Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia. Kwanza kabisa napenda kutoa shukrani zangu kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma aliyetuwezesha kufika siku ya leo na kuniruhusu mimi kusimama hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri kwama utekelezaji wa Mpango unahitaji fedha, na viko vyanzo vingi ambavyo vimeainishwa lakini moja kati ya chanzo ni mapato yetu ya ndani. Hivyo kwasababu dhima ya mpango inasema vyema kabisa, ni kujenga uchumi shindani wa viwanda kwa maendeleo ya watu. Kwa hiyo imani hapa ni kwamba fedha zikipatikana za kutosha za kutekeleza mpango huu tutakwenda kuifikia dhima hii. Nataka nichukue fursa hii kipekee kabisa kuuenzi mchango mzuri sana wa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwenye suala zima la upatikanaji wa mapato ambayo naamini pia Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan pia atauendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika kuishauri Serikali kuongeza wigo wa kodi (tax base). Duniani kote hivi sasa nchi nyingi zinaelekea katika mfumo wa kodi ya huduma za kidigitali, wanaita DST ni Digital Service Tax. Kwa mujibu wa Jarida la Statista la mwaka 2019 hivi sasa duniani kuna watumiaji wa mitandao ya kijamii zaidi ya bilioni 3.6 ambao katika nchi zinazoendelea kule Ulaya wameanza na utaratibu huu, wameanza kuweka miundombinu ya kuwafanya walipe kodi na kodi hii imeanza kuchangia kwa kiasi kikubwa sana katika uchumi wa nchi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ninavyozungumza hivi sasa nchi ya Ufaransa wameshakamilisha taratibu zote na sheria ya kutoza 3% halikadhalika Hispania na yenyewe wanatoza 3% na Uingereza 2%, huu ni utaratibu ambapo kama nchi pia lazima tuangalie hili eneo halijaguswa kabisa. Kwa Afrika nchi ambayo imeanza kulifanyia kazi jambo hili ni nchi ya Afrika ya Kusini. Afrika ya Kusini wameunda mpaka Tume chini ya PBO (Parliamentary Budget Office) ya Bunge la Afrika ya Kusini ya kuhakikisha kwamba wanapitia na kuona namna ambavyo watawatoza kodi hasa hawa main players wa kwenye social networks. Hapa nazungumzia search engines kama Google, Amazon, Spotify, huku kuna hela nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), kifungu cha 47 kimetoa ruhusa ya nchi yetu pia kutengeneza mifumo ya kukusanya kodi kupitia utaratibu huu. Nimuombe Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Mwigulu Nchemba twendeni tukaliangalie eneo hili, lina hela nyingi sana, badala ya kuendelea kuhangaika na bodaboda na vyanzo vingine twendeni huku kuna hela nyingi ambayo imelala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni maeneo mawili; la kwanza, tutengeneze payment platform ambayo itaifanya TRA iweze kutoza kodi. Hivi sasa tukinunua vitu kupitia kadi yetu ya Visa, Mastercard au PayPal pale TRA wana uwezo wa ku-capture tax wakifanya integration. Kwa hiyo, mfumo huu uwekwe vizuri na naamini kabisa ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu una uwezo wa kulisimamia hili likaongeza wigo wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo nataka niwapongeze wameanza kulifanya, tukae na main players hawa Facebook, YouTube. Najua mmeanza na Facebook na Facebook kwa takwimu za mwezi Februari wana watumiaji zaidi ya bilioni 3.1 ulimwengu mzima na sisi Tanzania pia tukiwemo humo ndani. Mimi naamini kabisa hili liko ndani ya uwezo na tukilisimamia vizuri tutaongeza mapato kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kwenye kilimo, bado naendelea kuamini kwamba sekta hii ina mchango mkubwa sana kwenye uchumi wetu hasa katika kilimo cha umwagiliaji. Hivi kwa nini tusiwe tuna miradi ya mkakati kwenye kilimo pia kama ilivyo katika maeneo ya miundombinu na uchukuzi, twendeni tukafanye haya kwa sababu naamini kabisa kilimo kina uwezo wa kutupeleka mbele zaidi kama sekta kiongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ameyavalia njuga sana yale mazao ya kimkakati lakini tumuongezee nguvu pia katika eneo hili. Rai yangu ni kumuomba kaka yangu Mheshimiwa Prof. Kitila na rafiki yangu Mheshimiwa Mwambe mkae pamoja na sekta binafsi ili tutengeneze soko la uhakika la wakulima wetu, kuwepo na backward and forward linkage, mkulima anayelima nyanya aunganishwe na kiwanda moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri Hussein Bashe amewahi kufanya kikao na Bakhresa nafahamu lakini tulikaa naye pamoja pia kwenye suala la ukwaju tu kwa sababu Bakhresa hivi sasa anaingiza mtambo wa kiasi cha shilingi bilioni 20 kwa ajili ya ukwaju tu lakini ukwaju huu ni wa kuutafuta. Sasa Serikali ndiyo sehemu ya ku-take advantage hapa kwa wakulima wetu, twendeni tukaweke mkazo hapo kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumze kuhusu zabibu, zabibu ndiyo dhahabu yetu Dodoma. Zabibu ya Dodoma nitaomba Wizara ya Kilimo itusaidie kufanya utafiti lakini inasemekana hakuna nchi yoyote duniani yenye uwezo wa kuvuna zabibu mara mbili isipokuwa Tanzania na yenyewe ni Dodoma tu. Serikali kupitia Wizara ya Kilimo iweke mpango mkakati madhubuti kulisaidia zao hili la zabibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatamani kuwatua akina mama wa Dodoma mabeseni yao ya zabibu ambayo wanauzia stendi wakatengeneze mchuzi wa zabibu badala ya kuhangaika kukaa kwenye jua Serikali ikawasaidia wakatengeneze mchuzi wa zabibu. Tunaishukuru sana Serikali imeshusha tozo ya mchuzi wa zabibu kutoka Sh.3,655 kwa lita mpaka Sh.450 hali ambayo imechochea sana ulimaji wa zao la zabibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikuombe Mheshimiwa Bashe, najua unafanya kazi nzuri sana, umeshaunda Kamati ya watu 12 kuhusiana na zao hili la zabibu twendeni mbele Zaidi. Natamani kuiona Tanzania inasifika kwa zabibu maana ndiyo zao pekee linavunwa mara mbili duniani unalikuta Dodoma. Nikuombe Mheshimiwa Naibu Waziri kazi ambayo umeianza naomba tuimalizie tuwatue mzigo wakulima wa Dodoma tupate soko la uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa najua tayari wanaendelea na masuala ya tafiti na mnakuja na mbegu mpya, mbegu ya Beauty, Georgina na Alphonse Lavalleé ambazo naamini kabisa zitaongeza tija. Nikuombe sana ndugu yangu na kaka yangu Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na Waziri katika eneo hili tuwasaidie wakulima wa zabibu wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo letu sisi tunataka tuanze sasa kuifanya Afrika Mashariki na Kati hasa Watanzania hapa tuache kuagiza St. Anne na wine zingine kutoka nje ya nchi, zabibu yetu ya Dodoma ndiyo zabibu nzuri na tamu kuliko zote pia ukiacha Italia. Hivyo niwaombe sana Wizara katika eneo hili twendeni tukawasaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini twende mbele Zaidi, Afrika Kusini hivi sasa kupitia zabibu inafanya utalii na imetengeneza ajira zaidi ya 450,000 kupitia mashamba ya zabibu. Mashamba ya zabibu hivi sasa ni utalii na uzuri katika Jiji la Dodoma kwenye masterplan yetu tumetenga maeneo ya kilimo cha mijini (urban farming), tunaomba msukumo wa Serikali. Tunataka tuifanye zabibu iwe sehemu ya kivutio cha utalii, watu waje washangae mashamba ya zabibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu akija Dodoma hapa akutane na kaulimbiu ile ya maneno makubwa kabisa ya Kilatini wanasema: “In vino veritas”, kwamba kwenye wine/mvinyo kuna ukweli, waje waukutie ukweli huo Dodoma. Naamini kabisa ndugu yangu Mheshimiwa Hussein Bashe na Prof. Mkenda mna uwezo wa kulisukuma hili. Tukifanya hili tutakuwa tumewasaidia sana wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, Mheshimiwa Waziri Mkuu alizungumza kuhusu mamlaka ya kilimo bustani (horticulture), alitoa maelekezo hayo. Wizara ya Kilimo anzisheni mamlaka hii, horticulture inakuwa kwa kasi sana hivi sasa, mamlaka ikiwepo itatusaidia sana. Wakulima wa kilimo cha bustani amebaki mtu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)