Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami namshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kwa kutupa afya ili tuendelee kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukuwe nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, Naibu wake, Katibu Mkuu na watumishi wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kutafuta uwezo na kuuweka katika utaratibu wa kuwezesha miradi ya Serikali ambayo inategemewa na Umma wa Watanzania kutelekelezwa kutokana na makusanyo ya kodi. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa nikiwa na nia ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Fedha kwenye suala zima la riba za mabenki. Mwelekeo wa sasa wa uchumi wa Taifa letu unategemea sana mchango wa sekta binafsi. Sekta binafsi inatutegemea sana kufanya mambo mawili makubwa; la kwanza ni kutengeneza sera ambazo zinaitambua sekta binafsi na kuiwezesha kufanya kazi zake. Sera bahati nzuri tunazo nzuri, sheria tunazo nzuri na taratibu tunazo nzuri na tunaendelea kuzirekebisha kila inapoonekana inastahili kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa katika hii sekta binafsi ni uwezeshaji; kuiwezesha kuchangia pato la Taifa. Katika uwezeshaji huu, chombo kikubwa cha kuwezesha sekta binafsi ni mabenki yetu. Nasikitika kusema kwamba mabenki yetu hayajawa katika mwelekeo mzuri wa kusaidia sekta binafsi na hasa kwa riba kubwa zilizopo kwenye mabenki ambazo zimekuwa mzigo mkubwa kwa sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, benki zetu kwa sasa zinatoza riba kati ya asilimia 13 mpaka 21. Kiwango hiki cha riba ni kikubwa sana, lakini ukiacha riba unakwenda kuomba mkopo kwenye benki, unaambiwa kuna kitu kinaitwa processing fee. Hiyo processing fee, wanakwenda kwenye computer wanabadili majina kutoka kwenye mkataba wa mtu mmoja kwenda mtu mwingine wanabadili figure, maandishi ni yale yale halafu wanakutolea hiyo copy ya mkataba wa wewe na benki, unaweza ukafika mahali ukailipia mpaka shilingi milioni tatu au milioni nne. Huo ni mzigo mkubwa kwa wafanyabiashara wetu, na hatuwezi kusaidia sekta binafsi kwa stahili hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kitu kinaitwa insurance. Sasa unashangaa, insurance hii wakati mwingine anatozwa anayekwenda kuomba mkopo wakati risk za mkopo ziko sehemu mbili; risk ya kwanza ni ya benki inayotoa fedha kumpa huyo mkopaji na risk ya pili ni ya mkopaji ambaye ameweka kitu chake collateral ili apate mkopo, lakini wanakwambia wewe nenda kalipe insurance. Hata ukimaliza hiyo mikataba wanakwambia peleka kwa mwanasheria. Ukipeleka kwa mwanasheria, gharama za mwanasheria unalipa wewe, lakini unakuta kuna processing fee, unalipa hapo.

Mheshimiwa Spika, kubwa ninalotaka kulieleza ni kwamba benki zetu bado riba zake ziko juu, haziwezi kusaidia sekta binafsi kukua. Hili nalisema kwa sababu nafahamu kwamba Wizara ya Fedha kupitia BoT ndiyo wanaopitisha hizi riba za mabenki. Maana siku moja nilikuwa na kiongozi mmoja wa Serikali, kasimama kwenye function moja analaumu mabenki kwa riba, mimi nikamwandika kameseji, lakini zimepitishwa na BoT.

Mheshimiwa Spika, hakuna benki hata moja inayojipitishia riba yenyewe, lakini BoT wanatufanyia kama hadithi ya kilio cha mti. Mti uliona mashoka yanapita yametoka dukani, wakawa wanasema yanakuja kutumaliza. Mti ukamwambia hapana, hayawezi kutumaliza hayo mashoka mpaka ifike mahli yawekwe mpini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi chombo chetu cha Serikali ndiyo kinachoshirikiana na mabenki kuwakandamiza hawa watu wa sekta binafsi. Kitu hiki hakiwezekani. Nataka Waziri atakapokuja hapa atueleze kwa kweli vizuri na kwa kutulia, ni namna gani watasaidia sekta binafsi kukua kwa kupunguza riba za mabenki?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, hili lina mifano mingi tu…

SPIKA: Ndiyo Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nataka tu nimpe taarifa mzungumzaji anayeendelea kuzungumza kwamba kitendo cha Serikali kupitia Benki Kuu yetu, kukopa kupitia bond kwa asilimia 15.95, hiyo inayahamasisha mabenki kuikopesha Serikali badala ya kukopesha wananchi. Ahsante sana.

SPIKA: Taarifa hiyo unaipokea?

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, naipokea vizuri sana kwa mikono miwili. Naomba niendelee na mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, ninayo mifano midogo ninayoweza nikaitoa hapa, maana hata sisi wengine tumeamua kuingia kwenye mikopo. Unaweza ukafika mahali ukajiuliza katika hali ya kawaida, mikopo kama ya asilimia 20, 18; mikopo yenye asilimia ndogo kama ya kwetu yenye government quarentee asilimia 13; unaweza ukajiuliza, hivi mtu unaweza ukampa shilingi milioni 200 au 300 halafu akafanya biashara, akakulipa wewe shilingi milioni 69 naye akapata faida? Kwa biashara gani kubwa ya namna hiyo? Hilo ndilo jambo kubwa la kujiuliza. Unafika mahali unamkopesha mtu, halafu ujiulize, huyu akitoa hii riba yangu, halafu naye atajilipa mshahara, halafu atatengeneza faida awe ameendelea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii nimesikia kwenye vyombo hapo kwamba Benki ya NMB inakwenda kugawana faida ya shilingi bilioni 60. Ni jambo la kushukuru na kufurahi benki kwamba yetu imetengeneza faida, lakini jambo la kujiuliza Serikali ni kwamba hao waliotengeneza hiyo faida wamebakije? Hao ambao hiyo Benki ya NMB inawakopesha ambao ni wateja wake wamebakije? Au inafurahia kusikia benki imetengeza faida bila kujali kwamba wale wateja wa benki hiyo nao wamebaki katika hali ambayo imewaendeleza au imewadidimiza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnaweza mkawa mmeitengeneza faida ya benki lakini mmewauzia watu majumba, mmefika mahali mmewaacha wananchi wenu taabani. Halafu kubwa zaidi tunalokuja kuambulia ni kugawa neti kwenye hospitali wodi mbili, mnagawiwa neti. Wanasema benki imerudisha faida kwa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze, katika kipindi hiki ambacho tunataka kuinua sekta binafsi, isaidie kukuza uchumi wa Taifa, ni namna gani mabenki yameandaliwa kushusha riba ili kuwezesha sekta binafsi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka kulizungumza ni hizi microfinance institution. Kuna vikampuni vimetengenezwa vya kukopesha wananchi, sijui hata nani anaye-control? Sijui ni BoT, sijui vimeachwa huru? Unaweza ukakopa shilingi milioni tano, unakalipa shilingi milioni 12.

MBUNGE FULANI: Kweli!

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Wana kitu kinaitwa compound interest. Kadri unavyochelewa, inaenda inazaa na hii deni na hii inazaa, yaani ni matatizo makubwa, watu wamenyang’anywa vitanda. Ukienda kwenye ofisi za hizo microfinance, utakuta vitanda, mafriji, magodoro, sijui nini? Wizara ya Fedha iko kimya, watu wake wananyonyolewa.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: …BoT iko kimya.

SPIKA: Mheshimiwa Kilumbe, upokee taarifa. Ndiyo.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ninampa taarifa mzungumzaji kuwa siyo tu kwamba wanachukua vitanda na magodoro, wanachukua ATM cards za hao watu wanaowakopesha na walioathirika zaidi ni walimu. Kwa hiyo, ATM cards zinakaa kwenye hizo ofisi, mishahara ikiingia wao wanatumia kuchukua pesa. Kwa hiyo, ni hali mbaya sana.

SPIKA: Mheshimiwa Kilumbe, pokea hiyo taarifa, na ninakuongezea dakika moja ufafanue hili jambo vizuri kwa sababu ni tatizo kubwa. Hata kule Kongwa walimu wangu wana hali ngumu kwa sababu ya hawa watu. (Makofi)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza naipokea taarifa hii, ni taarifa nzuri na inaendana na mchango wangu. Lakini vilevile nakushukuru kwa kuniongeza dakika hiyo, na nilitaka kuzungumza kidogo jambo la mfano kwa ajili ya Timu ya Wananchi, sitazungumza tena. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli jambo hili lazima niseme wote sisi tunalifahamu maana sisi ni wawakilishi wa wananchi, lazima Waziri atakaposimama hapa atueleze hizi microfinance institutions zinazozaliwa kama uyoga. Umefanya vizuri kwenye mabenki, mabenki mengine mitaji ilikuwa inadondoka na nini, mabenki mengine umeyafungisha ndoa yamekuwa pamoja; sasa tuambie kwenye hizi microfinance institutions unafanyaje. Kwa kweli ni msalaba mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ninataka niseme baadhi ya wazabuni kama alivyokuwa anasema dada yangu, Mheshimiwa Halima hapa, baadhi ya wazabuni wa Serikali wamekopa kutoka kwenye mabenki. Mikataba yao na mabenki iko palepale, Serikali haijawalipa, huku riba zinaendelea. Wengine wamefika mahali wamekuwa taabani.

Mheshimiwa Spika, sitaki kusema kama dada yangu, Mheshimiwa Halima, maana yeye ana lugha zake; anauliza, hii ni akili? Kwa sababu sisi tuliolelewa vizuri ukisema siyo akili maana yake unasema yule anayefanya hivyo hayuko sawasawa, na naamini wote hao wanaofanya hivi wana akili nzuri sana. Isipokuwa nauliza; ni busara? (Makofi/Kicheko/ Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, narudia kuuliza; hivi ni busara kweli kufika mahali mtu kawapa huduma, amekopa benki anakuja na karatasi yake, jamani naendelea kudaiwa, na ninyi ama hamuhakiki deni lake au hata mkihakiki hamumlipi, anaendelea kudaiwa, riba inaendelea kuchajiwa. Hata mkija mkimlipa hana tena cha kurudisha mfukoni mwake. Kwa hiyo, ninataka niseme…

SPIKA: Wizara ya Fedha, Mbunge anauliza tu, ni busara kweli hii? (Makofi)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, la mwisho nataka nimalizie hapa ni utaratibu wa kutoa fedha za miradi kwenda mikoani na katika wilaya. Atanisaidia Waziri wa Fedha; kulikuwa na utaratibu kwamba tukishapitisha bajeti hapa kwamba tumetenga kifungu hiki cha fedha kwa ajili ya mradi fulani, pesa hizo zinapelekwa mkoani. Sasa hivi mpaka mchakato uanze kule, kazi itangazwe, BOQ zitengenezwe, huko wakati mwingine wataalam wenyewe hatuna, BOQ zinachelewa kutengenezwa, pesa zinachelewa kuombwa.

Mheshimiwa Spika, ninauliza; kwani kuna tatizo gani la kufika mahali tukazingatia kasma iliyokwisha pitishwa na Bunge tukapeleka fedha hizo huko?

Mheshimiwa Spika, kwa sababu Waziri amemteua dada yangu pale kuwa balozi wa… mimi sitaki aniteue, najiteua mwenyewe kuwa balozi wa kutetea kupunguza riba kwa wananchi. Ahsante sana.