Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili niweze kujibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, nakuomba uje mbele hapa.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pili, napenda kutumia nafasi hii kwa heshima na taadhima ya hali ya juu kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuniamini na kunipa nafasi ya kuwatumikia wananchi wa Tanzania katika Sekta ya Afya na Maendeleo ya Jamii kama Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kusimama kidete kuhakikisha ndoto za wananchi wa Tanzania za kupata maendeleo endelevu zinafikiwa. Vilevile namshukuru kwa namna ya kipekee bosi wangu Madam Boss Lady Waziri wa Afya na Binamu yangu Mheshimiwa Ummy Ally Mwalimu kwa kunipa ushirikiano wa hali ya juu katika jukumu hili nililopewa na Mheshimiwa Rais la kumsaidia kusimamia na kuongoza Wizara hii nyeti nchini kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani za kipekee kwa wananchi wa Jimbo langu la Nzega Vijijini kwa kuniwezesha kufika hapa nilipo. Pia namshukuru sana Mke wangu mpenzi Dkt. Bayoum na watoto wetu Sheila, Hawa na HK Junior, nafahamu Mama Sheila uko hapa kunipa support. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nakushukuru wewe mwenyewe kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge hili, lakini pia kwa namna ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa uongozi madhubuti mnaotoa na ushirikiano mnaotupa katika kutekeleza majukumu yetu hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii na Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano wanaonipatia katika kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza watumishi wote wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakiongozwa na Katibu Mkuu Idara Kuu ya Afya, Dkt. Mpoki Ulisubisya na Katibu Mkuu Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii, Mama Sihaba Nkinga na wafanyakazi wote wa Sekta za Afya na Maendeleo ya Jamii kwa kazi yao nzuri wanayofanya na naomba tuendelee kufanya kazi kwa uadilifu, uaminifu na uhodari wa hali ya juu ili tuweze kufikia malengo, tusimwangushe Mheshimiwa Rais pamoja na Wabunge wenzetu, Madiwani na wananchi wote wanaotutegemea sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa maandishi na kwa kusema hapa Bungeni, kwa hakika michango yao inalenga kuboresha huduma za afya na maendeleo ya jamii nchini.
Kama mlivyoona Waheshimiwa Wabunge hoja zilizotolewa ni nyingi sana, lakini muda tuliopewa hautoshi kujibu hoja zote, nafahamu Mheshimiwa Waziri atajibu kwa mapana na marefu, lakini nami nimeona nichangie kwenye hoja hii angalau kwa kutoa ufafanuzi kwenye maeneo machache kama ifuatavyo na majibu ya kina ya hoja zote ambazo zimetolewa hapa yatawasilishwa Bungeni kwa Waheshimiwa Wabunge kwa maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja kuu ambayo imejitokeza hapa ni hoja ya namna ya ku-finance mfumo mzima wa afya. Kuna namna nyingi ambazo nchi mbalimbali duniani zinagharamia mifumo yake ya kutoa huduma za afya kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mfumo wa kutumia kodi, kuna mfumo wa kutumia pesa za wanaotaka huduma kulipia huduma hizo hospitalini kuna mifumo ya kulipia huduma kabla hujatumia. Hapa nazungumzia mifumo ya Bima ya Afya, mifumo ya kuchangia namna hiyo na Tanzania kwa kiasi kikubwa mfumo wetu unategemea zaidi pesa kutokana na kodi. Tuna asilimia takribani 25 ya watu ambao wanachangia kwa pesa kutoka mifukoni mwao pale ambapo wanahitaji kupata huduma za afya kwenye vituo vya kutolea huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiasi kidogo sana, kuna asilimia takribani 27 ya Watanzania ambayo inafaidika kwa mifumo mbalimbali ya Bima ya Afya iliyopo katika nchi yetu. Suala hili limejitokeza kwenye michango ya Mheshimiwa Seif K. Gulamali, Mheshimiwa Zitto Kabwe, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi (Sugu), Mheshimiwa Ester Bulaya, Mheshimiwa Lazaro Nyalandu, Mheshimiwa Taska R. Mbogo na Mheshimiwa Halima A. Bulembo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine ni Mheshimiwa Dua William Nkurua, Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mheshimiwa Godfrey W. Mgimwa, Mheshimiwa Agnes M. Marwa, Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mheshimiwa Zuberi M. Kuchauka, Mheshimiwa Allan J. Kiula, Mheshimiwa Amina S. Mollel, Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mheshimiwa Hamidu H. Bobali, Mheshimiwa Ahmed M. Shabiby, Mheshimiwa Susan L. Kiwanga na wengine watanisamehe kama sikuwataja majina yao hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiasi kikubwa wengi wamechangia suala la Bima ya Afya ama kwa namna moja ama nyingine gharama za huduma za afya nchini. Jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hususan ya Awamu ya Tano, ambayo inatafsiri Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, chama ambacho kimeshinda uchaguzi wa mwaka 2015 inasema kwamba: “Kufikia mwaka 2020 tutakuwa tumetoa bima ya afya kwa Watanzania wote na bima hiyo ya afya itakuwa ni ya lazima.” Sasa kuitafsiri Ilani ya Uchaguzi, sisi tuliopewa dhamana ya kutoa uongozi kwenye sekta hii, tayari tumeanza kufanyia kazi azma hiyo ambayo inaelekezwa na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua tulizochukua mpaka leo na Waheshimiwa Wabunge ni kwamba tuna mikakati ya aina mbili, kwanza tuna mkakati wa muda mrefu na mkakati huu ni wa kuelekea kuwa na mfumo mmoja wa bima ya afya nchini, mfumo ambao utakuwa ni wa lazima, mfumo ambao utataka kila Mtanzania awe na aina mojawapo ya kuchangia huduma kabla ya kutumia yaani mifumo kama ya Bima ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu ili hili lifanikiwe, ni lazima tuunganishe Mifuko na hili amelisema vizuri Mheshimiwa Zitto Ruyagwa Kabwe, lakini pia Wabunge wengine wamelichangia. Sasa ili kufanikisha hili, tayari tumeanza mchakato wa ndani ya Serikali kwanza kuhakikisha tuna mkakati wa kugharamia huduma za afya yaani National Health Financing Strategy, pia kuhakikisha tunaandaa mapendekezo ya sheria ya Single National Health Insurance ambayo tutaiwasilisha Bungeni ili iweze kupitishwa na Wabunge ianze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato wote huu ukikamilika tunaamini itakuwa imeshapita takribani miaka miwili hadi mitatu ili sheria hiyo iweze kuanza kufanya kazi kama itapita kwenye Bunge hili. Tayari ndani ya Serikali tumeanza mchakato huo, tuna National Health Financing Strategy pia tayari tumeshaanza kuandaa Muswada huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato ndani ya Serikali tayari umekwishaanza na matarajio yetu ni kwamba kwenye Bunge la Septemba kama kila kitu kitaenda sawa, tutaweka mezani kwenye Bunge lako Tukufu, Muswada wa Single Health Insurance mchakato huo utaanza. Hata hivyo, kwa kutambua ucheleweshaji ambao unaweza ukajitokeza ili sheria hii iweze kuanza kufanya kazi wakati sisi tumeweka malengo ndani ya Chama cha Mapinduzi kwamba kufikia Mwaka 2020 takribani asilimia 80 ya Watanzania wawe na Bima ya afya ya aina moja ama nyingine, tumeona tuanze kutekeleza mpango wa haraka na wa muda mfupi wa kufanya maboresho ya lazima kwenye mfuko wa kuchangia huduma za afya wa CHF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuanze kutekeleza hayo kwa sababu hatufanyi mabadiliko yoyote yale ya kisheria, tayari tuna Sheria ya CHF ya mwaka 2001, pia tuna sheria ya National Health Insurance Fund ambazo zinaishi na zinafanya kazi, tutafanya maboresho ya ki-program ya kiutekelezaji hapa na pale ili wananchi waweze kupata huduma bora zaidi za afya haraka zaidi wakati tukijipanga kutekeleza mpango huo ambao utakuja kwenye hiyo Sheria ya Single National health Insurance ambayo itaweka ulazima kwamba kila Mtanzania ni lazima awe na bima ya afya. Mabadiliko ambayo tunayafanya kwenye CHF iliyoboreshwa, siyo mabadiliko ya ajabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu Waheshimiwa Wabunge miongoni mwetu tunaweza tukawa ni beneficiaries wa mabadiliko hayo ambayo yameanza kufanyiwa kazi na taasisi mbalimbali ambazo zinafanya kazi kwa ukaribu na Wizara yetu katika baadhi ya mikoa hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto mbalimbali za kwenye CHF kama vile changamoto ya portability kwa maana ya kuhama na card ya CHF kutoka kwenye ngazi moja ya huduma kwenda kwenye ngazi nyingine itapatiwa ufumbuzi, maana hapa tunazungumzia kwenye maboresho haya mtu akiwa na card ya CHF kutoka kijijini aweze kupata huduma za afya kutoka kwenye ngazi ya zahanati, ngazi ya kituo cha afya, ngazi ya hospitali ya Wilaya mpaka kufikia ngazi ya hospitali ya Rufaa ya Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa niseme, tayari kwenye yale malalamiko ya D by D sitalieleza kwa upana sana hilo Mheshimiwa Waziri alifafanua. Tayari tumeanza mchakato wa ndani ya Serikali kutafuta namna ya kuzichukua hospitali za mikoa na kuziweka chini ya Wizara ya Afya, ili mfumo wa rufaa uwe chini ya Wizara ya Afya lakini mfumo wa afya ya msingi ubaki chini ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna mantiki kubwa sana. Chini ya TAMISEMI kuna uwakilishi wa wananchi na uwakilishi huo wa wananchi ni lazima. Hatuwezi kuwa na haki na usawa kwenye nchi kama wananchi hawashirikishwi kwenye kufanya maamuzi mbalimbali. Huu ndiyo msingi wa falsafa ya D by D, ugatuaji wa madaraka maana yake tunashusha nguvu za kufanya maamuzi kwenye mikono ya wananchi kwenye Halmashauri zetu, kwenye Kata, Kwenye Vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi ku-defeat the whole purpose ya kuwa na D by D kwa kutaka kufanya mabadiliko tu makubwa ya kiutendaji kwenye mfumo wa afya, lakini kwenye hospitali za mikoa uwakilishi wa wananchi haupo ndiyo maana tumesema hizi tunaweza tukazihamisha kutoka TAMISEMI tukazipeleka chini ya Wizara ya Afya na mfumo wa rufaa kwa ujumla wake ukawa chini ya Wizara ya Afya na ukafanya kazi vizuri zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye maboresho ya CHF tutaweza kumpatia huduma Mtanzania kutoka ngazi ya Zahanati mpaka ngazi ya hospitali ya Rufaa ya Mkoa. Tayari mchakato huu umekamilika na card zitakuwa ni za kielektroniki, tunasubiri mchakato ndani Serikali wa kufanya maamuzi ukamilike tuweze ku-launch mradi huu mkubwa wa maboresho ya CHF.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Susan Lyimo alizungumzia kwamba mimi ni Balozi wa Wanawake kwa nini sikukemea kauli iliyotolewa humu ndani? Naomba nimhakikishie tu kwamba Ubalozi wangu uko pale pale na dhamira yangu ni safi. Yaliyotokea ndani ya Bunge kwa bahati mbaya sana yalitokea wakati sipo, lakini tayari utaratibu wa Kibunge ulishalifanyia kazi suala hilo na hivyo siwezi kuliingilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kupandisha hadhi vituo. Waheshimiwa Wabunge wote ambao mna vituo mnataka vipandishwe hadhi, andikeni barua kwa Waziri wa Afya na kesho mnikabidhi, nita-assign Idara Maalum ya Ukaguzi iliyoko chini ya Wizara yetu ipite kwenye Majimbo yenu ikague hospitali, zahanati na vituo vya afya vyote na kisha imshauri Mheshimiwa Waziri wa Afya kama kweli kuna haja ya kuvipandisha hadhi ama la. Naomba mtekeleze hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu taasisi ya Saratani ya Ocean Road, tuna mpango kabambe wa kufanya maboresho makubwa kwenye taasisi hii, hili ni jambo ambalo limewagusa Waheshimiwa Wabunge wengi hata sisi linatugusa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kwa mara ya kwanza Mheshimiwa Waziri wa Afya alipotembelea hospitali ya Ocean Road alitoa machozi jinsi alivyokuta wagonjwa wale wanapata madhila makubwa kwenye huduma za afya. Tayari tumejipanga kununua mashine mpya ya LINAC ambayo tutaifunga kwenye jengo jipya ambalo amelizungumzia Mheshimiwa Rashid Ally Abdallah. Hata hivyo, pia tumetenga bilioni saba kwa ajili ya dawa, kwa hivyo yale matatizo ya chemotherapy aliyokuwa anayazungumzia kwenye mwaka wa fedha unaokuja yatakuwa yamepatiwa ufumbuzi wa uhakika.
Mheshimiwa Susan Mgonokulima alizungumzia kuhusu viroba, namwagiza hapa Mkurugenzi Mkuu wa TFDA aende akafanye uchunguzi wa kitaalam wa kemikali na kiwango cha alcohol kilichomo kwenye viroba kwenye viwanda mbalimbali vya viroba nchini na aniletee taarifa ndani ya siku 14. Mheshimiwa Mwakibete na Mheshimiwa Joseph Mbilinyi (Sugu) CT- Scan kwa ajili ya hospitali ya Rufaa ya Mbeya, tayari tumeshatoa maelekezo nilipokuwa nimefanya ziara pale Mbeya Rufaa takribani miezi miwili iliyopita ili muweze kupatiwa CT Scan machine.