Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami niweke yangu tena ya muhimu katika hoja hii iliyopo mezani ya bajeti ya Wizara muhimu na uti wa mgongo ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze na suala zima la VETA-Mikumi. Kwa kuwa Chuo cha VETA - Mikumi ndiyo chuo pekee kilichopo katika Jimbo la Mikumi na kwa kuwa ukombozi wa vijana wengi wanaohitimu shule za sekondari zilizopo Jimboni kila mwaka hukosa mwelekeo, hivyo ni muhimu kukipa kipaumbele chuo hicho kwa kukiboresha katika maeneo yafuatayo:-
(i) Kupanua wigo katika fani zinazotolewa ili ziendane na mazingira ya Jimboni, kuongeza fani ya ufundi-kilimo (agro-mechanics);
(ii) Kukiongezea uwezo wa udahili kwa kuongeza idadi ya mabweni hasa kwa ajili ya wasichana ili kuendana na sera ya kuleta uwiano katika udahili kati ya wasichana na wavulana;
(iii) Kuongeza idadi ya madarasa na karakana za kujifunzia, pia kupanua wigo wa mafunzo kwa vitendo; na
(iv) Kuongeza na kuboresha vifaa vya kujifunzia ili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ili kuwajengea vijana uwezo wa kitaalamu unaoendana na mabadiliko yanayotokea sokoni kila wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijikite kwenye changamoto zinazoikabili VETA-Mikumi kama ifuatavyo:-
(i) Baadhi ya watumishi kukaa muda mrefu sana bila kuhamishwa, wapo waliokaa zaidi ya miaka 20, hii inaathiri sana utendaji wa kazi kwa kuwa wanafanya kazi kwa mazoea na ufanisi kupungua;
(ii) Kuna upendeleo katika udahili hasa katika chaguo la pili hivyo kupelekea aidha ndugu wa viongozi au watu wao wa karibu kujaza nafasi hizo huku wananchi wazawa wa Mikumi wakikosa fursa hiyo. Katika udahili mwaka wa masomo 2016, wananchi wa Mikumi waliopata fursa ni asilimia 10 tu ingawa tunatambua kuwa usaili huwa unajumuisha waombaji kutoka kila kona ya nchi lakini vijana wa Mikumi walipaswa kupewa kipaumbele hasa katika chaguo la pili;
(iii) Kuwepo kwa uongozi usiofuata tararibu, kanuni za utumishi wa umma na utawala bora. Uongozi wenye mfumo kandamizi usiokubali kufanya kazi na watu waadilifu, uongozi unaofanya ubadhirifu na maamuzi yasiyokuwa na tija kwa VETA na Taifa kwa ujumla;
(iv) Chuo kimepeleka mini-bus kwa matengenezo Dar es Salaam zaidi ya wiki moja katika gereji bubu katika kipindi cha mwezi Mei 2016 bila kufuata taratibu za manunuzi. Pia kukiuka maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kupeleka magari yote ya umma kwa matengenezo TEMESA;
(v) Uongozi wa chuo (Afisa Rasilimali Watu na Mkuu wa Chuo) kuwa na mtandao mpana kuanzia VETA-Makao Makuu wa kuwakataa, kuwapinga na kuwahamisha watumishi wanaonekana kutokubaliana na mawazo yao ya kibadhirifu.
Kwa mfano Salum Ulimwengu (Mratibu Mafunzo) aliyekaa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhamishiwa Arusha baada ya kuvutana na menejimenti baada ya Mkuu wa Chuo kukiuzia chuo gari bovu lililokuwa likimilikiwa na rafiki yake, pamoja na ununuzi wa spea hewa za magari ya mafunzo. Suala hili lilichunguzwa na ofisi ya CAG na hakuna ripoti yoyote iliyotoka. Hata hivyo, uuzwaji wa gari hilo haukuhusisha ofisi ya Afisa Mafunzo ila Kitengo cha Ufundi magari bila kufuata taratibu za mamlaka;
(vi) Kukataa kumpokea na kushindwa kumkabidhi ofisi Mratibu wa Mafunzo kwa kipindi cha mwaka mzima kinyume cha section 3.13 ya VETA Staff Regulations and Conditions of Service ambayo inatamka kuwa mabadiliko yoyote ya kiutumishi lazima yafanyike kwa makabidhiano ya kimaandishi (Rejea Internal Audit Report VETA- Mikumi, March- December 2014);
(vii) Mkuu wa Chuo na Afisa Rasilimali Watu kushinikiza uhamisho ili kulinda wizi wa mali za umma na ubadhirifu. Mfano mwingine, Msuya (Stores Officer) aliyekaa kwa kipindi cha mwezi mmoja na kupelekwa Morogoro. Joseph Riganya (Stores Officer) aliyevutana na uongozi wa chuo na kuhamishiwa Ofisi ya Kanda kwa kisingizio cha matibabu. Riganya alipinga ukiukwaji wa Sheria ya Manunuzi na ubadhirifu katika manunuzi unaofanywa na Mkuu wa Chuo na Afisa Rasilimali Watu; mfano katika ripoti ya ukaguzi wa ndani (internal Audit report) ya Machi hadi Desemba 2016 inaonyesha kuwa Afisa Rasilimali Watu, Mhasibu na Mwalimu mmoja walipokea vifaa vya thamani ya shilingi milioni 35 kinyume na taratibu kwani Kamati ya Mapokezi ndiyo yenye dhamana ya kupokea vifaa hivyo. Walifanya hivyo ili kulinda maslahi yao binafsi;
(viii) Ukiukwaji wa taratibu za ajira kwa kumpa mkataba Neema Bui ambaye hana sifa na anafanya kazi za manunuzi kwa maslahi ya Mkuu wa Chuo na Afisa Rasilimali Watu kwa kuwa kila Afisa Manunuzi anayeletwa anaondolewa kwa hila ili asizibe mianya ya wizi; na
(ix) Afisa Manunuzi Rogate aliyehamishiwa mwezi Februari 2016 kutoka Tabora amepewa vitisho kwenye kikao cha menejimenti na sasa anafanya mpango wa kuhama kuwapisha wanaojiita wenye chuo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu ni kama ifuatavyo:-
(i) Kuwasimamisha kazi Afisa Rasilimali Watu na Mkuu wa Chuo ili kupisha uchunguzi;
(ii) Kuwahamisha watumishi waliokaa muda mrefu sana katika chuo hiki ambao ndiyo chanzo cha kulea ubadhirifu;
(iii) Kuangalia kama ilikuwa halali kumhamisha Afisa Mafunzo, Ndugu Salum Ulimwengu aliyekaa kwa kipindi cha miaka miwili na ambaye amehamishwa mwezi mmoja tu tangu amhamishe mke wake katika Sekondari ya Mikumi, hivyo mtu aliyepigania maslahi ya Taifa kuteswa kisaikolojia na kifamilia;
(iv) Kufanya uchunguzi maalumu juu ya masuala ya manunuzi na fedha katika chuo cha VETA-Mikumi; na
(v) Kufuatilia ilipoishia ripoti ya CAG ya Oktoba 2015 juu ya Mkuu wa Chuo kukiuzia chuo gari chakavu kinyume na maadili ya utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee suala zima la elimu bure ambapo kumekuwa na changamoto nyingi kama ifuatayo:-
(i) Ruzuku inayotoka Serikalini ya kila mwezi haikidhi mahitaji ya shule mfano mpaka sasa Walimu Wakuu hawana fungu la mlinzi, umeme na maji;
(ii) Idadi kubwa ya wanafunzi ukilinganisha na Walimu, madarasa na miundombinu mingine kuna vyoo, madawati na kadhalika;
(iii) Huduma ya chakula shuleni irudishwe ili kuhamasisha watoto waende shule; (iv) Upungufu mkubwa wa Walimu wa sayansi kwenye Jimbo la Mikumi;
(v) Walimu kutolipwa stahiki zao kwa muda mrefu na pia wengi kuchelewa kupandishwa madaraja; na
(vi) Hakuna nyumba za Walimu na pia hawalipwi posho za uhamisho na pesa zao za likizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ni baadhi tu ya changamoto nyingi za elimu kwenye Jimbo la Mikumi na Wilaya ya Kilosa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.