Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana katika Wizara hii kwa hotuba yake. Nampongeza sana kama mwanamke kwa kazi nzuri anayoifanya na nazidi kumtia moyo kwamba wanawake wote wa Tanzania wanamtegemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la afya, tunafahamu kwamba afya ni kila kitu katika maisha ya mwanadamu. Tunapozungumzia afya, tunafahamu kwamba bila ya kuwa na afya huwezi kufanya jambo lolote la kuleta maendeleo. Tunakumbuka kabisa kwamba mojawapo ya mambo yaliyokuwa yakipigiwa kelele ni suala la maradhi na maradhi haya ndiyo maana tunasisitiza sana suala la afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kuipongeza Wizara ya Afya na hasa Serikali kwa kuleta Mfuko wa Bima ya Afya. Pamoja na hayo, naomba nizungumzie machache hasa changamoto zilizopo katika Mfuko wa Bima ya Afya ambayo kwa namna moja au nyingine, umekuwa ni kikwazo kwa baadhi ya wanachama wanaokwenda kupata huduma ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na vizingiti kwa maana kwamba katika baadhi ya card hizi za Bima wanapokwenda kupata huduma ya afya na hasa kama tunavyosisitiza siku zote, ni vyema kwa mwananchi kujua afya yake. Atakapojua afya yake, anajua kabisa kwamba yeye ana matatizo gani ili aweze kukabiliana nayo mapema ili aweze kupata matibabu mapema. Wanachama wengi wa Mfuko wa Bima ya Afya wanalalamika kwa sababu wanapokwenda kwa ajili ya kufanya check-up ya miili yao, wanakataliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanakataliwa pamoja na kwamba wao ni wanachama wazuri na wamekuwa wakichangia. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa, atuambie ni kwa nini Mfuko wa Bima ya Afya umekuwa ukiwakatalia wanachama kuangalia afya zao ili waweze kujua na pengine kuchukua hatua mapema kutokana na matatizo wanayoyapata? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la dawa pia; kama Mfuko wa Bima ya Afya wamekubali kubeba dhamana ya Watanzania, kwa nini wazuie baadhi ya dawa wasizitoe wakati wanachama wote wanaotibiwa wanachangia Mfuko huo? Namwomba Mheshimiwa Waziri na naishauri Serikali na Waziri, atakapokuja kuhitimisha, atueleze ni kwa nini Mfuko huu wa Bima ya Afya umekuwa na hivyo vikwazo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kwa Madaktari. Madaktari pesa waliyopangiwa na huo mfuko wa afya kama consultant fees wanalipwa sh. 2,000/=. Hivi kwa wakati huu tuliopo na Madaktari hawa ambao ni wataalam wetu, tunawategemea, mabingwa, hivi kweli unakwenda kumlipa sh. 2,000/=! Ni aibu kwa Mfuko wa Bima ya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia Mfuko wa Bima ya Afya, naomba moja kwa moja niende katika masuala ya watu wenye ulemavu. Nawapongeza Wabunge wote ambao wamezungumzia suala la watu wenye ulemavu na hasa katika Mfuko wa Bima ya Afya na kuona umuhimu wa wao Serikali kutoa kipaumbele kwa watu wenye ulemavu kupata card za Bima ya afya ili waweze kutibiwa. Nawapongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nawaomba pia Wabunge wengine katika Majimbo yao waone umuhimu wa kuwachangia hawa watu wenye ulemavu ili basi wanapokwenda hospitali wasipate tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la vifaa saidizi. Tunafahamu kabisa ulemavu siyo kulemaa; na katika ulemavu unapomsaidia mtu mwenye ulemavu vifaa saidizi kwa wale wanaovitumia, tayari umepunguza vikwazo. Isipokuwa katika Bima ya Afya wanapokwenda, bado halipo. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri alione hili kwamba ni muhimu na aone ni kwa jinsi gani atawasaidia watu wenye ulemavu ili waweze kupata vifaa saidizi na kuweza kutimiza majukumu yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine naomba nizungumzie katika hospitali zetu na hasa wanawake wenye ulemavu wanapokwenda kujifungua. Vitanda siyo rafiki; na wakati mwingine hata Madaktari wenyewe au Manesi kwa namna moja au nyingine kauli zao siyo nzuri. Wanapowaona watu wenye ulemavu na hasa mwanamke amekwenda ni mjamzito, maneno ya dhihaka yanakuwepo mengi. Hivi katika suala la mama kumleta mtoto, hata kama mtu ni mlemavu hana ule uhitaji? Kwani wana kasoro gani? Si wanayo maumbile kama wengine? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba, nasimama mbele yao kama mwanamke mwenye ulemavu na naomba kuwatetea hawa, kuwasilisha kilio chao kwa sababu sio wote ambao wanaweza kufika huku na kuwasilisha kilio chao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia masuala ya watu wenye ulemavu, wana changamoto nyingi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hili pia, aangalie ni kwa namna gani basi tutafanya, kama ni kutoa elimu ili kwa namna moja au nyingine lugha hizi waziangalie, wasiwadhihaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuone umuhimu na hasa nimwombe Mheshimiwa Waziri kuona umuhimu wa kuweka Wakalimani katika hospitali zetu. Wanapokwenda watu wenye ulemavu hasa viziwi, inakuwa ni vigumu kwa wao kuweza kuwasiliana. Lugha inakuwa ni gongana! Kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Waziri, wakati mwingine tunapoajiri basi tuone umuhimu wa kuajiri hawa watu ambao ni wakalimani wa lugha za alama ili waweze kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Zahanati ya Nduruma. Zahanati hii ya Nduruma tayari imepandishwa hadhi na kuwa Kituo cha Afya. Zahanati hii inahudumia Vijiji vya Marurani, Manyire, Mlangarini na maeneo mengi katika Mkoa wa Arusha, Wilaya ya Arumeru; lakini mpaka hivi sasa hakuna wataalam na hakuna gari la wagonjwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, inakuwa ni tatizo kwa hata akinamama wanapokuwa wajawazito kwenda hospitali ya Mount Meru inakuwa ni shida, wanajifungulia njiani. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aone umuhimu na hasa Waziri mwenye dhamana kutuletea gari la wagonjwa katika Zahanati ya Nduruma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la watoto wa kike kwa sababu mimi ni mdau na vile vile niungane na ndugu yangu Mollel aliyesema kwamba shujaa ni yule anayejali mtoto wa kike. Katika shule zetu nyingi, watoto wa kike kwa mwezi hawaendi shule kati ya siku nne mpaka siku kumi. Naomba tu Mheshimiwa Waziri na nimwombe pia kwa sababu Waziri wa Fedha yuko hapa, aone basi umuhimu wa kupunguza…
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naunga hoja mkono.