Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni ya leo. Kwanza nampongeza kabisa kwa dhati Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni katika Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Wananchi la Tanzania limefanya kazi kubwa sana katika Jamhuri ya Muungano na nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tunaposema hapa kwamba jeshi lisitumike kisiasa, hatuna maana kwamba sisi sio wazalendo, tunalipenda jeshi letu lakini tunaonya kwamba vitendo vinavyofanyika Zanzibar na vilivyofanyika wakati wa uchaguzi na sasa vinaashiria uvunjifu wa amani na ukiukwaji wa haki za binadamu. Hiyo haina maana kwamba watu hawa siyo wazalendo au hawalipendi jeshi hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Wananchi wa Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizotoa askari kulinda amani katika Jeshi la Umoja wa Mataifa. Ripoti iliyowasilishwa tarehe 3 Machi inazungumzia matukio 99 ya ubakaji na udhalilishaji wa watoto yaliyofanyika mwaka 2005 na walinzi wa amani Umoja wa Mataifa katika nchi 69. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 6 Machi, 2016, kwa mujibu wa vyombo vya habari vilimnukuu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi akisema kwamba ripoti ya Umoja wa Mataifa juu ya yaliyotokea katika Afrika ya Kati na maeneo mengine, hajaipata. Leo ni tarehe 10 Mei, takribani miezi miwili tokea Waziri alipowaambia umma kwamba ripoti ile hajaipata. Tunaomba Mheshimiwa Waziri wakati anapojibu alieleze Bunge hili Tukufu, ni hatua gani zimechukuliwa kama askari wetu wa Jeshi la Ulinzi na Usalama walihusika na mambo yaliyotokea katika Jeshi la Kulinda Amani?
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni muhimu sana kwa kuwa jeshi letu limefanya kazi nzuri, linaheshimika duniani, ili lisiweze kuchafuliwa kwa mambo ambayo hayawahusu. Jambo hili ni muhimu pia likawekwa wazi kwa kuwa taarifa hizi zilitolewa hadharani na ziko katika mitandao na zipo katika Ofisi za Umoja wa Mataifa Jijini Dar es Salaam. (Makofi)
Jambo la pili, kuna taarifa kwamba Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania limeingia mkataba wa ujenzi wa nyumba kwa ajili ya makazi na Kampuni ya Henan Guijo Industry Investment Co. Ltd. Katika mkataba huo, Jeshi la Wananchi wa Tanzania litatoa ekari za mraba 26,082.87 katika eneo la plot number 1255 Masaki, Jijini Dar es Salaam. Katika mkataba huu mjenzi akikamilisha mradi kwa mujibu wa taarifa zilizopo, ataendesha eneo hili kwa muda wa miaka 40 na baada ya hapo eneo litarudi jeshini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri atueleze kama mkataba huo umesainiwa; na kama haujasainiwa nitaliomba Bunge hili Tukufu lielekeze kwamba mkataba huu ambao unaweza ukawa wa kinyonyaji upelekwe katika Kamati ya Ulinzi na Usalama ili uweze kupitiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi letu limewahi kuingia mikataba ya aina hii na ambayo baadaye ilikuja kuonekana imedhalilisha Jeshi, imedhalilisha Serikali ukiwemo mkataba wa Meremeta. Sasa ni vizuri tukajihadhari, lakini kibaya zaidi, ni kwamba kampuni ya Henan Guijo Industry Co. Ltd. ambayo imeingia mkataba na Jeshi la Wananchi au inataka kuingia mkataba na Jeshi la Wananchi, inajifunga mkataba mwingine na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kampuni hiyo itajenga pia nyumba ya Dkt. Hussein Mwinyi iliyopo plot number 2435/5 eneo la Sea View, Upanga Jijini Dar es Salaam. Kampuni hiyo ndiyo itakayolipia gharama za ujenzi...
TAARIFA
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.....
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema mita za mraba, labda hakusikia vizuri. Naomba pia unilinde kwenye muda wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mkataba huu, kama ambavyo unaweza kuwa ama umesainiwa ama haujasainiwa, ni kwamba mjenzi ndiye ambaye atajenga pia nyumba ya Dkt. Mwinyi. Sasa kama madai haya ni ya kweli, tunaomba Mheshimiwa Waziri atuambie huu siyo mgongano wa kimaslahi? Je, kwa mkataba huo, haina maana kwamba jeshi letu linaingizwa kwenye mkataba wa kinyonyaji kwa kuwa Waziri ananufaika? (Makofi)
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema kwamba uchunguzi ufanyike na vyombo vinavyohusika, vimchunguze Mheshimiwa Waziri na vipeleke taarifa kwenye Bunge hili Tukufu kwa kuwa uchunguzi huu ni muhimu kwa sababu unahusu hoja muhimu kabisa iliyopo mbele ya Bunge lako Tukufu.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kumalizia hoja yangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi letu la Wananchi tunalipenda sana, Taifa letu tunalipenda sana, Bunge letu Tukufu tunalipenda sana, lakini mambo ya namna hii yanatia doa Jeshi letu na Taifa letu. Kuna mambo yanazungumzwa mengi sana kwenye Taifa hili. Baadhi ya kampuni ambazo zinatuhumiwa katika maeneo mengine kwamba zimefanya biashara na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama likiwemo Jeshi la Polisi nazo pia zinatajwa kufanya biashara na Jeshi la Wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Kampuni ya Lugumi, baadhi ya nyaraka mbalimbali zinaonyesha kwamba Kampuni ya Lugumi iliwahi pia kufanya biashara na Jeshi la Wananchi na iliwahi kuuza silaha kutoka Taiwan lakini Jeshi letu lilizikataa kwa kuwa zilikuwa chini ya kiwango. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri sana kwamba…
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri jeshi letu likajiepusha na makampuni kama haya. Kwa nini vitu hivi vinajirudia mara kwa mara? Tunalipongeza sana kwa kazi nzuri ambayo Jeshi limefanya katika Taifa hili, limefanya kazi kiuadilifu, kiuaminifu na kwa kweli mambo mengi limepakaziwa. Jeshi linashinikizwa kufanya mambo kwa sababu za kisiasa. Mikataba mingi ambayo Jeshi hili limeingia ikiwemo Meremeta ni kwa sababu za kisiasa. Mambo mengi ambayo yanatokea Zanzibar, yamefanyika kwa mashinikizo ya kisiasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema haya, tunataka jeshi letu liondoke huko, likafanye kazi ya kulinda amani katika Taifa letu na kufanya kazi ya kulinda mipaka yetu. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kubenea muda wako umekwisha.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, siungi mkono hoja.