Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na uzima na kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili nami niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nimshukuru na kumpongeza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kutuletea mwekezaji ambaye ana nia ya kujenga Kiwanda cha Sulphur kule Mtwara, namshukuru kwa hilo. Nampongeza kwa hotuba nzuri ambayo siyo tu imeandikwa vizuri, lakini pia amewasilishwa vizuri sana na kila mtu atakubaliana na hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema Serikali ya Awamu ya Tano ni ya viwanda na tunaunga mkono sana hilo. Ushauri wangu kwa Serikali yangu ni kuhakikisha tunatoa vikwazo vyote vile ambavyo wawekezaji wanakumbana navyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wangu wa Mtwara, naomba nianzie huko. Tunaye mwekezaji ambaye ameonesha nia ya kutaka kujenga Kiwanda cha Mbolea na tayari wenzetu wa EPZA wamemuonesha eneo la kujenga kiwanda tangu mwaka 2015 Aprili, lakini mpaka tunapozungumza sasa hivi, anashindwa kuanza kujenga kiwanda kwa sababu Wizara ya Nishati na Madini wameshindwa kumhakikishia upatikanaji wa gesi kwa zaidi ya miaka minne ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wakati watu wa EPZA wanakuja kumuonesha eneo, walikuwa hawajazungumza na Wizara ya Nishati na Madini? Mwekezaji anaomba uhakika, kiwanda kile kitachukua zaidi ya miaka minne kukamilika, anaomba ahakikishiwe baada ya miaka minne kupewa gesi, mpaka leo Wizara ya Nishati na Madini haijampa uhakika kama watampa hiyo gesi. Kwa kweli kama Mwanamtwara, nasikitika sana, kwa sababu kiwanda hiki ni cha mfano. Mwekezaji alikuwa anafanya ubia na Halmashauri zote za Mkoa wa Mtwara na tayari tulishakubali, eneo wamepewa, lakini gesi hajapewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja, atueleze amefanya juhudi gani za kumsaidia mwekezaji huyo kupata gesi ili Kiwanda cha Mbolea ambapo nchi inaagiza mbolea kwa zaidi ya asilimia 90, lakini anakuja mwekezaji anataka kujenga hapa, tunamwekea vikwazo. Hivi tuelewe kuna lengo gani ambalo sisi wengine hatulifahamu? Haiwezekani gesi itoke Mtwara lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hakuna kiwanda hata kimoja kimepewa gesi katika mkoa ule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nataka kulichangia, ni suala la maeneo ya EPZA. Kama kweli tunahitaji kuwa na Serikali ya Viwanda, ushauri wangu ni kuiomba Serikali itafute fedha, ilipe fidia maeneo yote ambayo wanakusudia kuwa ni maeneo ya uwekezaji kwa maana EPZA na SES ili wawekezaji wanapokuja wasipate usumbufu wa aina yoyote wa kutafuta maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waziri atakapokuja atuambie, ana mikakati gani ya kuhakikisha kwamba maeneo ya EPZA yote yanalipiwa fidia kwa wakati ili yawe tayari, yasafishwe, yawekewe uzio tayari akija mwekezaji unamwonesha kwamba eneo la kuwekeza ni hili hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulianzisha ushuru wa korosho ambayo inasafirishwa ghafi kwenda nje, yaani export levy ili kuhakikisha kwamba, badala ya wafanyabiashara kupeleka korosho nje, wazibangue hapa. Lengo la ushuru ule ilikuwa ni kuwakatisha tamaa wale wanaopeleka korosho bila kuzibangua ili wawekeze viwanda katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitapenda Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze tangu tumeanzisha export levy mpaka sasa hivi ni viwanda vingapi vimeweza kujengwa. Kama hakuna kiwanda chochote, ameshauri nini, kwamba kodi ile iongezwe kwa kiasi gani? Wasiwasi wangu ni kwamba, labda ile export levy ni ndogo kiasi kwamba hakuna sababu, mtu anaweza akalipa na bado akapeleka nje kuliko akizalisha korosho ndani ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulichangia ni suala la kulinda viwanda vyetu. Kama tumeamua kweli kuwa nchi ya viwanda, ni lazima suala hilo liende sambamba na ulindaji wa viwanda vyetu vya ndani. Tanzania tuna uwezo wa kujilisha au kujitosheleza sisi wenyewe kwa mafuta ya kula, tuna uwezo wa kuzalisha alizeti. Tunayo Mikoa kama Singida, Tabora, Dodoma na kanda nzima ya kusini huku, tuna uwezo wa kuzalisha alizeti na kuweza kuzalisha mafuta ya kujitosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yatategemea iwapo tutakuwa tumeweka sheria ya kulinda viwanda vyetu. Kuna mafuta mengi sana ya kula yanatoka nje, wakisingizia kwamba mafuta hayo hayajakamilika, yaani yanakuja kusafishwa huku kwetu, lakini kimsingi yakifika hapa wanakuja tu kuya-park na kuanza kuyauza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Waziri wa Fedha pamoja na Waziri wa Viwanda na Uwekezaji, watuambie wana mikakati gani ya kulinda viwanda vyetu vya mafuta ya kula hapa nchini? Wenzetu Uganda wanafanya, Rwanda wanafanya, kwa nini sisi tuwe ni eneo ambalo mtu yeyote anayetaka kuleta mafuta ya aina yoyote ambayo hatuna hata uhakika wa usalama wa afya zetu, tunaruhusu watu kufanya hivyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumsikia Mheshimiwa Waziri anatuambia katika upande wa viwanda vya mbolea na korosho kule Mtwara anatuletea viwanda vingapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, namwomba tu Mheshimiwa Waziri ajiandae kuja kuniambia kiwanda kile cha mbolea ana mikakati gani au anamwezeshaje yule ili aanze kujenga kile kiwanda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.