Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Phillip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Madini, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza Mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Madini, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Taifa letu katika kuboresha maisha ya wananchi na pia utayari wetu wa ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio ya sekta ya madini, Serikali inashauriwa kuchukua hatua za kuimarisha zaidi sekta hii muhimu ili kukabiliana na athari za kiuchumi kutokana Covid-19 na sasa vita vya Urusi na Ukraine. Kutokana na athari ya kiuchumi uliokumba dunia nzima, hii inaweza kuwa fursa kwa Serikali kuvutia uwekezaji zaidi kwenye madini hasa dhahabu, madini ya chuma na madini ya calcium carbonate, limestone na phosphate. Dhahabu ina historia ya bei kutoyumba kwenye soko la dunia kwa vile mabenki yanatumia dhahabu kwenye kuwekeza na kutokana pia na kuyumba kwa thamani ya shilingi na hata dola ya Marekani, Serikali inaweza kutumia dhahabu kama mbadala wa kuwekeza amana zake.

Mheshimiwa Spika, vita vya Urusi na Ukraine vimesabisha upungufu mkubwa wa uzalishaji wa mbolea na hii ni fursa kwa Serikali kuwekeza kwenye viwanda vya mbolea kwa kutumia malighafi zinazopatikana hapa nchini kama vile phosphates, calcium carbonate, limestone na natural gas. Katika kipindi cha mtikisiko wa uchumi, bei ya madini ya chuma na hata makaa ya mawe haiyumbi na Serikali inaweza kupata mapato mengi katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali kuchukua hatua za makusudi na kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa chuma (Liganga Iron Ore) ikiwa ni pamoja na makaa ya mawe (the Mchuchuma coal mining and power projects). Mradi wa Liganga na Mchuchuma ulitarajia uwekezaji wa dola za Kimarekani bilioni tatu na kuzalisha ajira zaidi ya 30,000 na hii inaweza kuwa fursa nzuri katika hiki kipindi cha balaa la athari za Covid-19 na vita vya Urusi na Ukraine.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mradi wa Liganga na Mchuchuma, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya NIOBIUM ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja na reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa Kimataifa. Kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapa kwetu.

Mheshimiwa Spika, Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya NIOBIUM ambayo inapatikana milima ya Pandahill Wilaya ya Mbeya na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) ni makubwa duniani na hapa kwetu pia.

Mheshimiwa Spika, Serikali inahitaji kujiwekekea mikakati ya haraka (quick wins) ili kuhakikisha inakabiliana na athari za kiuchumi kutokana Covid-19 na sasa vita vya Urusi na Ukraine. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini, Serikali inaweza kutengeneza fursa nyingi na kupitia Mradi wa Niobium na Kiwanda cha Ferroniobium, ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakuwepo ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000. Mradi utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (US$ 220 million) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka shilingi bilioni 50 (US$ 22 million) na uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (Modern Manufacturing Plant and Smelter). Pamoja na kuingiza teknolojia hii adimu na ujuzi (skills transfer) pia itachangia huduma za kijamii (corporate social investment in community) na chanzo cha fedha ya kigeni. Naunga mkono hoja.