VETA. Wilaya ya Lushoto ni miongoni mwa Wilaya ambazo hazina Chuo cha VETA. Naiomba Serikali ikafungue chuo cha VETA Lushoto na kwa bahati nzuri kuna majengo ambayo yako tayari, kwani ni kuongea na TAMISEMI wawape majengo waliyoyaacha na kuhamia kwenye jengo lao jipya. Nia na madhumuni ni kusaidia vijana wetu hawa ambao hawakuweza kuendelea na masomo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naishukuru Serikali yangu kwa kutoa mikopo kwa wanafunzi hao, lakini wanafunzi hawa wanapomaliza vyuo, Serikali haiwapatii ajira vijana wetu hawa. Hapo hapo Serikali inatangaza wote ambao wamesoma Vyuo Vikuu kwa mikopo wanatakiwa warejeshe mikopo hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe binafsi najiuliza, vijana hawa bado hawajapata kazi na huu mkopo wataurudishaje? Naiomba Serikali yangu Tukufu iwapatie Vijana hawa ajira ndiyo waanze kulipa mikopo hiyo. Pia Serikali ijue ya kuwa kuna kundi kubwa sana la vijana ambao wapo mtaani hawana ajira. Kwa hiyo, ni muhimu sana kujenga vyuo vya VETA vijana wetu wakimaliza waweze kujiajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri aniangalie kwa jicho la huruma aniletee Walimu wa sayansi. Mungu akubariki mama yangu Mheshimiwa Profesa Ndalichako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anitembelee katika Wilaya ya Lushoto.