Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa hotuba yake nzuri yenye kulenga kukuza uchumi wa viwanda vidogo vidogo na kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi hii ya uwekezaji wa viwanda iliyoainishwa katika utekelezaji wake wa Mpango huu wa mwaka 2016/2017, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea maeneo mbalimbali ya Majimbo yao juu ya uendelezaji wa upandishaji wa thamani ya mazao yao wanayolima, lakini juu ya vijana na wanawake kuwezeshwa kushiriki katika uchumi huu wa viwanda vidogo vidogo ili kukuza ajira na kuleta ustawi wa vijana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, SIDO ni mkombozi mkubwa wa wafanyabiashara wadogo wadogo, lakini ni mkombozi mkubwa kwa vijana na wanawake katika kuyafanya makundi haya yaweze kushiriki katika uchumi huu wa viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali kusaidia SIDO Mkoa wa Lindi fedha za kutosha ili kusaidia kundi kubwa la vijana na wanawake kupata elimu ya kutosha kupandisha thamani ya mazao yanayolimwa Mkoani Lindi. Naishukuru Serikali, imetenga bajeti ya shilingi bilioni sita katika Mikoa minne tu. Naomba Mkoa wa Lindi ufikiriwe kuwezesha SIDO iweze kusaidia Mikoa ya Lindi na Mtwara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi ya uwekezaji EPZ, Lindi Manispaa ni wafaidika wa mradi huu. Eneo lilishatengwa lakini hatuoni chochote kinachoendelea juu ya mradi huu. Tunaomba Serikali itupe majibu juu ya mradi huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza sera endelevu ya viwanda ya mwaka 1996 Mkoa wa Lindi ulikuwa na viwanda. Kwa mfano, Kiwanda cha Usindikaji wa Mafuta ya Karanga na Ufuta (Nachingwea); na Kiwanda cha Ubanguaji Korosho, Lindi Vijijini na Lindi Manispaa. Viwanda hivi havikuwahi kufanya kazi hata siku moja, Mheshimiwa Waziri analijua hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yake ya swali namba 19 la Sera ya Maendeleo Endelevu ya Viwanda ya Viwanda 1996/2020 Mheshimiwa Waziri alisema, juhudi zinafanyika ili viwanda vilivyosimama vifanye kazi. Mheshimiwa Waziri anieleze, juhudi hizi zipo katika hatua gani za utekelezaji? Mheshimiwa Rais aliwapa matumaini Wana-Lindi na kuwaambia atahakikisha viwanda vinafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nangependa Mheshimiwa Waziri anieleze, Maafisa Biashara wana kazi gani katika Halmashauri zetu? Hatuoni chochote wanachofanya zaidi ya kusimamia ukataji wa leseni za biashara; kingine ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.