Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Mama Samia kwa kazi nzuri inayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha huu tunaoutekeleza fedha nyingi sana zimeletwa katika majimbo yetu na mimi katika Jimbo la Meatu tumeshapokea wastani wa shilingi bilioni 10 katika miradi mbalimbali, elimu, afya, maji, barabara na miradi mingine mbalimbali ikiwemo mifugo pamoja na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu wake mkubwa kwa Wabunge wenzake. Ni kipindi kirefu nimekuwa nikifuatilia kutekelezwa kwa ahadi aliyoitoa Mheshimiwa Samia Suluhu wakati akiomba kura, akiwa mgombea mwenza mwaka 2015, Meatu, aliahidi kujengwa kwa daraja la Mto Semu katika Kijiji cha Mwamanongu, lakini muda mfupi tu alipoingia nilivyomueleza jambo hili nishukuru tayari juzi tumeshapokea shilingi bilioni 43 kwa ajili ya kufanya usanifu wa daraja hilo, lakini nimshukuru pia Engineer Seif kwa ushirikiano wake mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe tu tusiishie katika usanifu kila tunapouliza maswali tuambiwe usanifu unaendelea. Kwa kuwa sisi Wilaya ya Meatu katika Mfuko wa TARURA tumetenga shilingi bilioni 2.7 katika miradi ya maendeleo kwa ajili ya kuanza ujenzi wa daraja hilo la Mto Semu katika Kijiji cha Mwamanongu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niiombe Serikali mwaka jana mwezi wa tisa iliniahidi kupanua shule ya Sekondari Nghoboko. Naomba wafanye utekelezaji huo kwa sababu, tulijipanga toka mwaka 2008 kupandisha hadhi shule ya Sekondari Nghoboko kuwa ya kidato cha tano na sita kwa sababu, tayari madarasa manne tumekamilisha, ofisi tatu, bwalo linahitaji kupauliwa, tunaomba bweni pamoja na maktaba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu leo kwa kiwango kikubwa nitajikita katika mapato. Tumeona Mheshimiwa Waziri amesema kutakuwa na ongezeko la asilimia 17.1 katika mapato ya Halmashauri ni jambo jema, lakini katika mapato ya Halmashauri yamekuwa na changamoto nyingi katika ukusanyaji wake ikiwemo mapato mengi ya Halmashauri yanakusanywa nje ya mfumo rasmi wa Halmashauri kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilianza ikatoa property tax ambayo ilipaswa ikusanywe na Serikali za Mitaa. Tumeona wameondoa parking fees, wametoa tozo za maji ambazo zote zilipaswa kukusanywa na Serikali za Mitaa na sasa kwa asilimia kubwa ushuru wa huduma unakusanywa na TRA. Mapato haya yalitakiwa yalindwe yakusanywe na Serikali za Mitaa kwa sababu zina mahitaji mengi na ni makubwa. Tumekuwa tunaziongezea mapato, lakini mapato yake yamekuwa yakipungua kila mwaka kwa kadri tunavyokwenda. Naomba hili suala liangaliwe kwa kina, Halmashauri zetu zinakuwa hazistawi katika mapato wakati kazi zake ni nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na katika taarifa iliyopita ya Julai/Disemba kwa mwaka wa fedha uliopita ushuru wa huduma ulionekana kuongoza kuwa chanzo chake kikubwa kwa sababu asilimia 19 ilikuwa imekusanywa ya mapato yote, lakini chanzo hiki kika changamoto nyingi. Mwanzo kazi za kandarasi zilikuwa zikilipwa Halmashauri, ushuru wa huduma ulikuwa ukibakia Halmashauri, lakini certificates sasa zinalipwa Hazina za miradi ya maji, miradi ya barabara, kwa hiyo, ushuru wa huduma umeendelea kukusanywa na TRA.

Niombe namna Serikali inavyoweza kurudisha katika Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na kuweza kuzirudishia Halmashauri ziweze kujitegemea kwa mapato kwa sababu Halmashauri zimeendelea kutegemea Serikali kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna miradi mikubwa pia kimkakati ambayo haikusanywi vizuri. Kwa mfano tulivyofanya ziara Kamati ya Bajeti, SGR hawajaanza kukusanya ushuru wa huduma, basi miradi kama hiyo ikibaki hata Serikali Kuu ikakusanywa irudishwe katika Serikali Kuu iweze kuzisaidia Halmashauri kwa sababu, tunaona watendaji wetu wa kata hawana ofisi, baada ya mradi ule wa undelezaji mtaji kusitishwa, kwa hiyo, yamebakia maboma. Warudishiwe basi zile fedha watendaji wetu wapate ofisi, wapate hata vitendea kazi kama pikipiki, waweze kusimamia vizuri ukusanyaji wa mapato kama ushuru wa mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo cha pili kulichoonekana ni kikubwa ni ushuru wa mazao, lakini ushuru huu umekuwa na changamoto nyingi katika ukusanyaji wake. Nishukuru Wizara ya Kilimo kwa kuamua kuwapatia pikipiki Maafisa Ugani waweze kusimamia uzalishaji wa mazao, lakini wameenda zaidi wakawawezesha kwa posho, jambo ambalo litasaidia uzalishaji wa mazao ambayo yanachangia kupata ushuru wa mazao tofauti na mwanzo mafaili yalikuwa yakibaki pale kwa Wakurugenzi mpaka msimu unakwisha hawajawaona wakulima wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe na sisi TAMISEMI tuige jambo lililofanywa na Wizara ya Kilimo kwa kuwawezesha watendaji wetu wa kata. Watendaji wa Kata ndiyo asilimia kubwa wanasimamia ukusanyaji wa ushuru wa mazao, lakini hawana pikipiki, hawalipwi posho, tumepewa shilingi 100,000; lakini shilingi 100,000 hii wakati mwingine inapita miezi miwili haijalipwa. Basi tuone namna inavyoweza kulipwa na Serikali kuu kwa sababu wenyewe hawawezi kumshinikiza Mkurugenzi kwa sababu ni mwajiri wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia ushuru huu wa mazao kumekuwa na uvujaji wa mapato kwa sababu katika hoja za ukaguzi tumeona fedha zimetumika zikiwa mbichi na moja ya sababu inayochangia kwa kuwa hawalipwi fedha za ukusanyaji wakati mwingine wanajilipa kabla zile fedha hazijafika Halmashauri. Kwa hiyo, tukiwawezesha mianya hii ya uvujaji haitakuwepo kwa sababu fedha inayotumiwa kabla haijafika Halmashauri haiwezi kutambulika katika vitabu vya Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namba tatu katika ukubwa wa mapato ya Halmashauri ni uchangiaji wa huduma ya afya, tumeona wananchi wamekuwa na mwitikio, lakini wananchi wamekuwa wakishindwa kuchangia kikamilifu, tukisimamia vizuri uchangiaji mapato yatakuwa zaidi kuliko mlivyoyategemea 13%. Yapo matatizo kwa sababu kuna upotevu mkubwa wa madawa, lakini Serikali tumekuwa tukiangalia tu upotevu wa dawa lakini pia kuna fedha ambazo hazilipwi na bima ya afya kwa sababu ya ujazwaji mbaya wa fomu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka miwili mfululizo Halmashauri zimepoteza bilioni mbili kwa ujazaji mbaya wa fomu za bima ya afya. Niiombe Serikali iwasaidie weledi katika ujazaji wa fomu watumishi wetu ili yale mapato yasiendelee kupotea, yale mapato yakiendelea kuwepo yatasaidia kuwa-revolving katika Halmashauri zetu wananchi wakienda hawatakosa dawa, wataendelea kujiunga na bima ya afya tutaisaidia Serikali siku ambapo itashindwa kupeleka fedha sisi tayari tutakuwa na fedha za revolving ambazo zitasaidia kuendeleza upatikanaji wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika service levy pia kuna mapato mengi ambayo hayakusanywi kutokana na kwamba tu ofisi za makampuni haziko Halmashauri ambapo wametekeleza miradi hiyo. Lakini pia kuna halmashauri zinakusanya ushuru huo bila kujua ni faida kiasi gani kilipatikana katika yale makampuni ni kwa sababu hazina access ya kupata turnover ya ile kampuni husika. Niiombe Serikali kupitia TRA na mwenyekiti wa mapato wa mkoa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwosha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya malizia sekunde mbili.

MHE. LEAH K. KOMANYA: Azisaidie Halmashauri kupata takwimu cha kiasi ambacho Halmashauri zinatakiwa kutozwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)