Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, lakini nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri Naibu Waziri na watendaji wote kwenye wizara hii na mimi nina mada moja tu ambayo itachangia mada ya mifugo nitajikita kwenye mifugo, baada ya mifugo kufanya vibaya kwenye bonde la Ihefu, Serikali ilifanya maamuzi ya makusudi kupeleka mifugo ile kwenye Mkoa wa Lindi na sisi Mkoa wa Lindi kuna wilaya mbili ndio tumepokea wafugaji Wilaya ya Kilwa na Wilaya ya Liwale. (Makofi)

Mheshimies Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale tulitenga vijiji vitatu; Kijiji cha Lilombe Ngapata na Kimambi ndio vijiji viliidhinishwa kupokea wafugaji, lakini kutokana na sababu sitofahamu ninyi wenyewe mnajua wafugaji sasa hivi Liwale nzima kuna wafugaji. Jambo ambalo nataka kuliongelea hapa Serikali hapakufanywa maandalizi ya kawaida au maandalizi mahususi ya kupokea mifugo. Hapakuwa na miundombinu yoyote ya kupokea mifugo ile naninavyoongea mpaka leo hakuna majosho hakuna malambo hapakuandaliwa lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, palihitaji maandalizi kwanza ya kimuundo mbinu, halafu maandalizi ya kielimu kwa maana kwamba watu wa kuandaa saikolojia kwa sababu sisi kwa asili sio wafugaji. Leo ninavyozungumza hapa ni zaidi ya miaka 10 mifugo iko Liwale lakini Halmashauri ya Wilaya ya Liwale haijawahi kunufaika na chochote kutokana na mifugo ile, hii ni kwa sababu hapakuandaliwa na miundombinu yoyote na vilevile sisi wenyewe wafugaji wana Liwale hatukuandaliwa kupokea mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie jambo moja mwaka 76 mzee Rashindi Mfaume Kawawa waziri wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alituletea ng’ombe sisi Liwale kila Kijiji ng’ombe 20 na kila shule tulipata ng’ombe ishirini lakini ng’ombe wale walidumu miezi sita tu sababu ni nini hakuna mzazi aliyekubali mwanae kumpeleka kuchunga ng’ombe ilikuwa ni adhabu. Kwa hiyo, Mwalimu akimpangia kwenda kuchunga ng’ombe huyo Mwalimu haamki, lakini ng’ombe wa kijiji nao walikufa kwa mtindo uleule hakuna mtu aliyekubali kwenda kuchunga ng’ombe akiwa na akili timamu. Ukimwona kwetu mtu anachinja ng’ombe basi ujue dishi limeyumba. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo ng’ombe wale walikufa sisi kwetu mfugaji anafuga bata tena dume kwa hiyo kwa msingi huo kwetu tulikuwa tuandaliwe kisaikolojia namna ya kuwapokea wale ng’ombe vilevile tuandaliwe kwa miundombinu. Sasa nini kinatokea hatuna wataalam wakutuelimisha namna ya kukuaa na wafugaji wale na vijiji vyetu havikuingia kwenye matumizi bora ya ardhi. Jambo hili linatuletea migogoro sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua jukumu la matumizi bora ya ardhi ni jukumu la halmashauri lakini halmashauri inaingia kwenye jukumu hili kwa faida ipi ambayo tumeipata kutokana na mifugo ile? Naiomba sana Serikali, ije Liwale ije itusaidie kuanza kuhakikisha vijiji vile ambavyo tayari vina wafugaji vinaingia kwenye matumizi bora ya ardhi ili kutupunguzia migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi pia tunatakiwa tuwe na malambo kwa ajili ya wafugaji wale, jambo linalofanya sasa Liwale nzima isambae mifugo, kwa sababu wafugaji wanatafuta maji, hawana mahali pa kupata maji, kwa hiyo, tumeruhusiwa vijiji vitatu sasa vijiji vyote 70 vina wafugaji na miaka mitano, sita ijayo idadi kubwa ya wafugaji itakuwa kubwa kuliko wenyeji wa pale kwa hiyo tunaomba tuletewa wataalam kwa ajili ya miundombinu tuletewe wataalam kwa ajili ya kutuelemisha namna ya kufuga mifugo ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusu minada tunaomba sana tupate mtu specific ambaye anajua mambo ya minada, aje atufunguliwe mnada Liwale, Kilwa ng’ombe wanakwenda Mtwara wanakula ng’ombe Mtwara wanakula ng’ombe Songea wanakula ng’ombe wapi lakini ng’ombe wanachukuliwa kutoka Liwale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwambia, Halmashauri ya Wilaya ya Liwale haijawahi kupata hata shilingi, tunahitaji juhudi za makusudi ili na sisi tuone faida ya kuwepo ile mifugo pale Liwale. Hilo ndio jambo mahususi niliyokuwa nimeomba nafasi hii kulizungumzia kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa dakika tano hizi; naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)