Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro na Naibu wake Mheshimiwa Godfrey Pinda na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu uwepo wa sheria iliyo kwenye GN. 269 ya Aprili, 2020. Sheria ilitoa kipindi cha mpito cha miaka miwili kuitekeleza na sasa iko kwenye hatua za utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, sheria hii inayokataza uwepo wa maduka ya dawa mita 500 kuzunguka Hospitali za Serikali kwa hisia kwamba baadhi ya wataalamu wa Wizara ya Afya wanaihujumu Serikali kwa kuiba dawa na kuziuza maduka ya karibu au kuwa na maduka karibu na hospitali za Serikali na huishia kuyakuza maduka yao.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu alitoa agizo la kuondolewa kwa maduka yote ya dawa ambayo yapo mita 500 ndani ya eneo la hospitali za Serikali kwa kile kinachodaiwa kuhujumu upatikanaji wa dawa katika hospitali hizo. Tangazo hili lilisababisha taharuki kubwa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mawazo yangu, sheria hii ilipotungwa haikuzingatia maslahi ya wagonjwa wa Kitanzania na wamiliki wa maduka binafsi ya dawa yaliyo karibu na hospitali. Maduka haya yapo kusaidia upatikanaji wa dawa kwani Serikali yenyewe bado haina uwezo wa kusambaza dawa zote na vifaa tiba kwa wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, hii sheria ina mapungufu makubwa sana. Mimi naona hakuna mwananchi anayependa kwenda nje ya hospitali kutafuta dawa au vifaa tiba bali changamoto za uhaba wa madawa na vifaa tiba zilizopo ndani ya hizo hospitali ndio zinafanya waende nje.

Mheshimiwa Spika, madhumuni ya kuanzisha sheria hii yanakinzana kabisa na uhalisia uliopo. Tatizo kubwa lililopo Wizara ya Afya ni katika mfumo mzima wa ugavi, usambazaji na usimamizi wa dawa, na si uwepo wa maduka ya watu binafsi ya dawa karibu na hospitali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, watumishi wasio waaminifu wakiiba na kutoa dawa nje ya hospitali, dawa inaweza kwenda popote nje ya hospitali na hata mikoa ya mbali kwa haraka kwa kutumia mbinu mbalimbali zikiwemo bodaboda.

Mheshimiwa Spika, ninachokiona, si kweli kwamba maduka yaliyo karibu na hospitali ndio wateja wa wizi wa dawa kutoka hospitali za Serikali. Kutokana na ukweli huu napendekeza kwa Waziri wa Katiba na Sheria kwa kushauriana na Waziri wa Afya sheria hii ifutwe kwani kwa kufanya hivyo tutawapunguzia wananchi adha ya kutafuta dawa na vifaa tiba wanazoandikiwa kwenda kununua nje ya hospitali za Serikali; Wizara ya ya Katiba na Sheria itambue kwamba Wizara ya Afya ilitoa vibali mbalimbali vya kuanzisha maduka ya dawa. Kufunga biashara zao kutasababisha hasara kubwa kwa hawa wawekezaji wazalendo na kuikosesha Serikali mapato yatokanayo na kodi wanazolipa; maduka ya watu binafsi ya dawa hasa yale yaliyo karibu na hospitali husaidia upatikanaji wa dawa kirahisi kwani Serikali yetu yenyewe bado haina uwezo wa kutoa dawa zote na vifaa tib ana kufuta hii sheria kutaonesha hawajali wafanyabiashara na wawekezaji wa biashara ya dawa na vifaa tiba hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.