Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa nimpongeze Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara pamoja na timu yote kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kwangu nitatoa tu ushauri wa kuongeza mapato katika Wizara hii. Nchi yetu hii imejaliwa misitu mingi sana na misitu hii imejaa miti dawa na mimea dawa. Ndiyo maana hata imefikia hatua ina maana tumekabiliana na ugonjwa huu wa Covid-19. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inasikitisha sana, Wizara imeangalia mali hizi bila kuzifanyia kazi, hata katika taarifa yake hotuba ya Mheshimiwa Waziri hakuna sehemu iliyotaja miti dawa, hakuna sehemu iliyotaja dawa zetu za asili. Nimwombe sasa, naamini ametaja tu eneo ambalo kwa kweli ni la vinyago, kwamba vinyago viwekwe kwenye maduka ya utalii. Nishauri kabisa na dawa za asili ziwekwe kwenye pharmacy za kitalii. (Makofi)

MHE: FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niende moja kwa moja …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Shekilindi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Flatei Massay.

T A A R I F A

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa ndugu yangu Shekilindi asisahau ku-declare interest kwamba yeye pia ni mtalaam na ana madawa hayo kupitia hiyo miti mishamba, hiyo ya Covid na sisi tumetumia humu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kwa ile kanuni yetu hawezi kusema hayo kwamba yeye ana maslahi kwenye hilo jambo, kwa sababu yeye anachangia kuhusu misitu yote, maana ukisema una maslahi lazima ututajie kiasi gani, sasa yeye si anauza dawa yake jamani inaitwa Shekilindi, watu wakanunue huko.

Mheshimiwa Shekilindi malizia mchango wako.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, mimi sikutaka kufanya hivyo kama Massay anavyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kuishauri Serikali sasa, kwamba watalaam wetu washirikiane na watalaam kama sisi kuhakikisha kwamba tunaanzisha viwanda vya kutengeneza dawa zetu hizi. Pia kama unavyofahamu nchi za wenzetu Ulaya kule wanakuja kuchukua miti yetu huku na anaenda kutengeneza dawa, sisi ndugu zangu tupo wapi na nchi hii ina watalaam ambao ni wabobezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Serikali yangu Tukufu kwamba, hebu sasa watalaamu wakae na sisi tuhakikishe kwamba tunaenda kujenga viwanda, then tunaenda kutengeneza dawa zetu, ukizingatia sasa hivi deni, Wizara ya Afya inadaiwa na MSD mamilioni ya fedha, karibu asilimia 93 za dawa zinatoka nje, lakini tukishajenga viwanda vyetu hivi kwa sababu raw materials zetu tunazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, basi niishauri Serikali kwa kweli isichukulie jambo la mzaha kwamba asilimia 93 hizo hatuwezi tena kwenda kuzichukua nje tuna uwezo wa kujenga viwanda vyetu hapa na dawa za kutosha zikatengenezwa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo niiombe Serikali iwe serious juu ya jambo hili, kwa sababu watu wanasema sijui nini taharuki ndiyo maana sasa hivi hapa hatuvai barakoa kwa sababu dawa za Corona zipo kwa watu ambao ni watalaam wa dawa za asili. Kwa hiyo, Serikali iwashike mkono watu hawa, iwaboreshee ili pato la Serikali hususan Wizara hii kama inaingiza asilimia 17, basi naamini itapiga mara mbili asilimia 34. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Serikali iwe serious juu ya jambo hili, iwashike mkono watu hawa ili wazungu nao washike adabu kwetu, wajue kabisa kwamba Watanzania nao kumekucha, siyo wachukue mizizi yetu, waende wakatengeneze dawa then waje watuuzie sisi. Mfano, nchi ya Nchi ya China, Bara la Asia inatengeneza dawa zao za asili, lakini sisi tunakimbia kivuli chetu, kwa nini? Hivi tumerogwa na nani, namwomba sana Mheshimiwa Waziri alichukue hili ili akae na wataalaam kama sisi na watalaam hao tunaamini wa nchi hii ni waelewa na wana uwezo mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu sasa ingekuwa Wizara haina…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele imegonga.

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)