Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, ya kuweza kuongea na Waheshimiwa Wabunge waliopo humu ndani na kupitia Bunge lako Tukufu kwa Watanzania wote. Nina mambo manne ambayo ningependa kuyasema. Jambo la kwanza nichukue nafasi hii kuishukuru sana, Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Kwa taarifa nzuri ambayo wamewasilisha mbele ya Bunge lako Tukufu. Wameainisha maeneo ambayo tumefanya vizuri na pale kwenye changamoto wametueleza ili sisi tuweze kutekeleza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuahidi, Wizara tumepokea ushauri huo na tutaenda kuutekeleza; na utekelezaji huo unaanza leo. Kwa hiyo, kuanzia kesho mkiona utekelezaji unaendelea, msishangae, Serikali hii ni Sikivu. Tunasikia maoni ya Waheshimiwa Wabunge na tunayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, watu wameongea sana na wanaendelea kuongea. Jambo moja lililoongelewa ni kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii inataka kuwapokonya ardhi Wamasai. Naomba nitoe angalau ufafanuzi kidogo. Tanzania hakuna mwenye ardhi, hakuna kabila lenye ardhi Tanzania, ardhi yote ni mali ya Mheshimiwa Rais. Kwa mujibu wa sheria tulizozitunga humu ndani, anaweza akaitwaa muda wowote. Haki ya wewe ambaye ardhi hiyo inatwaliwa ni fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wameongea Waheshimiwa Wabunge hapa kuhusiana na mambo ya fidia. Hii dhana ambayo inakwenda na mpaka vyombo vya nje vinaandika: “Government of Tanzania is Grabbing Maasai Land,” ni upotoshaji! Hakuna sheria hiyo. Tukienda huko tutarudi wakati wa ukoloni, tutasema Ngoni Land, Sukuma Land, Nyakyusa Land; tulishatoka huko toka mwaka 1963. Kwa hiyo, turudi kwenye msimamo, tuelewe mwenye ardhi ni nani; na mamlaka yake ni yapi kwa mujibu wa sheria ambazo tumezitunga? Tukitaka kumnyang’anya Mheshimiwa Rais mamlaka hayo, tuje tutunge sheria, tuseme kuanzia sasa ardhi imilikiwe na makabila kama zamani. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri hapo kwenye ardhi kumilikiwa na Rais, nadhani upaweke vizuri kisheria. Ardhi inamilikiwa na Umma, Rais anaishika kwa niaba ya Umma. Sasa isije ikaleta picha ambayo pengine inaweza kusababisha mkanganyiko. Ardhi ni ya Umma wote wa Watanzania lakini Rais anaishikilia hiyo ardhi kwa niaba yetu sisi sote. (Makofi)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa mwongozo wako. Nilichokuwa ninasisitiza hapa ni kwamba, kwa sababu ardhi ni ya Umma, hakuna kabila moja linalomiliki ardhi. Ni Umma wa Watanzania wote; ndiyo maana ukienda Zanzibar utawakuta Wangoni wanakaa kule; ukija Songea utawakuta Wamasai wapo kule, kwa sababu ardhi ni ya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya tatu ambayo ningependa kuiongea ni suala la haki za binadamu, limeongelewa sana hapa. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tazania inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ni Serikali inayojali haki za binadamu. Hatutafanya chochote kinyume cha haki za binadamu. Kwa kuwa tunaheshimu haki za binadamu, pia hatutaingilia uhuru wa vyombo vya habari kwa sababu ni haki za binadamu, lakini kama umekwazwa na vyombo vya Habari, mamlaka za kisheria zipo. Unaweza ukaenda Mahakamani au TCRA kwenda kuvishtaki. Ila Serikali ikikifungia chombo cha Habari, ni ukiukwaji wa haki za binadamu, hatutafanya hilo.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa kulisema, watu wameongelea hapa Sheria ya Ngorongoro ya Mwaka 1975. Toka imetungwa ni miaka mingi sana. Mliyoyaongea Waheshimiwa Wabunge yameonesha mapengo yaliyopo kwenye sheria ile. Msingi wa sheria ile ni nguzo tatu; nguzo ya uhifadhi, nguzo ya utalii na nguzo ya maendeleo ya jamii. Inaonekana nguzo hizi sasa zimeshindikana kushikiliwa kwa Pamoja. Kwa hiyo, sasa kwa mapendekezo ya Kamati na maoni yenu, sisi kama Wizara mapema iwezekenavyo tutaleta mabadiliko ya sheria hii na endapo Bunge hili Tukufu litaridhia, basi yataweza kupita na kuamua kwa mujibu inavyofaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nisistize kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo Mheshimiwa Rais amenipa mimi na Mwenzangu Mheshimiwa Mary upendeleo wa kuisimamia, tutahakikisha haki ya kila Mtanzania wakiwemo Wamasai walipo Ngorongoro inalindwa. Hakuna litakalofanyika kinyume cha sheria wala kuvunja haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge kabla hajawa Mbunge alishakuja ofisini akiwa Mwenyekiti na alikuja kuongelea haki za watu wa Ngorongoro. Hakuwa Mbunge lakini nilimpokea, tukakaa na tukaongea na nikamweleza msimamo kwamba tunapenda haya mambo yaende kwa kuelewana, kwa kukaa Mezani pasipo kumkandamiza mtu. Hiyo ndiyo approach ya Serikali, tufike sehemu tutatue tatizo pasipo kukwaruzana; wale wapate haki yao na Serikali ipate ambacho ni haki ili Ngorongoro isife. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii na ninawapongeza sana Kamati kwa taarifa hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)