Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge zilizotolewa wakati wa kujadili Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu kwa mwaka wa fedha 2016/2017. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya ambaye kwa kweli tumekuwa tunafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na hata katika kuandaa hii hoja, tumekuwa naye bega kwa bega hadi tarehe 21 ambapo bahati mbaya alipata taarifa za msiba wa mama yake.
Kwa hiyo, nafahamu sasa hivi atakuwa na majonzi mara mbili; anasikitikia kuondokewa na mama yake, lakini anasikitika kwamba hajaweza kuwa pamoja na mimi katika kuhitimisha hoja hii. Naendelea kumpa pole sana na ninamwombea Mwenyezi Mungu aendelee kumtia nguvu katika kipindi hiki kigumu alichonacho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitumie fursa hii kumshukuru kwa dhati kabisa Katibu Mkuu wa Wizara yangu, Bibi Maimuna Tarishi kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Kwa kweli ananipa ushirikiano mkubwa sana katika sekta hii ya elimu ambayo wote mnakubali kuna changamoto. Nawashukuru sana Manaibu Katibu Wakuu, Watendaji wa Taasisi, Wakuu wa Vyuo na Watendaji wote katika Wizara ya Elimu kwa ushirikiano wao mkubwa ambao umeniwezesha hata kusimama kuhitimisha hoja hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Peter Serukamba pamoja na Wajumbe wote wa Kamati hii kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuchambua kwa kina bajeti ya Wizara yangu. Kwa hakika niseme kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu kwamba nimefarijika na nimefurahishwa sana na maoni na ushauri wa Kamati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yao yanaonyesha jinsi gani Kamati yangu imejaa Wajumbe ambao wana weledi mkubwa katika sekta hii ya elimu na wana dhamira ya dhati kabisa ya kuona mabadiliko katika Sekta ya Elimu. Nawashukuru sana na niwaambie tu kwamba mambo yote mliyoyasema tutayazingitia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nichukue fursa hii kumshukuru kwa dhati kabisa classmate wangu Mheshimiwa Suzan Anselim Lyimo, Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani, kwa kuwasilisha vyema maoni ya Kambi ya Upinzani, lakini vile vile kwa ushauri na mapendekezo yake ambayo kama nilivyosema, tunachoangalia ni kuwatumikia Watanzania na kujenga nchi yetu. Kwa hiyo, mapendekezo yote ambayo yana tija kwa Tanzania tutayafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kabisa nirudie tena kutoa shukrani za dhati kabisa kwa familia yangu, mume wangu amekuja kuniunga mkono; lakini pia nashukuru kwamba yupo pamoja na mwanangu, tangu jana wamekuwa na mimi hadi leo ninavyohitimisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishukuru familia yangu yote kwa ujumla, wamekuwa wakinivumlia na wananipa ushirikiano mkubwa. Haya majukumu huwezi kuyafanya vizuri bila ushirikiano wa familia. Naomba mwendelee kunivumilia, kazi iliyopo mbele yangu ni kubwa ili niweze kuwatumikia Watanzania. (Makofi
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa majadiliano ya hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Waheshimiwa Wabunge 16 walitoa hoja zao kuhusiana na Sekta ya Elimu. Aidha, baada ya kuwasilisha hotuba yangu Waheshimiwa Wabunge 60 wamechangia hoja kwa kuongea na Wabunge 61 wamechangia kwa maandishi, ninawashukuru sana Waheshimiwa wote ambao mmechangia katika hoja yangu ama kwa maandishi ama kwa kuzungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwashukuru niwashukuru pia hata wale ambao hawakuweza kupata nafasi ya kuchangia nikiamini kwamba yale yaliyochangiwa na wengine yamewakilisha mawazo yao pia. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba, Wizara yangu itazingatia ushauri uliotolea na Wabunge wote na itafanyia kazi pia mapendekezo yaliyotolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisikiliza kwa makini sana michango ambayo imekuwa ikitolewa, kuanzia kwenye Kamati yangu ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, upande wa Upinzani na kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamezungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kujali itikadi zetu, bila kujali upande gani tumekaa nadhani wote katika hoja yangu tumezungumza lugha moja, tumezungumza lugha moja kwamba, tunataka kuona elimu katika nchi hii inatoa wahitimu wenye ubora, tunataka kuona mazingira ya kujifunzia yako vizuri, tunataka kuona ukaguzi wa shule unafanyika vizuri ili kudhibiti ubora wa elimu.
Tunataka kuona maslahi ya Walimu na stahiki zao zinaboreshwa, tunataka mamlaka za udhibiti wa ubora hizi tunazozipigia kelele TCU, NACTE na ukaguzi zifanye kazi zao vizuri ndicho tunachokitaka, tunataka wanafunzi wenye uhitaji maalum wafanye kazi vizuri na mambo mengine ambayo ziwezi kuyaorodhesha lakini wote kwa kauli moja tumeonesha kwamba, haya ndiyo mambo ambayo Watanzania wanayataka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema ni kuwa Waheshimiwa Wabunge wamekuwa na mambo mengi mazuri ambayo wameyachangia, labda niseme tu pengine kuna sehemu nyingine tofauti tu ni ile aina ya uwasilishaji na lugha inayotumika lakini mimi kimsingi naangalia hoja ile ambayo inawasilishwa na kama nilivyosema yote yatazingatiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kulialifu Bunge lako Tukufu kwamba, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kabisa katika kuboresha na kuinua ubora wa elimu katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimenukuu katika kitabu changu cha bajeti, na hii haikuwa ni bahati mbaya. Nimemnukuu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania maneno yake ambayo aliyatoa katika Bunge hili siku ya tarehe 22 mwezi wa Novemba, wakati alipokuwa analizindua Bunge rasmi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alisema na ninaomba kunukuu “Serikali ya Awamu ya Tano itajielekeza katika kuongeza ubora wa elimu inayotolewa ikiwa ni pamoja na kuongeza mkazo kwenye masomo ya sayansi” mwisho wa kunukuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameongea kwa uchungu sana, tena sana wakielezea masikitiko yao makubwa kuhusiana na hali ya elimu ilivyo sasa hivi nchini kila mmoja wetu hapa anasikitika. Waheshimiwa Wabunge, wanaonekana kutoridhishwa kabisa na ubora wa elimu inayotolewa katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie kwamba, sasa hilo ndilo jukumu ambalo Mheshimiwa Rais amenikabidhi na nina nia ya dhati, ninao uwezo wa kuweza kuhakikisha kwamba elimu yetu inakwenda vizuri. Kwa hiyo tu nianze kwa kusema kwamba, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge wote mniunge mkono katika bajeti yangu ili sasa nikaanze kufanya ile kazi ambayo wote mnahamu kuona ikiwa inafanyika katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekii, ninawahikishia tu kwamba tunayo dhamira ya dhati na nimefarijika kabisa na michango yenu ambayo inaendana na ile kipaumbele chetu ambacho maneno yake nimeyatoa, siyo kama ninasema tu kwa sababu mmechangia lakini hiyo ndiyo kauli na ahadi ya Mheshimiwa Rais. Ninachoweza kusema tu kumbe katika Sekta ya Elimu tulipoweka kipaumbele cha kuinua ubora wa elimu hakika tumelengesha kwa sababu ndipo Tanzania wanapopahitaji. Ningependa tu niseme kwamba, tunaposema kuboresha elimu maana hiyo ndiyo msingi ya hoja zote ilikuwa katika hali halisi ya elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaposema kuboresha elimu maana yake ni nini? Maana yake lazima tujitazame tulipo, tuangalie changamoto tulizonazo na mahali ambapo tunataka kuenda. Niwakumbushe tu maneno aliyekuwa anasema Mheshimiwa Rais wetu katika kampeni zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alikuwa anawaambia wananchi kwamba, akichaguliwa anakuja kuleta mabadiliko ya kweli katika nchi hii. Na mimi naomba Bunge lako Tukufu liniruhusu nifanye mabadiliko ya kweli katika Sekta ya Elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana mturuhusu kufanya mabadiliko ya kweli, kwanini ninasema hivyo. Tumekuwa na utamaduni wa kuwa tunatoa mapendekezo na Serikali inakwenda kufanyiakazi mapendekezo lakini baada ya kufanyiakazi mapendekezo wakati mwingine inakuwa inaonekana kwamba, kunakuwa pengine na maoni tofauti.
Mabadiliko ya kweli yanahitaji mabadiliko ya mfumo, huwezi ukawa na mabadiliko ya kweli wakati mfumo ni uleule na hatuwezi kuwa tayari hapa tulipo kama kweli hatuna dhamira ya dhati ya kufanya mabadiliko katika mfumo wetu wa elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika michango kumekuwa na hoja inayojitokeza kwamba kila Waziri anayekuja, anakuja na mitaala yake anakuja na mabadilikoyake. Kwa hiyo niseme tu kwamba, kama hayo ndiyo yatakuwa maoni kwamba, labda sasa katika sekta yetu ya elimu tubaki kama tulivyo inamaana tukubali kubaki na elimu ambayo wote tunailalamikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, pale inapohitajika mabadiliko tutayafanya lakini tutahakikisha kwamba, tunashirikisha wadau wote muhimu ili kufahamu misingi ya mabadiliko, nafikiri hilo ndilo jambo la msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofanya mabadiliko, mabadiliko hata wanataaluma kuna mtaaluma mmoja ambaye amekuwa anaandika sana mambo ya masuala ya mabadiliko, Profesa Fulani amekuwa anasema kwamba kunakuwa na uwoga wa mabadiliko hilo ni jambo la kawaida, mtu anapotaka kufanya mabadiliko kunakuwa na uwoga. Mabadiliko lazima yawaguse watu, mabadiliko lazima yaguse sehemu ambazo pengine niseme kwamba, zinaweza zikaleta maumivu labda kwa lugha ambayo ni nyepesi. Kwahiyo tukubali tunapokuwa tunayafanya hivyo kwa sababu haiwezekani tukatoka hapa tulipo kama tutabaki kama tulivyo.
Mhesimiwa Mwenyekiti, labda nikitolea tu mfano sasa labda kwanini nimeanza na utangulizi huu mrefu, nimeyasema haya yote kwa sababu ninatambua umuhimu wa kufanya mabadiliko katika sekta ya elimu na kwakweli ndiomana nasema nimefurahishwa sana na michango yote ya Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia katika Wizara hii, michango yote ni mizuri sana yenye afya na yenye tija katika sekta ya elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kuwakumbusha tu kwamba, sasa tunaposema tunafanya mabadiliko tunakubali wote kwamba kuna changamoto, kama kuna changamoto lazima tuwe na mahali pa kuanzia na tunaposema mahali pa kuanzia kwa mfano, nikianza sasa kutoa mifano, tunaposema walimu wawe bora ni dhahiri kwamba, kuna baadhi ya Walimu pengine inawawezekana wakawa wamepita wasiokuwa na sifa ambazo ni stahiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itakapokuwa inachukua hatua za kukagua na kuhakikisha kwamba walimu waliopo wanasifa mtuunge mkono maana kunakuwa na ile ku-symphasize kupita kiasi kwa hiyo mara nyingi tunaonea huruma watu badala ya kuionea huruma nchi na ndiyo matatizo yanakuwa yako mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la wanafunzi wa St. Joseph ambalo limejitokeza sana katika michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi walipokuwa wanachangia hoja yangu. Hili suala nimeliongea kwa kirefu katika hotuba yangu na nirudie tu kusema kwa kifupi ni kwamba, hawa wanafunzi nimesikia michango mingine wanasema kwamba walikuwa wanasifa za wakati huo, mimi kwa kweli sijafahamu ni lini Serikali hii kulikuwa na sifa ya mwanafunzi kwenda kusoma digrii akiwa amemaliza kidato cha Nne akiwa na ufaulu wa D nne. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kuna wengine humu ndani wanafahamu kwa heshima kabisa ili tuweze kwenda vizuri, wanisaidie kwa sababu kuwa Waziri haina maana unafahamu kila kitu, sipuuzi kabisa naheshimu michango ya watu, lakini pengine tuwe tunasaidiana kwa kuonyeshana na lini Tanzania hii tulishawahi kuwa na sifa za mwanafunzi kujiunga na Chuo Kikuu akiwa na ufaulu wa Kidato cha Nne na „D‟ mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo majibu niliyoyatoa na maelezo niliyoyatoa mbele ya Bunge lako yanazingatia hali halisi ya elimu na kumekuwa na kuchanganya kati ya sifa ya kujiunga na Chuo Kikuu na sifa ya kujiunga na Cheti cha Ualimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tu kwamba, hata katika kujiunga na cheti cha uwalimu hawa wanafunzi walipokuwa wanadahiliwa mwaka 2013/2014 ilikuwa ni ufaulu wa point 27 ambazo ni sawa mtu awe na angalau D 6 na C moja ndiyo ilikuwa kiwango cha chini. Kwa hiyo, wale ambao walikuwa wanajua kwamba zilikuwepo sifa za namna hiyo, nikizipokea Wizara yangu itapitia kwa kuzingatia pia na hizo taarifa ambazo mpaka sasa hivi hazipo mezani kwangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa nataka kusema sasahii ndiyo mfano ambao tunakuwa tunasema tunataka mabadiliko lakini pale ambapo hatua mahsusi zinapochukuliwa za kuonesha kwamba, tunataka kuwa na elimu iliyo bora pia sasa tunakuwa tunapata pingamizi au tunakuwa tunapata malalamiko. Ninawaomba sana Waheshimiwa mtuunge mkono katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ni sawa na kiwanda bahati mbaya ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage ana shughuli hayupo hapa maana kila siku ndiyo eneo lake kila akisimama anazungumzia masuala ya viwanda na ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu mambo ya kilimo. Nataka tu kusema kwamba, elimu ni sawa na kiwanda, haiwezekani kama wewe unataka kutengeneza nguo kiwandani ukaanza na pamba iliyo mbovu ukategemea utoe nguo iliyo bora, haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kupata products nzuri kiwandani lazima na malighafi ziwe na ubora ulio mzuri. Kwa hiyo, hii inakwenda hivyo hivyo hata katika sekta ya elimu. Haiwezekani uwe na wahitimu wazuri wanaoweza kuchangia katika kuleta maendeleo katika nchi hii wakati unaowadahili wana viwango vya chini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi mwanafunzi amefeli katika somo, katika level ya Kidato cha Nne unampeleka akachukue digrii na kwa miongozo ya Wizara ya Elimu, mwanafunzi mwenye digrii ya uwalimu anatakiwa afundishe A-Level. Yeye mwenyewe hajafika, yeye mwenyewe hakufaulu halafu anatakiwa akafundisha A-Level hivi kweli itawezekana! (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge, naomba katika hili mtuunge mkono na kwamba, mturuhusu tuendelee kufanyakazi ambayo wote kwa siku mbili mmekuwa mkichangia kwamba mnataka kuona elimu hii inakwenda vizuri. mtuunge mkono kwamba, huo ni mwanzo tu tutaendelea kusafisha katika elimu, tutaendelea kusafisha katika vyuo vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama wapo ambao wamekwisha maliza wako katika soko la ajira tutafika hata huko. Tusipofanya hivyo tutakuwa tunayasema haya kila siku. Kwa hiyo, ninachotaka kusema ni kwamba, hilo suala tutalifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni utofauti unapozungumzia mtumishi hewa sioni tofauti na mfanyakazi asiyekuwa na sifa akikaa mahali. Tofauti tu ni kwamba, mmoja, ni mtumishi hewa haonekani kabisa, lakini mwingine ni mtumishi hewa amekaa mahali ambapo hastahili na hawezi kuleta tija katika Taifa hili. Kwa hiyo, kwasababu mmekuwa mnachangia kwa siku mbili mfululizo ninaamini kwamba, michango yenu ilikuwa inatoka moyoni na mlikuwa mnachangia kwa dhati kabisa na ndiyo maana nimesema bila kujali mchango umetoka upande gani, kwa sababu haya ndiyo malengo ya Serikali ya Awamu Tano katika sekta ya elimu. Nashukuru kwamba, wote tuna-share vision moja na Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tuliyoifanya St. Joseph haitaishia hapo, kazi ndiyo imeanza na kwa heshima tu labda ya wale ambao wako kwenye utumishi wanatumi vyeti feki, wanatumia qualification feki. Mimi niseme kwamba, mjitoe katika Utumishi wenu kwa heshima yenu, vinginevyo tutawafikia, wajitoe wenyewe, wajisafishe wenyewe kwa sababu tunaposema mnataka mabadiliko basi mkubali mabadiliko ya kweli ni mabadiliko ya kweli ni kuthubutu kuchukua hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nguvu na ujasiri wa kuthubutu tunao na hatua tutazichukua. Kwa hiyo, hili suala la St. Joseph ni mwanzo tutaendelea kama nilivyosema tutavikagua Vyuo kama vina watu ambao hawana sifa tutawaondoa. Pia kama mlivyoshauri na ninaungana na ninyi kabisa kwamba, tutaangalia na hatua za ziada za kuchukua kwa sababu haiwezekani kufanya utapeli, unawapotezea muda vijana kwa kitu ambacho unajua kabisa mwisho wa siku hawatafika popote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kwa kweli ndugu yangu Mwanasheria Mkuu wa Serikali atanisaidia tuangalie hatua gani za ziada zitachukuliwa lakini suala la wale wanafunzi kurudi pale halipo, isipokuwa tutaangalia kuwashauri kulingana na sifa zao, kwa sababu kuna nafasi mbalimbali katika elimu basi wanaweza wakaenda katika nafasi nyingine ambazo zipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata humu ndani kama kuna watu wembe ni huo huo. Ni lazima tukubali kwamba Kiongozi ni kuwa mfano, kwa sababu haiwezekani tu tuwe tunakemea. Haiwezekani sisi tuwe wa kwanza kupaza sauti halafu sisi wenyewe tunakuwa na matendo hayo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie eneo lingine ambalo limechangiwa kwa nguvu sana, suala la ada elekezi; Kwanza nimefurahi kuona kwamba humu ndani hata nikiamua kufanya kikao cha kutoa maelekezo kuhusu shule nitapata tu column ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa wengi ambao wamechangia wamekuwa wanasema ni wamiliki wa shule, wengi humu ndani wameonyesha ni wamiliki wa shule, ni jambo jema. Lakini tu niseme kwamba ni kwa nini Serikali ilianza huu mchakato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la ada elekezi lilianzia humu ndani ya Bunge lako Tukufu, ambapo Waheshimiwa Wabunge mmekuwa mkitumwa na Wawakilishi wenu muihoji Serikali kwamba, ni kwa nini Serikali inaziachia shule zipandishe ada kiholela? Huu ndiyo msingi na chimbuko la ada elekezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyokuwa nafuatilia mjadala kidogo nikawa nasema ndiyo hivyo, wanasema kila wakati kingereza every day is a new beginning kwamba, kila siku inakuwa na mambo yake, sina maana kama napinga maoni yaliyotolewa lakini tu nilikuwa nataka tukumbuke historia ambapo tumetoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika hili suala la ada elekezi tumekuwa na hoja nyingi zimekuwa zinatolewa na wananchi mbalimbali wakilalamika kwamba, viwango vinapandishwa kiholela, humu ndani katika Bunge lako kukawa na ombi au maelekezo kwa Serikali kwamba ije na ada elekezi ili kutoruhusu shule kupandisha ada kiholela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii inaendelea kufanyika ambapo kulikuwa na mtaalam elekezi ambaye anatoka Chuo Kikuu Huria aliyekuwa amepewa kuifanya kazi hii. Hii kazi ilikuwa inafanyika kwa ushirikishwaji wa wamiliki wa shule binafsi na mpaka mwezi Februari kulikuwa tayari na majadiliano yanaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuifanya kazi hii ni kweli kumekuwa na changamoto hilo lazima nikiri, haikuwa rahisi sana kuweza kufikia viwango kutokana na kwamba shule ziko katika madaraja tofauti tofauti, kwa hiyo mwezi Februari tulikaa kikao cha pamoja na wamiliki wa shule binafsi kwa sababu wao ni wadau tulikuwa tunataka kitu cha ushirikishwaji ambacho tukikitoa wote tunakuwa tunaelewa kwamba misingi na sababu ya kufika tulipofika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kikao kile tulifikia hatua ya wote tulikubaliana hizi shule tulizozikagua viwango viko tofauti. Kwa hiyo, tukawa tumefikia hatua ya kwamba, tuweke madaraja lakini kabla hili zoezi halijakamilika wenzetu ambao tumekuwa tunafanya nao kazi upande wa pili, wamiliki wa shule binafsi wakawa wameona ni vema labda hili suala walifikishe huku. Kamati yangu ya Kudumu ya Huduma za Jamii tulifanya kikao cha pamoja kujadili suala la ada elekezi nafikiri ilikuwa tarehe 15 Aprili na katika kikao hicho hoja za pande zote zilizingatiwa na tukawa tumefikia muafaka kwamba, kwa sasa hivi hilo suala kwa sababu limechukua muda kulikamilisha na kumekuwa na changamoto, Kamati ikawa imetushauri kwamba kwa sasa Wizara tuna changamoto nyingi, hebu hilo tuendele kulitafakari na kuliangalia labda namna bora zaidi ya kuli-approach na Serikali ikawa imekubaliana na ushauri wa Kamati, tukawa tumesema kwamba kwa sasa hili suala la ada elekezi tutaendelea kulifanyia utafiti kwa kuzingatia changamoto ambazo zimejitokeza.
Kwa hiyo, mimi nilikuwa nasikiliza michango tu lakini kimsingi tulikuwa tunajadili suala ambalo ukurasa huo ulikuwa umeshafungwa tarahe 15 mwezi Aprili mbele ya Kamati. Ninashukuru hiyo michango mliyochangia tutaizingatia lakini hili suala lilikuwa limeshahitimishwa tarahe 15 mwezi Aprili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nimalizie kwamba suala hili la ada elekezi limehitimishwa kivipi, maana hilo ndiyo jambo la msingi. Kwamba kumekuwa na malalamiko ya shule za binafsi kupandisha ada na pia kumekuwa na michango ya kiholela. Kwa sasa hivi tulipofika makubaliano tuliyofika tutatumia taratibu zetu na ukiangalia katika hata Sera ya Elimu kabla ya hii mpya ambayo ilikuwa 1995, imeonyesha kabisa kwamba, shule binafsi zitaweka ada kwa kupata kibali cha Kamishna wa Elimu, kwa sasa hivi ofisi ya Kamishna wa Elimu itaendelea pamoja na Wakaguzi wa Shule kuendelea kuangalia uhalali wa ada zinazotozwa katika utaratibu ambao umeainishwa katika Sera ya Elimu na taratibu za elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Serikali haiwezi ikajitoa kabisa katika hili jambo, kwa sababu humu ndani tunapozungumza tumegawanyika pande mbili. Wengine humu wanaochangia wanasema ni huduma wengine wanasema ni biashara, kwa hiyo tutakachokifanya hatuweki ada elekezi lakini ni ile tu kuangalia uhalali kwa sababu kuna shule nyingine Mwanafunzi anaambiwa kila mmoja mchango wa majengo sasa kama shule ilikuwa haina majengo ilisajiliwa vipi? Kuna michango mingine ambayo haina uhalali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kigezo kimojawapo ili uweze kupata usajili wa shule lazima uwe na majengo na je, unapowachangisha wazazi wachangie majengo yako ya shule na wao watakuwa wabia katika shule yako? Kwa sabaabu shule ni ya kwako mwenyewe. Kwa hiyo kuna mambo ambayo lazima kama Serikali tutayaangalia na kamwe hatuwezi kuyafumbia macho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule zingine zinamtoza kila Mwanafunzi shilingi 100,000 kwa ajili ya Ulinzi, hiyo shule ina Walinzi wangapi? Je, kila Mwanafunzi ana mlinzi wake? Kwa hiyo ninachotaka kusema kwamba, katika msafara wa kenge na mamba wanakuwemo! Kwa hiyo hata katika shule binafsi katika msafara wa kenge…..hivyo hivyo! (Makofi na Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoendeleza maana ya ada elekezi haina maana Serikali itaacha tu mtu atumie kivuli cha shule, akilala, akiamka anawaambia wazazi kesho mje na kitu fulani. Tutaangalia, tutaenda katika utaratibu ambao tutakuwa tumekubaliana ambao utazingatia kanuni na taratibu zilizopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie kuhusiana na suala la VETA kwasababu hili suala limekuwa linajitokeza kwa wachangiaji wengi. Ni kweli kumekuwa na ahadi ya Ujenzi wa VETA ambao labda kasi yake haijaenda kwa kiwango ambacho Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla walikuwa wanatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika hati idhini ya Serikali ya Awamu ya Tano, Vyuo vyote vya Maendeleo ya Jamii vimewekwa chini ya Wizara yangu, kwa hiyo niwaombe kwa dhati kabisa Waheshimiwa Wabunge mnipitishie bajeti yangu ili sasa niende nikaviangalie vile Vyuo vya Maendeleo ya Jamii, mmekuwa mnaomba sana mpate VETA tutafanya ukaguzi tuangalie vina hali gani ili tuweze kuanza mara moja kuvitumia hivyo kwa sababu mtaji wa kuanzia utakuwa ni mdogo kuliko kuanza kujenga upya. Ninaamini kabisa hatua hiyo ya Serikali ya kuleta Vyuo vya Maendeleo katika Wizara ya Elimu itaweza kutatua kwa kasi kubwa suala hili la VETA ambalo kwa kweli ni muhimu sana.
Waheshimiwa Wabunge ningeomba tu niwasihi na kuwaomba sana, tunapozungumzia VETA tusizungumzie kwamba ni kwa sababu ya Watoto waliofeli, hapana! VETA ni kwa ajili ya kujenga uwezo, VETA ni kwa ajili ya kujenga ujuzi ili Watoto waweze kuleta tija, tusiichukulie kwamba ni chuo cha wale ambao wameshindwa kwa sababu inaweza ikatufanya tusipate watu ambao ni wazuri ambao wanaweza wakalisaidia Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie ndugu yangu alikuwa anaulizia kuhusu suala la VETA ya Ludewa na akawa anasema kwamba atashika shilingi yangu. Mheshimiwa Mbunge wa Ludewa wala huna haja ya kushika shilingi yangu, mimi na Serikali ni waaminifu, Serikali haiwezi kusema uwongo, tuliahidi tutajenga VETA Ludewa tutaijenga na pengine huioni katika kitabu kwa sababu inasomeka kama Chuo cha VETA cha Mkoa wa Njombe. Hiki Chuo cha VETA Mkoa wa Njombe kitajengwa katika Kijiji cha Shaurimoyo ambayo iko Ludewa, kwa hiyo utakuwa na bahati kwamba ni Chuo cha Mkoa lakini kinajengwa sehemu ya Ludewa, inapatikana katika ukurasa wa 59 wa kitabu changu cha bajeti.
Hivyo, Waheshimiwa Wabunge wamechangia na nikubaliane na ninyi kwamba kasi ya ujenzi wa VETA haijaenda kwa namna ambavyo tulikuwa tunatarajia, lakini naomba tu kwamba sasa kwa kuwa tumepewa hivi Vyuo vya Maendeleo ya Jamii mniruhusu kwamba nikalifanyie kazi, nikaviangalie vile ambavyo vitakuwa vinaweza kutumika mara moja na mdogo wangu Mheshimiwa Esther Matiko asubuhi alichomekea wakati Mheshimiwa Grace anachangia, kwa hiyo vyuo vyote katika Nchi nzima tutavitazama ili viweze kutumika mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo limechangiwa ni suala la Bodi ya Mikopo, suala la urejeshwaji wa mikopo pamoja na ule uhalali wa Bodi ya Mikopo ku-charge zile tozo zinazotolewa kwa Wahitimu. Kwanza kabisa nishukuru kwa michango yenu kuhusiana na suala hili la Bodi ya Mikopo na vilevile Waheshimiwa Wabunge walisema kwamba wana mambo ya ziada ambayo wanaweza wakanipatia ili niweze kuyafanyia kazi. Naomba sana, niko tayari kupokea michango hiyo na niwahakikishie kabisa nikiipata nitaifanyia kazi kwa sababu hizi fedha ni kwa ajili ya Watanzania na kwa ajili ya kuwakopesha watoto wa Kitanzania ambao hawana uwezo, kwa hiyo ni jukumu letu sote kusaidiana ili ziweze kurejeshwa kwa kasi inayotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tu kwamba ni kwanini kumekuwa na hii retention fee katika Bodi ya Mikopo. Suala la retention fee linawekwa ili ile thamani ya fedha iweze kubaki pale pale. Nitasema viwango. Inawezekana ikaonekana 60 percent kwa sababu mtu amekaa nayo muda mrefu, kadri unavyochelewa kulipa ni wazi kwamba ile fedha itaongezeka, lakini kiwango ambacho kinatozwa cha value retention fee ni asilimia sita ya mkopo wa mwanafunzi lakini vilevile kunakuwa na administration fee ambayo inakuwa ni one pecent ya mkopo anaouchukua mwanafunzi. Hivyo, kadri mtu anavyochelewa retention fee inakuwa ni kubwa kwa sababu kuna wengine ambao walikopa tangu Bodi ya Mikopo inaanza lakini bado hawajarejesha mikopo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina nia ya kukusanya mapato ya ziada kwa watu, kinachotakiwa, madam watu wanafahamu kwamba kunakuwa na retention fee, basi turejeshe mapema ili tusichajiwe kwa sababu ni hiari ya mtu ukirejesha mapema hautachajiwa, lakini wale ambao watachelewa ili thamani ya shilingi yetu iweze kubaki pale pale, ni lazima tuchaji hiyo retention fee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la urejeshwaji mikopo, changamoto zake zimezungumzwa kwa kirefu na mimi nikiri kwamba kama nilivyokuwa nimekiri kwenye hotuba yangu natambua kwamba kuna changamoto lakini kuna hatua ambazo tayari tunazichukua na vilevile kuna changamoto pia za kisheria. Baadhi ya maeneo katika Sheria ya Bodi ya Mikopo itakuwa vema kama ikifanyiwa marekebisho ili kuweza kuongeza kasi ya urejeshwaji ili kuwawezesha Watanzania wengi zaidi kunufaika na mikopo inayotolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine lililozungumziwa ni suala la utekelezaji wa sera, kwamba kumekuwa na maswali hii elimu ya lazima ya miaka kumi inaanza kutekelezwa lini na kadhalika. Niseme tu kwamba, ukisoma Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, imeainisha wazi kwamba ili utekelezaji wa sera hiyo uwe fanisi, kuna sheria ambazo zinahitaji kufanyiwa marekebisho. Sasa hivi tuko katika hatua ya kupitia sheria mbalimbali, kwanza kuna Sheria ya Elimu sura ya 353, kuna Sheria ya Serikali za Mitaa sura ya 287 na sura ya 288 na sheria nyingine ambazo zitawezesha sasa hii Sera ya Elimu iweze kutekelezwa kwa ufanisi. Hivyo, tupo tunafanya kazi na nategemea katika Bunge lijalo, baadhi ya sheria tutazileta na natarajia pia hata katika Bunge hili, Sheria ya Marekebisho ya Bodi ya Mikopo nitaiwasilisha kwenu, kwa hiyo itakapokamilika na taratibu zake zikawa zimewekwa na mikakati ya kuangalia madarasa na walimu, basi hiyo Elimu ya Msingi ya miaka 10 ndipo itakapoanza rasmi, sasa hivi bado tunaendelea na mikakati ya kuhakiksha kwamba tunakamilisha maandalizi ya msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imezungumziwa ni kuhusiana na suala la kutokuwepo kwa mtaala wa elimu ya awali na kutokuwepo na walimu wa kutosha. Ningependa tu kusema kwamba, mtaala wa elimu ya awali unaounganishwa na muhtasari wake umeshaandaliwa. Nikiri tu kwamba mtaala ambao ulikuwa unatumika zamani sasa hivi umerekebishwa na wako katika hatua sasa ya kuandaa vitabu. Pia kuhusiana na idadi ya Walimu kuwa pungufu ni kwamba katika mwaka 2013/2014, Wizara yangu iliongeza idadi ya Vyuo vinavyotoa mafunzo kwa ajili ya walimu wa elimu ya awali kutoka vyuo tisa hadi vyuo 13.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi tuna wananfunzi 3,200 ambao wanasoma ili wawe walimu wa elimu ya awali, kwa hiyo ninaamini kabisa kwamba jambo hili ni changamoto ambayo tunaikabili lakini tayari kuna hatua ambazo zinachukuliwa na ninaamini kwamba hawa watakapomaliza mwakani hili suala litatatuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika mafunzo ya walimu kunakuwa na somo la elimu ya awali ambalo ni somo la lazima kwa kila mwalimu na hivyo basi, pamoja na kwamba wale wanakuwa hawajabobea kwa maana ya specialization katika elimu ya awali lakini katika mafunzo yao ya Ualimu wamepata course ya elimu ya awali, kwa hiyo naamini kabisa kwa kutumia ujuzi huo wanakuwa wanaweza kuwafundisha vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango mwingine ambao umechangiwa kwa wingi sana na Waheshimiwa Wabunge ni kuhusiana na suala la ununuzi wa vifaa vya maabara. Ni kweli juhudi kubwa sana ilifanyika ya ujenzi wa maabara, na nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wananchi wote, Halmashauri zote na watu wote walioshiriki katika ujenzi wa maabara hizi ambazo kwa sasa zimekamilika. Tunatambua kwamba maabara zilijengwa ili zitumike na ninaomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara yangu inafanyia kazi suala hilo kupitia mpango wa program yetu ya lipa kulingana na matokeo ambayo hii ni sehemu ya BRN.
Katika BRN kulikuwa na makubaliano na washirika wetu wa maendeleo kwamba, Wizara tunapokuwa tunatekeleza vigezo ambavyo tumekuwa tumewekewa, tunakuwa tunapata fedha ambazo kwa kweli zinakuwa na msaada mkubwa sana na hizo fedha tunazozipata katika Wizara yangu tunakuwa tunaachiwa uhuru tofauti na fedha nyingine za wafadhili ambazo wanakuwa wamekupangia, hizo ndiyo fedha pekee ambazo wanakupa halafu wanasema panga unavyotaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo pamoja na kwamba jukumu la kununua vifaa vya maabara liko katika ofisi ya Rais - TAMISEMI lakini niseme tu kwamba Wizara yangu imetenga kiasi cha shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kununua vifaa vya maabara na tayari hizi ni katika fedha za mwaka unaokwisha, sasa tunavyoongea ni kwamba tumeelezea hata katika kitabu chetu iko katika ukurasa wa 75, kwa hiyo niwahakikishie kabisa kwamba hilo suala tunalitambua, tunataka wanafunzi wajifunze Sayansi kwa vitendo na siyo kwa nadharia kwahiyo shule zote ambazo zimejenga maabara na imekamilika kabisa, naomba niseme vizuri, shule ambazo zimejenga maabara na zimekamilika kabisa mpaka mwezi Februari tulikuwa tumezitambua shule 1,536 hizi zote zitapata vifaa. (Makofi)
Kwa hiyo, nichukue fursa hii pia kuzihamasisha Halmashauri nyingine ambazo hazijakamilisha ujenzi wa maabara basi nazo zikamilishe na niseme tu kwamba kwasababu hii program ya pay for results bado inaendela na kwa kutambua kwamba kipaumbele chetu ni kuboresha elimu yetu inayotolewa, niwahakikishie tu kwamba hizi fedha kila tunapozipata tutakuwa tunazitumia katika kuboresha elimu na tunatambua kwamba hatuwezi kuwa na elimu bora kama hatuna vifaa vya kufundishia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la elimu maalum. Limechangiwa vizuri na Dada yangu Mheshimiwa Dkt. Elly Macha amezungumzia suala la kiwanda cha kuchapa vitabu na ile lugha ya alama na kadhalika kuhusiana na elimu maalum.
Naomba tu niseme kwamba, kama ambavyo nilikuwa nimesema katika hotuba yangu, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, elimu maalum itakuwa ni kipaumbele. Tutahakikisha tunanunua vifaa, tayari kuna fedha ambazo tumezitenga kwa ajili ya elimu maalum na ni fedha nyingi takribani bilioni 5 siyo hela kidogo hizo, tunataka kuhakikisha zile kero za msingi katika hii elimu maalum tunaziondoa. Kwa hiyo nirudie kuwahakikishia kwamba umuhimu wa elimu maalum tunautambua na katika bajeti yetu tumezingatia. Tumeweka fedha za kutosha na tutaendelea kuimarisha kadri uwezo wa kifedha unavyojitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kiwanda cha kuchapa vitabu vya wasiiona pia nacho tutakifanyia maboresho na vilevile suala la lugha za alama nililipata nilivyoenda kutembelea Kilimanjaro, kuna changamoto kule kwamba kuna shule ya wanafunzi wanafundishwa lakini wanakuwa wengi wanashindwa kwenda sekondari kwa sababu hakuna wataalamu, tayari tumeshaanza kulifanyia kazi na tunashirikiana na kitengo cha elimu maalum katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Wameniandikia andiko la mapendekezo ya jinsi gani ambavyo tunaweza tukatatua hilo suala la lugha za alama ili kuwawezesha wanafunzi hao kuendelea na elimu ya sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala ambalo limeongelewa kwa kirefu pia sana humu ndani, suala la watoto wa kike wanaopata mimba kuweza kurejea masomo yao. Hili suala la kuwarejesha wanafunzi ni suala ambalo najua limeanza muda mrefu kidogo na nakumbuka nilikuwa na Kamati, Mheshimiwa Zaynab Vullu nakumbuka alikuwa ni Mjumbe wa hiyo Kamati, tulishafanya hata na presentation muda, lakini na Mheshimiwa Suzan Lyimo na Margret Sitta wote walikuwa kwenye hiyo Kamati Maalum ilikuwa imeundwa ajili ya kuangalia ni kitu gani cha kufanya na pia walienda hata kutembela hata katika Nchi nyingine kuona, kimsingi pendekezo ambalo lilikuja ni kwamba, hawa wanafunzi wapewe nafasi ya kuweza kurudi shuleni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Waziri mwenye dhamana ya elimu ambaye pia nina dhamana ya kuangalia elimu nje ya mfumo rasmi, elimu ndani ya mfumo rasmi sina pingamizi kabisa na hawa wanafunzi kurudi shuleni. Kitu ambacho tutafanya katika Wizara yangu ni kukaa na wadau ambao ni muhimu katika jambo hili hasa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, ili tuhakikishe kwamba tunapomuangalia binti arudi shuleni, lakini pia tusimsahau mtoto wake, kwa sababu binti ana haki ya kupata elimu lakini na huyu mtoto ana haki ya kupata malezi. Kwa hiyo, hicho kikao cha kuangalia utaratibu gani utawekwa ili hizi pande zote mbili ziweze kunufaika bila ya kuwa na madhara, tukiweza kuwa na utaratibu mzuri sioni kama kuna tatizo lolote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema michango ni mingi na nimejitahidi kuongea mengi lakini naona kengele ya kwanza imeshagongwa, siwezi kuyamaliza yote lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja zenu zote tutazijibu na tayari tuna rasimu hii hapa – tumeshaanza kuzijibu, tutamalizia na tutawakabidhi. Kwa hiyo wale ambao pengine hoja zao sijazijibu naomba tu msione labda pengine siyo za muhimu ni kwa sababu ya muda, michango yote kama nilivyosema ni muhimu, michango yote ina tija na mtapata majibu kwa maandishi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa nigongewe kengele ya pili, nihitimishe hoja yangu kwa kukushukuru sana wewe Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kutuongozea majadiliano, nashukuru sana pia Naibu Spika ambaye tulianza naye jana na Wenyeviti wote ambao wameshiriki katika kuongoza majadiliano ya hoja hii. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu na sasa ninaomba sana kwa heshima kubwa mniunge mkono ili nikafanye kazi ambayo mnataka tuifanye. Naomba muunge mkono hoja yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.