Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kwa mara nyingine kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo anatuongoza hususan katika Wizara hii ya Katiba na Sheria. Namshukuru Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambayo wanawafanyia Watanzania.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee nikushukuru tena wewe kwa namna ambavyo unaliendesha Bunge la Kumi na Mbili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, tumepokea maoni ya kamati mbili; Kamati ya Katiba na Sheria pia Kamati ya Bajeti ikieleza mambo mengi mbalimbali ambayo Wizara tunapaswa kuyatilia maanani ili kuhakikisha kwamba haki siyo tu inatendeka lakini pia inaonekana ikitendeka.

Mheshimiwa Spika, kwa moyo wa dhati kabisa nazishukuru Kamati zote mbili na hasa Wenyeviti wake; Mheshimiwa Dkt. Joseph Kizito Mhagama na Mheshimiwa Sillo, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, kwa maoni yao. Nawaahidi kwamba tumeyapokea na tutakwenda kuyatekeleza.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru pia wanakamati wote wa Kamati zote hizo mbili na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa michango yao kwa Wizara ya Katiba na Sheria siku hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa ufafanuzi kwa baadhi ya hoja chache zilizotolewa. Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imejipanga kumfanya kila Mtanzania aweze kuzielewa sheria, aweze kuzitekeleza na kuzitii ili lile suala la kutokujua sheria isiwe utetezi, liweze kuondoka kabisa. Kwa kufanya hivyo, tumejikita katika kutafsiri sheria kutoka kwenye lugha za Kiingereza kwenda kwenye lugha ya Kiswahili. Mpaka hivi sasa katika sheria 466 tulizonazo katika nchi hii, sheria 212 zimeshatafsiriwa. Kila sheria mpya ambayo inatungwa, itakuja kwa lugha ya Kiswahili ili mwananchi aliyeko Kijijini, aliyeko kule Songea na Mbeya, aweze kuzifahamu sheria hizi, kuzitii na kuzitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maboresho ya Mahakama yameongelewa vizuri sana Mheshimiwa Naibu Waziri, niongeze jambo la muhimu. Pamoja na miundombinu ambayo imewekwa na inaendelea kuwekwa, Mahakama imeleta mfumo wa kuwasiliana na mwananchi wa kawaida, kupitia namba ya simu ambayo ni huduma ya bure, kila mwananchi anaweza akapiga na kutuma meseji bure. Tumeitaja namba hiyo ni 0752 500 400; na mpango huo umepewa jina unaitwa “Sema na Mahakama,” kwa saa 24 ndani ya siku saba katika wiki.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa mtu yoyote anaweza akatumia mfumo huo kutoa kero zake, kutoa hoja zake, hata pale ambapo anahisi kwamba kuna kesi imeendeshwa kinyume cha maadili, kuna viashilia vya rushwa, basi atumie mfumo huo. Tahadhari tu ni kwamba mfumo huo siyo rufani; mfumo huo ni kuelezea kero za kiutawala zilizopo, na wala hutaweza kutangua maamuzi yaliyotolewa kihalali kabisa.

Mheshimiwa Spika, pia kumetolewa hoja na Waheshimiwa Wabunge kuelezea mfumo wa jinai na kwa jinsi gani umekuwa ukichelewesha mashauri za kesi za jinai. Niwaeleze Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote, sasa hivi tuna mkakati wa kuuchukua mfumo mzima wa jinai na kuuingiza maabara ili kuweza kujua changamoto hasa ni nini? Baada ya hapo, tuufanyie mabadiliko makubwa sana mfumo wote wa jinai. Tukifanya hivyo tutaondoa kero za kucheleweshwa kesi.

Mheshimiwa Spika, katika hilo, tunaangalia maeneo matatu; eneo la kwanza, tunaangalia Ofisi ya Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Serikali, wengi hupenda kumwita DPP. Ili tuweze kufanya kazi vizuri, mmesema hapa Waheshimiwa wabunge, lazima tuitendee haki ofisi hiyo. Lazima tuipe vitendea kazi na mambo mengine ili kesi ziweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia tunaangalia Mahakama na Mfumo wa Jinai, wapi kuna vikwazo? Tunaenda kuangalia pia Magereza na mfumo wa jinai tunaamini tukifanya hivi ndani ya mwaka huu wa fedha na kuendelea tutakuwa tumetatua matazo makubwa yanayoikabili mfumo wa jinai.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Neema Lugangira amesimama na kutoa hoja ambazo zinagusa sheria mbili; moja ni sheria ya vyama vya siasa; na ya pili ni sheria ya uchaguzi. Mahususi ameongelea kwa jinsi gani sheria hizi hazimtendei haki mwanamke katika uwanja huu wa siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Neema tumepokea maoni yako kwa uzito mkubwa kabisa. Naomba nichukue fursa hii kuiagiza Tume ya Kurekebisha Sheria kuanzia kesho waanze kuzifanyia kazi sheria hizi mbili; na wawashirikishe wadau wote wakiwemo Waheshimiwa Wabunge wanawake, Waheshimiwa wanasiasa wanawake na wadau wengine ili kujua wapi panawakwaza na tuweze kubadilisha sheria hizi.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Chama cha Mapinduzi kinasema, sheria hizi zinapaswa kuwatumikia watu, na sio watu kuzitumikia sheria hizi. Ni muda sasa wa kuzirekebisha ili kuweza kutenda haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Agnesta ameongelea sana kuhusiana na Tume ya Haki za Binadamu.

Tunapokea maoni yake na tuko tayari kuboresha tume hizo. Niseme tu kitu kimoja, katika bajeti ya mwaka huu, Tume za Haki za Binadamu - Fungu la 55, fedha ambayo inapendekezwa endapo Bunge hili Tukufu litapitisha ni shilingi bilioni 6.5. Hiyo ndiyo fedha ambayo tunapendekeza. Kwa hiyo, Mheshimiwa Agnesta, hebu tupitishie hii ili Tume iweze kupata fedha hiyo. Katika fedha hiyo, fedha za nje ni shilingi milioni 155 tu. Kwa hiyo, tunataka kwenda kubadilisha utendaji wa Tume ili Fungu hili la 55 likaibadilishe Tume, Tume itende haki, pia Tume iwafikie wananchi na kutatua kero zote zinazowagusa.

Mheshimiwa Spika, kwa mara nyingine tena nakushukuru wewe na Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, naafiki.