Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii nami katika Bunge hili niweze kuchangia Wizara inayoamua Watanzania leo tuendelee kuishi ama la. Wizara ya Afya ni Wizara nyeti sana, ndiyo inayosababisha sisi leo tuko humu ndani tukiwa na afya njema pamoja na Mwenyezi Mungu kutujalia. Wizara hii ni Wizara ambayo bado inachechemea. Wizara ambayo inakwenda kuamua hatima ya maisha ya Mtanzania, bado tunakwenda kuiletea mzaha na kufanya ushabiki kwenye maisha ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni takribani miaka 55 ya uhuru, hatuna Vituo vya Afya ndani ya Kata zetu 3,990. Tuna vituo vya afya ambavyo havifiki 500, halafu tuko humu ndani leo tunajisifu, tunapongezana kwa makofi eti kana kwamba tunakwenda kufaulu. Hatufaulu, tunarudi nyuma na tunaendelea kutokuwatendea haki Watanzania. Hali ya hospitali zetu kwenye maeneo yetu tunakotoka; tuachane na hospitali hizi za mjini, hebu twende kule vijijini. Mheshimiwa Waziri hotuba yake nikiiangalia na kuisoma imelenga maeneo ambayo yako hapa mbele yetu. Haijatugusa kule vijijini!
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijijini hospitali zetu zinasikitisha, zinatia huruma, wananchi wetu wanapata tabu. Hospitali zisizokuwa na maji! Hospitali zisizokuwa na umeme. Mbali na maji na umeme, lakini hospitali hizi hazina Wauguzi, hazina Madaktari, hazina madawa! Tunawatakia nini hawa Watanzania? Shida yetu ni nini? Si mtwambie Chama cha Mapinduzi miaka 55 mmeshindwa kuleta hoja ya msingi ya kuweza kuokoa maisha ya Watanzania! Tunabaki tunapigiana makofi humu ndani! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuachane tu na suala zima la hali mbovu za hospitali, uwepo wa hizo hospitali zenyewe! Mkoa wangu wa Dodoma wenye Wilaya saba, tuna Wilaya nne tu ndiyo zina hospitali; Wilaya tatu hizi hazina Hospitali za Wilaya. Mnaweza mkasema Wilaya ya Chemba ni mpya, Wilaya ya Bahi ni mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chamwino ambayo awali ilikuwa inaitwa Wilaya ya Dodoma Vijijini mpaka leo ambako Ikulu ipo ya Chama cha Mapinduzi, hawana hospitali wale wananchi! Wanatoka Vijiji vya Chamwino, Mtera huko imepakana na Iringa wanasafiri kuja Manispaa ya Dodoma kupata huduma. Hivi mnawatakia wema kweli hawa Watanzania wa Mkoa wa Dodoma? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambieni tu ndugu zangu, katika mikoa ambayo inawakoa, bado inasuasua ni Mkoa wa Dodoma ndiyo ambao angalau mnaambulia, lakini Waswahili wanasema usimwamshe aliyelala, utalala mwenyewe. Ipo siku wananchi hawa watakuja kuchoka na mateso na ahadi kila kunapokucha, mnaenda kuwaahidi kwamba tutawaleteeni hospitali ambazo hamzipeleki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma zinazotolewa kwenye hospitali zetu, wenzangu wamesema, naomba niongezee. Niende huduma zinazotolewa kwenye huduma ya mama mjamzito. Huduma zinazotolewa kwenye hospitali zetu kwa mama mjamzito, zinawakatisha tamaa wanawake kwenda hospitalini ndiyo maana wengine wanaamua kuzalia majumbani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wa kike ambao hawajafikisha umri wa miaka 18 kwa Dini ya Kiislamu mtoto anaweza kuolewa hata miaka 14, 15, 16; mtoto huyu akiolewa akipata ujauzito akienda hospitalini kwa ajili ya kujifungua, hapewi huduma. Atapewa kashfa kibao, atapewa matusi ya kila aina na kumsababishia mtoto yule hata kukosa ujasiri wa kwenda kutimiza wajibu na jukumu lake katika Taifa lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lugha hizi zinatusababishia vifo vingi vinavyokwenda kuwapoteza akinamama, vinavyokwenda kuwapoteza watoto ambao tunahitaji kesho na wao waje watupokee mzigo huu tulionao katika Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wanawake ambao wana umri mkubwa kuanzia miaka 40, hawa nao imekuwa ni changamoto kwenye hospitali zetu. Wakifika Hospitalini, “limama jitu zima, limebebelea limimba mpaka leo linazaa! Hizo ni lugha ambazo zinatolewa na wafanyakazi wetu kwenye hospitali zetu. Mheshimiwa Waziri wewe ni mwanamke, unajua uchungu wa kuzaa…
MWENYEKITI: Siyo wote ni baadhi! Ni baadhi, siyo wote!
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni baadhi!
Mheshimiwa Waziri unajua jinsi wanawake tunavyopata tabu, lakini kuna mwanamke mwingine yawezekana kwenye usichana wake amehangaika kupata mtoto ameshindwa. Imefika umri wa miaka 40 huyu mtu kabahatika kupata hiyo mimba, asizae? Kwa nini baadhi ya hawa watumishi wasipewe onyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona wiki iliyopita Mbeya, Muuguzi alichomtendea yule mama aliyekuwa anajifungua pale, Mkuu wa Mkoa alikwenda pale hospitalini. Yule mama anaeleza kwa uchungu namna alivyofanyiwa na mhudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli tunataka kuwatendea haki hawa wanawake? Tunataka kweli wanawake hawa waendelee kuja kwenye hospitali zetu kwa ajili ya kupokea kejeli, matusi na kashfa! Ya kazi gani? Vifo vya wanawake vinasababishwa na hizi kashfa; wanawake wengi wanashindwa kwenda hospitali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake pia tunashindwa kwenda Hospitali kujifungua mahali salama; siyo salama, pale napo tunakwenda kutafuta vifo vingine. Ukienda hospitalini, kaka yangu Mheshimiwa Kuchauka amesema, unaambiwa mwezi wako wa mwisho, mwezi wa Nane unaenda wa Tisa kwenda kujifungua, utaambiwa unapokuja njoo na ndoo; maeneo ambayo hayana maji, anaambiwa aende na maji mama mjamzito. Maeneo ambayo hayana umeme, mama anaambiwa aende na taa au mafuta ya taa ili aweze kupata huduma ya kuweza kutimiza wajibu wake na majukumu katika Taifa letu ya kuongeza Watanzania katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, CHF, janga la Taifa hili. Tunawatwisha Watanzania mzigo juu ya mzigo. Mmeshindwa kupeleka dawa; ili mjifiche kwenye kichaka, mmeamua kuwaundia mradi unaoitwa CHF mwendelee tena kukusanya fedha zao, wakienda hospitalini hakuna dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, CHF hii watu wetu wamekwenda kujiunga; akienda hospitali na kadi ile akifika fursa pekee anayoipata kwenye ile kadi ama huduma pekee ni kwa ajili tu ya kumwona Daktari. Akitoka kwa Daktari, amepata dawa ni paracetamol. Awe anaumwa tumbo atapewa paracetamol, awe amevunjika mguu atapewa paracetamol, awe anaendesha atapewa paracetamol. Ugonjwa wowote huduma pekee atakayoipata ataambiwa paracetamol ndiyo dawa atakayoipata pale, akipata bahati sana ya kupata dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huyu mwananchi anauliza, hivi nimeambiwa na Serikali yangu nijiunge kwenye Mfuko huu ili niweze kuokoa maisha yangu. Hata pale ninapokuwa sina fedha nipate huduma, lakini leo hii wananchi wetu wametoa fedha zao na badala yake wanaenda kuambulia maneno ama kuoneshwa maduka ya kwenda kununua dawa. Mradi huu siyo rafiki kwa Watanzania. Mheshimiwa Waziri tunaomba aje na mbadala wa biashara hii ya CHF. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata miradi mingine ya Bima ya Afya, NHIF; ukienda na kadi ile, ukifika pale, kwanza kabla hata hujaitoa, unauliza jamani dirisha la Bima ya Afya liko wapi? Bima ya Afya? Eeh! Mhudumu anaweza akakukata kushoto akaendelea na safari zake. Kama uko kwenye foleni hujauliza chochote, unaulizwa; unatibiwa cash au una Bima? Ukimwambia una Bima, anakwambia subiri, kaa pale! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wenyewe Wabunge imetutokea, mimi nikiwa ni mhanga. Nimeenda Dar es Salaam Agakhan pale. Nimefika nikawaambia naumwa, nina Kadi ya Bima ya Afya – NHIF. Nikaambiwa, dada tunaomba usubiri pale. Nilisubiri zaidi ya dakika 45, nikaona haina sababu ni heri ninyanyuke nijiondokee zangu nikatafute hospitali nyingine nitoe fedha niweze kutibiwa. Sasa sisi kama tuko humu ndani yanakuwa namna hiyo na hizo kadi zenu mlizotupa, walioko kule nje hawa ambao mnawakatia hivi vikadi vyenu inakuwaje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)