Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kuchangia hotuba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Ufundi kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu bure ukweli kabisa sera hii imezibagua shule za Kata za kutwa na zile shule za Serikali ambazo zinahudumiwa kwa chakula kwa mabweni yaliyojengwa na wananchi na watoto/wanafunzi kukaa bweni wakati shule hizo bado zinaitwa za kutwa na hawapewi fedha za kununuliwa chakula kutoka nyumbani.
Hivyo ni vema suala hili likaangaliwa upya namna ya kusaidia shule hizo zenye mabweni zipewe chakula kama nyingine za Serikali. Wapiga kura wetu wanapiga kelele juu ya ubaguzi huo wa shule za bweni za wananchi hivyo kuongeza mzigo wa michango ya chakula. Shule hizo ni nyingi sana zilizopo kwenye Kata mbalimbali nchini kuliko shule za Serikali za bweni mfano Semeni, Likumbule, Wamasakata, Walasi, Malumba na Mbega Mchiteka Wilayani Tunduru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo ya posho za likizo za Walimu na madai ya zabuni mbalimbali. Kuna madai mengi hawajalipwa walimu katika shule mbalimbali kutokana na posho za likizo, uhamisho na posho nyingine mbalimbali. Kuna chuo cha maendeleo Nandembo watumishi wanadai 7,164,000 na wazabuni wanadai 5,447,000 na wametishia kusitisha kutoa huduma zao na kuna mtumishi mmoja Saidi Salanje alifariki mwaka 2011 lakini warithi wale hawajapata mafao yao ya kiinua mgongo mpaka leo hii. Ni vema madai hayo yakashughulikiwa mapema ili kuondoa malalamiko na kero zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kukarabati shule za sekondari za Serikali, majengo ya shule za sekondari Tunduru, masonya na Frank Wiston zilijengwa muda mrefu zaidi ya miaka 30 iliyopita lakini hakuna ukarabati wowote uliofanyika katika majengo na yanatishia usalama wa wanafunzi na walimu wao. Hivyo, tunaomba majengo hayo yafanyiwe ukarabati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa walimu wa shule za msingi na sekondari; Kuna upungufu mkubwa sana wa walimu wa sekondari hasa wa sayansi karibu shule zote za sekondari zilizopo Tunduru na walimu wa shule za misingi takribani mia tano jambo ambalo linashusha kiwango cha ufaulu wa watoto wetu katika masomo ya sayansi. Tunaomba tupewe kipaumbele cha kupewa walimu katika ajira ya mwaka 2016/2017 ili kupunguza pengo hilo na mwaka 2015/2016 hatukupewa hata mwalimu mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vya kufundishia tunaomba Serikali kuliingilia kati suala la vifaa vya maabara ili watoto/wanafunzi wajifundishe kwa vitendo badala ya kuwaachia Halmashauri zetu, kwa sababu uwezo wa Halmashauri nyingi kupata vifaa hivyo kwa kutumia mapato ya ndani ni mdogo sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuboresha walimu kimasomo. Tunaomba Serikali itoe fursa kwa walimu wa vijijini kujiendesha kielimu ili kuwapa motisha wa kazi zao za kila siku. Ni vema kuimarisha vyuo vya Ualimu ili kupewa elimu na ujuzi wa kufundishia.