Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mungu kwa fursa ya kuchangia hotuba hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda pamoja na Naibu, Makatibu Wakuu na watendaji wa Wizara yake kwa hotuba inayoainisha mipango mizuri inayogusa maeneo yote muhimu yanayoleta maendeleo ya viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. Hongera sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kupitia Wizara hii kwa mpango unaozingatia uanzishwaji wa viwanda kwa kuanza na mazingira bora ya kuwekeza kwenye viwanda ambayo ni rasilimali zilizopo nchini kama ardhi, mazao ya kilimo, ufugaji, uvuvi, misitu, mbegu za mafuta, pamba na kadhalika; miundombinu muhimu na wezeshi kama vile barabara, umeme, maji, mawasiliano na rasilimali watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa rai kwa Serikali kupitia Wizara ya Viwanda kuhakikisha kuwa wawekezaji wanaandaliwa sera na sheria zinazokinzana zirekebishwe ili kuepuka migogoro na wananchi na taasisi za Serikali zinazosimamia ukusanyaji mapato. Sheria, sera na taratibu za taasisi zetu zizingatie kuondoa urasimu na kuhakikisha kuwa maamuzi juu ya uwekezaji yanafanywa bila ucheleweshaji wowote na usumbufu kwa wawekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirikiano kati ya Wizara ya Viwanda na Wizara nyingine wezeshi na uchocheo uchumi uanze tangu mipango inapoanza kuwekeza viwanda. Kwa hiyo ni mategemeo yetu kuwa Mheshimiwa Waziri atatuainishia mfumo uliopo wa mipango kati ya Wizara ya Viwanda na Uwekezaji, Nishati na Madini, Miundombinu, Maji, TAMISEMI, Kazi na Elimu ya Juu na Ufundi ili kila mmoja aonyeshe jinsi gani atachangia katika kukamilisha mipango ya kuendeleza viwanda hivyo na utekelezaji wa mipango hii. Hii itatatua changamoto nyingi zinazotokana na kuwa kila Wizara inajiendesha yenyewe bila kuwa na mawasiliano ya karibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuboresha mazingira ya viwanda vilivyopo kwa kuhakikisha kuwa wanapata huduma muhimu kujiendesha kama vile maji, umeme, miundombinu, masoko, maghala, mawasiliano na mitaji. Hii itakuza pato, kuongeza bidhaa na kuzalisha ajira za kutosha. Hii itasaidia kuwaaminisha wananchi na wageni wanaotaka kuwekeza kwenye viwanda na kuwavutia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru Serikali kupitia Wizara ya Viwanda kwa kuzingatia katika mpango huu wa kuendeleza viwanda kila kanda ya nchi kwa uwiano unaoendana na rasilimali zilizopo na comperative na competitive advantage. Hii itaondoa kuwa maeneo machache ya nchi yanaendelea zaidi wakati mengine yako nyuma ilhali wana fursa nyingi za kuwa na viwanda. Wilaya kama Wilaya yangu ya Ileje na nyingine nyingi zenye kuzalisha nafaka na mazao mengine kwa wingi zipewe kipaumbele tunapopanga kuwekeza viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kutoa rai kwa Serikali kuhakikisha sasa kuwa sambamba na uanzishwaji wa viwanda tuanzishe viwanda vyenye kuzingatia soko la ndani. Serikali ijipange kuzalisha bidhaa zinazofaa kutumiwa nchini ili kukuza soko la ndani na kwa hiyo kuongeza ajira na kuondoa umaskini. Kwa hili tunamuomba Waziri ahakikishe kuwa mipango inazingatia kukuza soko la ndani na soko la Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla, tupatiwe mkakati wa kuanza kupunguza uagizaji wa bidhaa ambazo zinazalishwa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango na vipimo. Bidhaa nyingi ambazo hazikidhi viwango zinaingia nchini na nyingine ni hatarishi, vilevile nguo na bidhaa za nguo zinazozalishwa na kuagizwa nchini au hata bidhaa za vifaa vya ujenzi hazizingatii vipimo sahihi; wanapunja kwa kupunguza sentimeta katika bidhaa. Hii inawadhulumu wananchi, kwa hiyo natoa rai kuwa TBS na WMA wajengewe uwezo wa kupatiwa wafanyakazi wengi zaidi ili waweze kukagua viwanda na bidhaa hizi ili viwango na vipimo vizingatiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu masoko na vituo vya mipakani, Tanzania ina mipaka mingi na majirani zetu ambayo kwa mtazamo chanya ni fursa muhimu ya kuboresha biashara ya mipakani na nchi jirani. Yapo masoko mengi ya mipakani na yapo maeneo kama Ileje ambayo hayajaendelezwa lakini yana uhitaji mkubwa wa kuendelezwa ili wananchi wa maeneo haya ambao wengi wao ni wanawake na vijana wapate kipato na kuinua familia zao na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ina fursa ya kuwa na soko la kimataifa la mazao ya kilimo yaliyosindikwa ya ufugaji, uvuvi na misitu. Ileje inapakana na Malawi na Zambia lakini pia iko karibu na Mji wa mpakani wa Tunduma na hii kibiashara ni fursa kubwa. Ningependa Serikali itufahamishe jinsi ilivyojipanga kuboresha masoko yote ya mipakani kwa kuiwekea miundombinu muhimu na kujenga vituo vya forodha na soko la Kimataifa la Isongole.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu jinsia na maendeleo ya viwanda. Wanawake ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi, pia ni wafanyabiashara wazuri. Tungependa kuishauri Serikali izingatie umuhimu wa kundi hili muhimu kuzingatia maendeleo ya viwanda tangu ngazi ya mipango hadi utekelezaji. Wanawake wanahitaji viwanda vya usindikaji, kufuma masweta na nguo za baridi, nguo kama khanga, vitenge, vikoi na hivi pamoja na viwanda vya kusindika matunda, mboga na mazao ya mifugo, karanga na mafuta ya kula. Ningependa kujua jinsi gani wanawake watazingatiwa katika uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgodi wa Kiwira utafufuliwa lini? Naunga mkono hoja.