Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipa na kwa sababu ya changamoto ya muda pia mchango wangu nitaupeleka kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, kwa dakika hizi chache nilizozipata niseme kwamba tuko leo kujadili makadirio ya mapato na matumizi ya sekta muhimu sana ya Wizara nyeti ya Katiba na Sheria ambako tunaenda kuwahakikishia wananchi wetu kwamba haki itaendelea kutolewa pia haki itaendelea kupatikana kwa wakati na rasilimali zao za umma zitaendelea kulindwa.

Mheshimiwa Spika, bado tuna changamoto nyingi sana kufikia haki hizi kutolewa sawasawa.

Moja, kuna baadhi ya Watendaji wa Serikali ambao wanavunja Katiba na wanavunja na Sheria wakati wa kutekeleza majukumu yao.

Pili, bado kumekuwepo na usiri mkubwa sana kwa mikataba inayoingiwa na Serikali kwa niaba ya wananchi.

Tatu, bado kuna ucheleweshaji mkubwa wa maamuzi ya Mahakama na taasisi zingine ambazo zimepewa jukumu la kutoa haki.

Nne, maeneo mengi muhimu ya kiuchumi na kijamii hayajatungiwa sheria na hivyo kutumia matamko ya Viongozi katika kutoa uelekeo wa nini kifanyike katika eneo husika.

Tano, ni upendeleo na kukosekana kwa uwiano wa utoaji wa adhabu zinazotolewa katika baadhi maeneo ya kisheria.

Mheshimiwa Spika, haya yasipofanyiwa tathmini vizuri tutaendelea kupiga mark time kwa sababu yana madhara makubwa sana katika uchumi wetu tunaousimamia. Tunasema tu kirahisi kwamba Mahakama imechelewesha maamuzi au Taasisi iliyopewa dhamana ya kutoa haki imechelewesha maamuzi, lakini madhara yake ya maamuzi hayo kwenye Taifa ni yapi, madhara hayo ya kuchelewa kwa maamuzi kwa mtu aliyetakiwa kuipata hiyo haki ni yapi.

Mheshimiwa Spika, tunasema tu kiurahisi kwamba mikataba inaingiwa kwa usiri na inatunzwa kwa usiri, lakini madhara ya kutunza mikataba kwa usiri kama Taifa ni ipi. Tunakuwa kwenye changamoto kubwa za namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, niweze tu kutoa mfano wa madhara makubwa sana ambayo tunayapata kutokana na ucheleweshaji wa maamuzi wa kesi katika Mahakama. Hapa tunakumbuka kwamba tulikuwa na tatizo la pingamizi za kikodi la Shilingi Trilioni 360, hili jambo lililalamikiwa na Bunge hili, hili jambo lililalamikiwa na mimi mwenyewe binafsi hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, kwa taarifa ya CAG ya mwaka 2020/2021 inasema kwamba Mahakama hizi zimehitimisha haya mashauri na katika hitimisho Trilioni 5.65 jumla ya kesi 54 zenye thamani ya Shilingi Trilioni 5.65 zimeamuliwa na Mahakama, Serikali pamoja na wadau wa makampuni ya madini wamekabidhiwa kwenda kufanya mjadala wa namna ya kuhitimisha hili suala. Kesi zenye thamani ya Shilingi Trilioni 343.5 zenyewe zimerudishwa TRA kwa majadiliano, na kesi zenye thamani ya Shilingi Trilioni 5.19 zenyewe bado zinaendelea katika Bodi na Baraza la Rufani za Kodi.

Mheshimiwa Spika, kwa taarifa zilizopo hivi sasa ni kwamba tayari Serikali imehitimisha mjadala huu na imekubaliana kupokea Dola za Kimarekani Milioni 300 ambayo badala yake ukibadilisha nadhani ni kama Bilioni 692.61.

Mheshimiwa Spika, hiki kidogo kilichopatikana ni cha kupongeza, nami kabisa nataka nipongeze na Bunge lako hili Tukufu kwa kulisimamia hili jambo, tumeweza kupata hizo Bilioni 692.61 jambo ambalo hapa tuliambiwa hizi fedha ni za mchongo, haya makampuni ya madini madeni ya nyuma hatuwezi kulipwa kwa hiyo tunapoteza muda. Fedha hizi tumezipata leo Bilioni 692.61 ni suala la kujivunia sana.

Mheshimiwa Spika, hapa namkumbuka tingatinga Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alivyosimama kidete kuhakikisha kwamba hizi fedha za Watanzania zinapatikana, watu wakasema haziwezi kupatikana lakini dunia nzima aliiambia na akaihakikishia na leo Taifa limepata Bilioni 692.61.

Mheshimiwa Spika, nakubali kabisa kwamba ndiyo maana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alimteua Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Makamu wa Rais Awamu ya Kwanza na Awamu ya Pili, alimuona uwezo wake na ndiyo maana leo hii amekuja kulisimamia hili kwa kauli yake aliyoisema kazi iendelee.

Mheshimiwa Spika, jambo moja lingine pamoja na mafanikio haya tuliyoyapata lakini suala la kujiuliza hawa wenzetu walioenda kwenye negotiation Mahakama zilisema Trilioni 5.65 zinaweza kupatikana na Serikali iende ikajadiliane walikubalije kupokea Milioni 300 ambayo ni Bilioni 692 tu wakati Mahakama hizi za Bodi ya Rufaa za Kodi, Bodi pamoja na Baraza zilisema kwamba Trilioni 5.65 zinaweza kupatikana kama kodi, kwa nini tupate Bilioni 692.65.

Mheshimiwa Spika, ninaomba eneo hili lina changamoto kubwa na ninashauri na kulishawishi Bunge lako likubali tuunde Tume Teule ya Bunge ikachunguze suala hili, kwanza negotiation timu hiyo ilifikiaje maamuzi ya kupokea Bilioni 692.61, pia ikaangalie uhalali wa majadiliano hayo na kile ambacho kilichopatikana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni hapo ambapo bado ukiondoa sasa hivi kesi za makinikia kwa sababu ni karibu zote zimeondolewa mahakamani. Ukiondoa hizo, bado tunabakiza kesi zenye thamani ya Shilingi Trilioni 5.19 za makosa tu mbalimbali, sasa hivi ukataji wa rufaa kwenye bodi hizi na Mabaraza ya Kodi za Rufaa yamefikia wastani wa Trilioni Mbili kwa mwaka, tukiruhusu hili likaendelea na tukaendelea kuchelewesha hizi kesi? Tutajikuta watu wote watatufungulia kesi au watatukatia rufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kama leo imefikia Trilioni Mbili inakatiwa rufaa Mahakamani na wadau hawa wa kodi, ni lazima tuhakikishe kwamba kesi zinamalizika kwa wakati, sababu za kuchelewesha kesi eti Mabaraza hayana pesa, sababu za kuchelewesha kesi eti kwa sababu mabaraza haya hayana watumishi! Hili ni jambo ambalo haliingii akilini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo unaweza kwenda kukusanya mapato siku hiyo hiyo kesi zikiamuliwa, haki za wale waliokata rufaa zikasikilizwa, pia haki ya Serikali kupata kodi yake na yenyewe ikaweza kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kutokana na changamoto hii ya muda ni usiri mkubwa wa mikataba ambayo Serikali inaingia. Mfano mmoja wa usiri wa mikataba unavyoliathiri Taifa letu ni utekelezaji wa bwawa la Mwalimu Nyerere, utekelezaji wa bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Spika, nizungumze hapa kwa kusema kabisa kwamba maeneo haya ya kimkataba yana changamoto nyingi na ndiyo maana taasisi zetu za kiuchunguzi CAG, PPRA pamoja na PCCB wote wamekuwa wakilalamikia maeneo haya ya kimkataba kuwa na changamoto nyingi sana za ubadhirifu wa fedha za umma, changamoto za wizi wa fedha za umma, changamoto za ufisadi wa fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa Bwawa la Mwalimu Nyerere na mkataba wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, hivi majuzi hapa tumetangaziwa kwamba mkataba huu utamalizika baada ya miaka miwili ijayo, lakini ndani ya mkataba iko clear kwamba kuna Bilioni 260 ambazo ni CSR lakini Mkandarasi akichelewesha mkataba wetu anapaswa kulipa asilimia Kumi. Kwa hiyo, kama amechelewesha Mkandarasi kwa miaka miwili anapaswa kutulipa shilingi trilioni 1.3.

Mheshimiwa Spika, kwa nini haya mambo hayajawekwa wazi katika hili jambo? Tunamdai bilioni 260 za CSR, tunamdai ucheleweshaji wa miaka miwili ambayo ni Trilioni 1.3. Kwa nini haya mambo yana usiri gani? Siri hizo zinawekwa kwa ajili ya kumlinda nani?

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa nafasi.(Makofi)