Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia. Kwa sababu nachangia kwa mara ya kwanza, naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa kwake lakini kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwapa moyo Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kumpongeza Makamu wetu wa Rais Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu, kwa kuwa Makamu wa Rais, mwanamke wa kwanza Tanzania kuwa nyadhifa kubwa katika nchi yetu na imeweza kutupa heshima kubwa wanawake wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu na Baraza lake Tukufu la Mawaziri kwa kuchaguliwa kwao lakini kwa kuthibitishwa kwake Waziri Mkuu katika Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nami naendelea kumwombea kwa Mwenyezi Mungu ili aendelee kumwongoza aweze kuwatumikia Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ya kipekee kabisa niwashukuru wapiga kura wanawake wa Mkoa wa Lindi, UWT wa Chama cha Mapinduzi kwa kuniwezesha leo nikawa ndani ya Bunge lako Tukufu, nami nawaahidi kuwatumikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nachukua nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa Hotuba yake nzuri aliyoitoa ambayo imeelekeza mipango ya utekelezaji wake kwa kipindi hiki kitakachoanzia 2016/2017, hotuba ambayo inatupa matumaini makubwa katika kuhakikisha afya za Watanzania zinaboreka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza sana jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Nne katika kuboresha huduma ya afya nchini kwetu. Tunajua na tumeona mafanikio makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Nne, mafanikio hayo ndiyo ambayo yatazaa matunda mema katika kipindi hiki kinachokuja cha 2016/2017. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo makubwa tuliyoyaona, lakini bado tuna changamoto kubwa nyingi katika maeneo mbalimbali. Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea changamoto mbalimbali zilizopo katika Majimbo yao lakini zilizopo ndani ya mikoa yetu. Napenda kuongelea changamoto kubwa ambazo zimo katika Mkoa wetu wa Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo hospitali ya Mkoa wa Lindi Manispaa inayoitwa Sokoine Hospital. Hospitali hii ina changamoto kubwa sana, changamoto kubwa tunajua kwamba Hospitali ya Mkoa wateja wake wakubwa ni wagonjwa kutoka katika maeneo mbalimbali ya Wilaya mbalimbali zilizopo katika Mkoa wa Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Sokoine, ina wagonjwa wengi sana, lakini Madaktari waliokuwepo ni wachache, kwa hiyo, inasababisha wagonjwa kushindwa kupata huduma kwa wakati kwa sababu tu ya mlundikano wa wagonjwa wengi kwa kukosa Madaktari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunalo tatizo kubwa la Madaktari Bingwa wa Wanawake. Wanawake tunapata matatizo makubwa sana na wengi wanapoteza maisha kwa sababu tu ya kukosa huduma iliyokuwa stahiki. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri alitazame kwa jicho la huruma suala ili Mkoa wa Lindi tuweze kupata Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapokuwa na Daktari Bingwa katika Hospitali ya Mkoa itanusuru wanawake wengi kutoka wilaya mbalimbali. Kwa hiyo, tunaomba sana tuweze kupata Daktari Bingwa katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto nyingine kubwa ya kutokuwa na miundombinu iliyo kuwa mizuri ya majitaka na majisafi. Hospitali ile ya Mkoa wa Lindi tunajua ni hospitali kongwe, ni hospitali ya muda mrefu, miundombinu yake ya maji imekuwa michakavu sana na kusababisha katika wodi ya wazazi kukosa maji na Mheshimiwa Waziri ni mwanamke, anajua maji yalivyokuwa muhimu katika wodi ile ya wazazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba kwa dhati kabisa suala hili la kufanya ukarabati wa miundombinu katika hospitali yetu ya mkoa, Serikali itusaidie kuhakikisha miundombinu ile inabadilishwa na kuwekwa miundombinu mingine. Katika Hospitali ya Mkoa wa Lindi naisemea sana ile kwa sababu ndiyo inabeba wagonjwa wengi kutoka katika maeneo mbalimbali ya Wilaya za Mkoa wa Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo mashine ya endoscopy, mashine ile inakosa mtaalam na kusababisha mashine ile kukaa muda mrefu bila kutumika lakini wagonjwa wanakosa tiba kwa kukosa mtaalam ambaye anaweza kutumia mashine ile. Kwa hiyo, tunamwomba Mheshimiwa Waziri atutazame kwa jicho la huruma ili tuweze kupata mtaalam atakayeweza kuiendesha mashine ile ili wagonjwa wa magonjwa haya ya vidonda vya tumbo waweze kupata tiba kwa wakati muafaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya mbalimbali tumeona Wilaya nyingine zimekosa kuwa na Hospitali za Wilaya, ni pamoja na Lindi Manispaa. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya hitimisho lake atueleze ni namna gani ataweza kuzisaidia Wilaya hizi ambazo hazina Hospitali za Wilaya ili Wilaya hizi ziweze kupata hospitali na wanawake na watoto waweze kupata huduma hizi za afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ambayo imeongelewa na Waheshimiwa Wabunge wengi ni ukosefu wa madawa katika hospitali zetu. Katika hospitali zetu za Mkoa wa Lindi zote zinakosa madawa. Tuna Wilaya sita katika Mkoa wa Lindi, ikiwepo Wilaya ya Liwale, Nachingwea, Lindi Vijijini, Kilwa, Lindi Manispaa pamoja na Ruangwa, tunakosa madawa ya kutosha na kufanya wagonjwa wakose madawa na hatimaye wengine kufa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba wananchi wetu wengi hawana uwezo wa kununua madawa katika maduka ya dawa. Wanapokosa dawa katika hospitali zetu za Serikali zinawafanya washindwe kupata tiba kwa wakati na kusababisha vifo vingi vya wanawake na watoto. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili la upatikanaji wa madawa katika hospitali zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mfuko huu wa Bima ya Afya. Nchi yetu sasa hivi tumeingia katika Mfuko huu wa Bima ya Afya na wananchi wetu tunawahamisha kuingia katika Mfuko huu wa Bima ya Afya. Suala hili Waheshimiwa Wabunge wengi wameliongelea, tunapata tatizo kubwa kwa sababu wanapokwenda hospitali wanapata maandishi tu na badala yake dawa wanakosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inawakatisha tamaa; na hata wale ambao wangependa kuingia katika mfumo huu wanapata hofu na kuacha kuingia katika mfumo huu wa Bima ya Afya. Kwa hiyo, naiomba Serikali ifanye jitihada zaidi ya makusudi katika kuhakikisha hospitali zetu nchini kote zinakuwa na madawa ya kutosha na tutakapofanya kampeni hii ya kuingia katika Mfuko wa Bima ya Afya, wananchi wetu watakuwa na matumaini ya kupata dawa katika mahospitali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala lingine la Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake katika Halmashauri zetu. Katika Halmashauri zetu tunatenga asilimia kumi; tano ya vijana na tano ya wanawake, lakini tumeona katika Halmashauri zetu nyingi hazina mapato ya kutosha na kupelekea pesa inayopatikana kuonekana kwamba ni kidogo haitoshelezi. Katika Majimbo mengine yana Kata zaidi ya 30. Majimbo mengine yana Kata 33, mengine yana Kata 30, na mengine Kata 35.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapokuwa na mapato madogo, mathalan unapata shilingi milioni 10 ya vijana na shilingi milioni 10 ya wanawake…
MWENYEKITI: Ahsante. Muda wako ndiyo huo, tunakushukuru.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.