Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote nianze kwa kukupongeza wewe na Mheshimiwa Naibu Spika kwa kuchaguliwa kwa asilimia zote na Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa viongozi wetu katika mhimili huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza Mwenyekiti wangu wa Kamati kwa uwasilishaji mzuri wa ripoti. Nina mambo mengi ya kuzungumza, lakini nitaomba kwanza nianze na hili moja tu, na sidhani kama muda utanitosha.

Mheshimiwa Spika, ni kwamba mnamo Aprili 6, 2020 CAG aliwasilisha Taarifa ya Ukaguzi wa Fedha za Serikali Kuu kwa Mwaka Unaoishia 30, Juni, 2020. Katika uwasilishaji wake, CAG hapa Bungeni alinitaja kwa jina na nafasi niliyokuwa nashika mpaka kufikia mwaka 2020, Desemba - nafasi ya Waziri wa Maliasili na Utalii, akinihusisha na hatua mbalimbali za upungufu wa kiutendaji uliotokea kwenye Wizara niliyokuwa naisimamia.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, CAG alisema mimi nikiwa kiongozi pale, na alinitaja kwa jina; na leo nimejiridhisha kwa kupitia ripoti hizo, kwamba niliidhinisha matumizi ya Tamasha la Urithi (Urithi Festival) shilingi bilioni 2.085 na haikuwa kweli. Hata leo ukienda kutazama kwenye vitabu utaona siyo sahihi, kwa sababu kwanza wakati tamasha hili linaandaliwa na hata linafanyika, mimi nilikuwa nimelazwa hospitali kufuatia ajali niliyoipata tarehe 4, Agosti, 2018 na tamasha lilifanyika mwezi mmoja baada ya hapo, mimi nikiwa nimelazwa Muhimbili. Akasema mimi niliidhinisha wapewe Clouds Media, wapewe TBC, wapewe Wasafi, pesa za kufikia kiwango cha zaidi ya shilingi bilioni mbili, taarifa ambayo haikuwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo, CAG alitamka hapa Bungeni wakati akiwasilisha kwamba mimi nilifanya safari binafsi kupanda Mlima Kilimanjaro mnamo Septemba, 2019 na safari ile ilitumia pesa za TANAPA na NCAA kwa kufuata maelekezo yangu, jambo ambalo pia halikuwa kweli, kwa sababu safari hiyo ilikuwa ipo katika mpango wa marketing wa Wizara na mambo yote haya yalikuwa yako katika Mpango wa Tanzania Unforgettable ambao ulikuwa unatekelezwa na Wizara…

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, ili twende vizuri kwenye huu mjadala wa taarifa zetu hizi mbili za Kamati, maana nilikuwa najaribu kufuatilia, maana hivi vitabu ninavyo hapa na kwenye kompyuta. Hii taarifa unayoizungumzia, ipo kwenye ipi kati ya hizi taarifa mbili? (Makofi)

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya kurahisisha rejea yako, unaweza ukapitia Ripoti ya Mwaka ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu ukaguzi…

SPIKA: Sasa ngoja. Leo tunajadili taarifa za Kamati za Bunge mbili ili zituongoze kwenye Bunge letu kufanya maamuzi fulani ambayo tutayapeleka kama maazimio ya Bunge kwa Serikali ili wayafanyie kazi.

Sasa nataka kuelewa vizuri, ili tuelewane tunaendaje na huu mjadala? Maana naona ulipoanzia mwanzoni na hapa ulipofika sasa, ni “taarifa ile siyo kweli, taarifa ile siyo kweli na taarifa ile siyo kweli,” mpaka hapa nilipokusikiliza. Sasa sijajua muda wako wa kuchangia umeamua kutumia nafasi yako kukanusha taarifa ile au umeamua kutumia muda wako kuchangia kwenye hoja hizi zilizo mbele yetu, ili Bunge baadaye liamue kwamba linaielekeza nini Serikali cha kufanya? Hicho ndicho ninachotaka kuelewa ili Kanuni zetu zituongoze vizuri tunakotaka kwenda.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, sawa. Nashukuru na bila shaka unanitunzia muda wangu, maana yake nina dakika tano tu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naorodhesha hii mifano kwa sababu Kamati ya PAC imechambua taarifa zinazoishia Juni, 2020. Kwenye taarifa hiyo ambayo inaishia Juni, 2020 ndimo mimi nilitajwa, lakini katika proceeds za kazi za Kamati, hayo madai ya CAG hayaingii kwenye hii ripoti kwa sababu waliyatupilia mbali kwa kuwa yalikuwa ni ya uongo.

SPIKA: Sawa. Nimekuelewa vizuri Mheshimiwa.

Waheshimiwa Wabunge, nadhani maelezo ya Mheshimiwa Dkt. Dkt. Kigwangalla sote tumeyasikia hapa na mimi nimeyasikia. Nafikiri zitumike njia sahihi zinazotakiwa kukanusha Taarifa ya CAG. Kwa sababu sisi hapa ndani tunafahamu Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali inapoletwa hapa ndani tunaipeleka kwenye Kamati ikafanyiwe kazi. Sasa ikiwa ile taarifa inazo taarifa ambazo siyo za kweli, basi lazima tutumie njia iliyo sahihi.

Kwa sababu mimi niliyekaa hapa mbele mkiniweka katika mazingira kwamba niishike ile taarifa nianze kusema nani ni mkweli na nani siyo mkweli, ili niseme Taarifa ya CAG siyo kweli ama ni kweli, lazima zote mbili niwe nazo na niwe na vielelezo. Kwa sababu hapa, yaani Bunge lina Taarifa moja tu ya CAG.

Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, taarifa ya kukanusha uko huru kabisa kuileta kwa Spika kwa maandishi ili ifanyiwe kazi kwa utaratibu mzuri. Ukisema hapa ndani utalielekeza Bunge kuliambia kwamba kipengele hiki cha Taarifa ya CAG siyo kweli kwa sababu wewe umesimama kutoa maelezo hapa, utakuwa unaniweka mimi katika mazingira ambayo; sijaiona mimi taarifa yako ambayo inakanusha zaidi ya maelezo unayoyatoa sasa.

Kwa kuwa taarifa niliyonayo mimi ni ile ya CAG, basi nakuruhusu ulete maelezo yako ya kukanusha ile taarifa ili ifanyiwe kazi kwa utaratibu ulio wa kawaida. Sote tunafahamu Kanuni zetu haziruhusu Mbunge kuchafuliwa na mtu yeyote wala mtu mwingine yeyote kuchafuliwa na Mbunge.

Kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge hujatendewa haki na ile taarifa, wewe ulete malalamiko yako kwa njia ya kawaida kabisa na yatafanyiwa kazi na Bunge hili. Wala usiwe na wasiwasi, unalindwa kabisa. Ila kutumia muda huu wa kuzijadili hizi taarifa za Kamati hapo ndipo ambapo wewe sasa utakuwa unazikosea taratibu zetu za Bunge.

Kwa hiyo, ama uchangie kwenye hizi au kama ni hayo yako ya kuilalamikia ile taarifa na kueleza namna ambavyo siyo sahihi, utumie njia za kawaida ambazo unaruhusiwa kabisa Kikanuni. Kama ni hayo tu ulikuwa nayo, niite mtu mwingine, halafu wewe kama nilivyotoa maelezo, una nafasi ya kumletea Spika malalamiko yako ili yafanyiwe kazi.

Haya, ahsante sana. Waheshimiwa Wabunge, ameonesha ishara ya kuonesha kwamba pengine atachukua hizo hatua nyingine, lakini kwa sasa hana mchango mwingine zaidi ya huo aliokuwa anazungumza kuhusu yeye na ofisi ambayo aliwahi kuihudumia.