Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami kwa jioni hii ili niweze kutoa mawili, matatu, lakini ili kuweka record sawa jina langu sahihi naitwa Mwanne Ismail Mchemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uwezo leo wa kuwa hapa na kuweza kupata nafasi ya kuchangia. Naanze na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya kuhusu suala zima la sukari. Nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la sukari tusiliangalie hivi hivi tu kwa lele mama, sukari inaathiri jamii nzima ya Kitanzania na ndiyo maana wanakamatwa sasa hivi kwa sababu ya laana ya Mwenyezi Mungu. Sukari hiyo inapofichwa inaathiri watoto, wagonjwa, wazee, wajawazito lakini siyo hilo tu kwamba eti kwa sababu ya mwezi wa Ramadhani, hawazidi kwa sababu ya mwezi wa Ramadhani; mpaka hivi leo ninavyokwambia kuna watu wanafunga. Kwa hiyo, inaathiri sehemu kubwa. Nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Mawaziri; nampongeza Mheshimiwa Waziri Ummy na kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla kwa kazi nzuri wanayofanya. Imeonyesha tangu walivyoteuliwa kwamba hawa watu wanatosha. Ni tumaini langu kwamba Wizara waliyopewa ni sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia. Maradhi ya wanawake yako mengi sana, ni vyema Wizara sasa ikaangalia kutoa kipaumbele kwa maradhi ya akinamama. Kwa mfano, kansa ya mfuko wa uzazi kwa wanawake ni tishio, ni balaa! Kuna kansa ya matiti nayo pia ni balaa! Kuna ugonjwa wa fistula, huo nao ni muziki! Watu wengi wanaachika kwa sababu hiyo. Bado elimu haijawafikia walengwa hususan vijijini. Vile vile kuna uvimbe kwenye tumbo la uzazi la wanawake; namwomba Mheshimiwa Waziri, magonjwa kama haya yapewe kipaumbele na kutoa elimu hususan vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza MEWATA. Mheshimiwa Waziri naomba Kitengo hiki cha akinamama walionesha ujasiri, MEWATA nadhani Serikali ingewapa support kubwa sana. Wamefika mpaka vijijini; ni Madaktari Bingwa ambao wamejiamini kuwasaidia wanawake. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri anaye Daktari, anajua umuhimu wa timu ya Madaktari wa MEWATA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, wodi za wazazi haziridhishi. Naomba wodi hizi ziangaliwe, zipewe kipaumbele, kwa sababu kuna matatizo makubwa, hususan vitanda vya kuzalia. Vitanda vya kuzalishia vijijini havipo? Anaambiwa tu kaa hapa, jipange na nini, wewe mama unajua, kwa sababu shule hii umeipitia, ni kiwanda nyeti. Kwa hiyo, naiomba Serikali kupitia mama yangu hapa iliangalia hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende moja kwa moja kwenye ukarabati wa majengo katika Hospitali ya Kitete, Tabora. Tuna matatizo! Kuna miradi ambayo ilishaanza, lakini haijakamilika. Naiomba Serikali ikamilishe miradi hiyo ili angalau sasa madhumuni ya kile chuo kuwepo yaonekane. Kuna wodi ambazo zipo hazijakamilika, nazo ni za akinamama, naomba Mheshimiwa Waziri, nilichangia kwa maandishi, lakini ziangaliwe pia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo kubwa la mashine ya kufulia nguo. Jamani, ile sasa hivi ni Hospitali ya Rufaa, hatuna mashine ya kufulia nguo na iliyopo ni ya zamani ukilinganisha na population ya watu sasa hivi, inahudumia Wilaya saba na wagonjwa wale wanakuwa referred kwenda pale, lakini mashine hakuna. Siyo hilo tu, pia uchakavu wa jiko, miundombinu yake ni ya tangu Ukoloni. Inawezekana hata mimi nilikuwa sijazaliwa bila shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaangalia, kwa sababu kuna watu wengine ambao wanatoka vijijini, hawana ndugu, lakini ameletwa pale kaachwa kwa sababu hakuna sehemu ya kuweza kusubiri wagonjwa. Kama chakula kitaandaliwa vizuri, basi hata wagonjwa wetu watapata nafuu. Kwa hiyo, uchakavu huo ni mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uchakavu wa jengo la wagonjwa, sijui wanaitwa wagonjwa wa akili, sijui lugha gani nzuri…
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wenye matatizo ya akili, ile wodi ya miaka mingi! Miundombinu yake hovyo, hakuna vyoo, yaani wale tusiwa-dump, wale nao ni wagonjwa kama wagonjwa wengine. Magonjwa haya hayana kuchekwa, mtu unaweza kupata ugonjwa huo au akapata ndugu yako. Kwa hiyo, naomba nchi nzima kuwe na mradi maalum ambao unaweza kutembelea wodi hizo. Ni tatizo kwa kweli! Ukienda pale yaani mpaka utawaonea huruma, wale hawakupenda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba na kusisitiza, wodi ya Kitete ya Kichaa, yaani ya wagonjwa wa akili, kwa kweli iangaliwe vizuri ili waweze kupata msaada, hawakupenda. Kwa hiyo, nilikuwa nataka nilisisitize hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kuzungumzia makazi ya wazee. Makazi ya wazee, nachukulia ya kwangu Mkoa wa Tabora kwa sababu nimezungukia, hayafai jamani. Tunaita makazi ya wazee lakini yalikuwa ya aina mbili; kuna wale ambao walikuwa na ugonjwa wa ukoma, waliambiwa wasitiriwe wakae mahali pamoja kwa ajili ya matibabu. Kuna wazee ambao hawajiwezi, nao makambi yao yapo, lakini huduma yao hafifu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, huduma kwa wale wa makambi ya wenye ugonjwa wa ukoma, wale jamani vifaa vingine vinafanya kazi. Ni wazima! Wamezaa na wanazaana na kuna watoto na wajukuu. Kwa hiyo, kama mna hesabu ya wazee, basi wapo wengine kwa sababu kazi ile wanafanya bado. Kwa hiyo, wanazidi kuzaana. Ukienda Kambi ya pale Ipuli kuna watoto wadogo, kuna vijukuu vipo mle. Kwa hiyo, naomba wasihukumiwe kwamba ni wazee, lakini bado mambo mengine wanaendelea nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Sheria ya Ndoa. Tumeambiwa kwamba Sheria ya Ndoa inafanyiwa marekebisho, lakini mpaka ikifika kufanyiwa marekebisho, akinamama wameumia, kwa sababu sheria ile inasema unapodai fidia ya mtoto, unalipwa sh. 100/= kwa sheria ya zamani. Kwa hiyo, akinamama wanateseka. Sheria hiyo pia gharama za fidia kwa akinamama wajane napo kuna matatizo wanapokwenda Mahakamani. Kwa hiyo, naomba pia sheria hii iangalie pia na mazingira ya wajane na mazingira ya watoto, kwa sababu ndoa zinapovunjika watoto wa mitaani wanakuwa wengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba suala hili la sheria hii ya mwaka 1971, Mheshimiwa Waziri ashirikiane na Mheshimiwa Waziri wa Sheria ili iweze kufanya kazi yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Maafisa wa Ustawi wa Jamii. Kwa kweli naomba wapewe vitendea kazi; wanunuliwe basi hata pikipiki ili waweze kuzunguka vijijini. Kama tunasema bajeti finyu, lakini hawa watu hawawezi kufanya kazi inavyotakiwa, inakuwa ni ngumu sana kwa sababu hawa watu ndio tunaowategemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nizungumzie kuhusu Benki ya Wanawake, nawapongeza. Benki ya Wanawake ni mwanzo, tuliianzisha mwaka 2009. Walioanzisha Benki ile kwa kusaidiana na Serikali walikuwa Wabunge wa wakati ule, walichangia sana. Nampongeza Mama Chacha kwa kazi nzuri anayofanya ila tuendelee kumwomba kwanza riba ipungue, lakini waende mikoa yote na ndiyo ilikuwa azma yake, kwamba wafungue madirisha kila mkoa ili angalau watu waende kwenye dirisha kwenye mabenki yale wafaidi, lakini sasa hivi wanafaidi upande mmoja tu na ndiyo ambao wanapata mkopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo asilimia 10, naomba Mheshimiwa Waziri, kwa sababu nayo hiyo huduma ya wanawake iko kwake, hatupewi, asilimia 10 haifiki! Kwa sababu kinachotakiwa, kweli sisi ni Madiwani kwenye maeneo husika, lakini inapofika kwamba bajeti finyu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja asilimia mia kwa mia. Ahsante sana.