Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa wasilisho zuri na mpango mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo wananchi wa Jimbo la Ludewa wamenituma niombe mambo machache yaweze kufanyiwa kazi kwenye sekta ya barabara za vijijini na sekta ya afya. Kwa kuanzia na barabara za vijijini, mara zote tafiti zimekuwa zikituonyesha kwamba wananchi wengi wa Tanzania wanaishi maeneo ya vijijini na tatizo kubwa ni umaskini ambao unawasumbua. Kwa hiyo, ningependa kumwomba Waziri wa mwenye dhamana Ofisi ya Rais, TAMISEMI aweze kuwaongezea fedha watu wa TARURA ili zile barabara za vijijini ziweze kuboreshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina changamoto kubwa sana kule Jimboni kwangu Ludewa, kuna barabara inaanzia Lusitu inakwenda Madilu, Ilininda mpaka Mundindi; msimu huu wananchi wanatumia gharama kubwa sana kuweza kukodi bodaboda, barabara hazipitiki kabisa. Barabara hii hasa inayoanzia Madilu mpaka Ilininda halijapata matengenezo kwa miaka zaidi ya nane. Wananchi wa Ludewa wamekuwa wakijitolea sana kuchimba hizi barabara kwa majembe ya mkono, lakini wanakatishwa tamaa baada ya kuona Serikali haiwaungi mkono kwa kutenga fedha na kufanya ukarabati wa mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika, kuna eneo la Kigasi – Milo - Ludende mpaka Amani; barabara hii nayo ni muhimu sana, wananchi wa maeneo hayo ni wakulima, wana mazao mengi yanapaswa kupita kwenye barabara hii, lakini ina changamoto kubwa sana msimu wa mvua haiwezi kabisa kupitika. Mwaka huu nimelazimika mara kadhaa kwenda kushirikiana na wananchi kwa ajili ya kwenda kufanya matengenezo. Kwa hiyo, wananchi wanajihisi kama Serikali imewaacha, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri, naomba eneo hili liweze kuangaliwa na barabara hii ipewe fedha na kuweza kutengenezwa kwa kiwango cha changarawe ili iweze kupitika wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna ile Kijiji cha Masimavalafu, kuna Mto Ruhuhu ambapo panahitajika kivuko, ambako inakuwa ni rahisi sana wananchi kwenda Hospitali ya Peramiho kuweza kupata matibabu. Kwa hiyo katika eneo hili tungeomba hata kama kuna kivuko kimeachwa sehemu, tupewe sisi kitusaidie pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia na sekta ya afya; naomba sana hawa wananchi tunaowahamasisha waweze kuwa na hizi bima za afya, wanavyokwenda hospitali waweze kupata dawa na matibabu stahili yanayohitajika. Maana imekuwa ni changamoto kubwa sana, wataalam wanajitahidi kuwahamasisha wananchi wanakuwa na bima za afya lakini hawapati huduma kwa kiwango kile ambacho kinakubalika. Kwa hiyo, naamini sana Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake wote wawili wanaweza wakasimamia eneo hili tukaboresha ili wananchi waweze kuona kwamba Serikali inawathamini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, napenda kushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)