Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kukupongeza Mheshimiwa Waziri na Serikali yetu kwa hotuba nzuri kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda. Hotuba hii inaongelea mambo mazuri sana na kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda jambo ambalo litaleta fursa ya ajira kwa vijana wetu ambao wako mitaani, hawana ajira, pia tukiwa na viwanda tutainua kipato cha mwananchi na kipato cha Taifa kitaongezeka na uchumi wetu utakua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa ni lazima tuhakikishe tunaweka mazingira rafiki ambayo yatawapa fursa wawekezaji kuja kuwekeza nchini kwetu bila usumbufu yaani tuondoe urasimu uliopo, pia viwanda ambavyo vipo tuhakikishe tunavilinda. Niiombe Serikali yangu ili tuweze kufanikiwa na tuingie kwenye uchumi wa viwanda wa kati tuhakikishe tunakuwa na umeme wa kutosha ili viwanda vyetu vitumie umeme wetu kupunguza gharama za uzalishaji na ndipo kipato cha Taifa kitaongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwekeza kwenye kilimo cha kisasa ili kupata malighafi za kupeleka kwenye hivyo viwanda, tuweke mazingira rafiki ili huyu mkulima anacholima kiwe na ubora kwa ajili ya viwanda vyetu hatuwezi kufanikiwa. Mheshimiwa Waziri tutumie huu umeme wa REA ambao umefika vijijini, tuwawezeshe na kuwapa elimu vijana wetu kufungua viwanda vidogo vidogo wapate ajira na kuongeza kipato cha Taifa.
Namuomba Mheshimiwa Waziri, Kyerwa kuna kahawa ambayo ni zao muhimu linaloingizia Taifa kipato. Serikali iongeze Benki zetu hasa hasa Benki ya TIB ipunguze riba ili wananchi wakopeshwe mashine za kukoboa kahawa, hili litaongeza kipato kwa mwananchi kitu ambacho kitapunguza wizi wa kahawa inayopelekwa nchi jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kufikiria kufungua kiwanda Kyerwa cha kusafisha Tini ili kuinua kipato cha wachimbaji wadogo wadogo na hili litaondoa Tini nyingi inayovushwa kupeleka nchi jirani maana karibu asilimia 75 ya Tini inayochimbwa Kyerwa inanufaisha nchi jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali ipeleke viwanda maeneo husika ili kuongeza ajira kwa maeneo husika mfano, viwanda vipelekwe maeneo ya uzalishaji pamba, matunda, tumbaku na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa neema ya gesi tunaweza kuzalisha vitu vingi. Niiombe Serikali tusiishie kwenye kuzalisha gesi kwa ajili ya umeme tu, bali kila kitu kinachotoka kwenye gesi maana gesi tunaweza kuzalisha vitu vingi sana.