Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa hii fursa ya kutoa mchango wangu. Nianze kwa kuwashukuru wapiga kura wa Nkenge kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kunirejesha katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii pia, kupongeza hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Rais alipozindua Bunge hili. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa taarifa aliyowasilisha leo hii hapa Bungeni ambayo imezingatia pia maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Ukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Rais katika ukurasa wa 16, alibainisha kwamba matarajio yake ifikapo mwaka 2020 angalau viwanda viweze kutoa ajira 40% ya ajira zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa sasa na taarifa za Mheshimiwa Waziri alizowasilisha, inaonesha kwamba kwa mwaka 2014 viwanda vimetoa ajira kwa asilimia 3.1. Sasa lengo letu ni kuhakikisha sasa viwanda vitoe ajira ifikapo mwaka 2020 kwa 40%. Sasa kutoka asilimia 3.1 kwenda 40% kuna kazi kubwa ya kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu wa leo, nitabainisha masuala muhimu ambayo yakizingatiwa tutaweza kufikia 40% ya ajira kutolewa na viwanda. Jambo la kwanza, ukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, amebainisha kwamba, kwa vyovyote vile itakavyowezekana lazima tutekeleze utekelezaji wa miradi mikubwa ya kielelezo au wanasema flat projects.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimepitia ile orodha ya ile miradi, nikagundua kuna mradi mkubwa umesahaulika kwa bahati mbaya na mradi wenyewe ni ujenzi wa Kajunguti International Airport. Mheshimiwa Rais alipokuwa kwenye kampeni, jambo mojawapo aliloahidi wana Misenyi, alisema akiingia Ikulu, fedha zote atakazozikuta atazileta Misenyi kulipa fidia kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa Kajunguti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwakumbusha wasaidizi wake, wahakikishe katika Mipango ijayo, wahakikishe wanazingatia maelekezo ya Mheshimiwa Rais, lakini pia Kajunguti International Airport ni muhimu siyo tu kwa Misenyi, lakini pia kwa Taifa. Tunazungumza kuanzisha masoko ya kimkakati kwa sababu uwanja huo wa Kajunguti, siyo tu tutajenga uwanja wa Kimataifa lakini utaendana na ujenzi wa viwanda, utaendana na kuendeleza maeneo maalum (Special Economic Zones), utaendana na kuweza kuzalisha bidhaa mbalimbali zilizo karibu na Soko la Afrika Mashariki ukizingatia ukweli kwamba tunapakana na Rwanda, Burundi na Uganda, lakini pia tunaweza kuuza maeneo mengine. Kwa hiyo, naomba hilo lizingatiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia, tunaposema kwamba tunahitaji kuwa na uchumi wa viwanda, hatuwezi kusahau kilimo. Nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri aliyowasilisha leo hii hapa, nimesoma yote, lakini sioni maneno ya kilimo kwanza yakijitokeza, nikafikiri labda tumeanza kusahau sahau kilimo kwanza. Nitoe ushauri, kilimo kwanza ni jambo la muhimu, hatuwezi kuwa na uchumi wa viwanda bila kuwa na kilimo kinachozalisha kwa ziada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nimesoma hotuba hii, mara tatu, mara nne, sikuona maneno Big Results Now yakijitokeza. Nikaanza kufikiri kwamba labda sasa Big Results Now siyo msisitizo tena, lakini nikumbushe kwamba Big Results Now ni muhimu, zile sekta sita ni muhimu, zisipozingatiwa kwenye mipango yetu tutafika sehemu tuisahau.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia ni kwamba unapozungumza kwamba unataka uwe na uchumi wa viwanda lakini unapenda vilevile kuhakikisha una kilimo kinachozalisha kwa ziada, lazima tuhakikishe migogoro ya wafugaji na wakulima inakoma. Jimboni kwangu kuna mgogoro mkubwa wa Kakunyu. Mgogoro huu umechukua zaidi ya miaka 15. Sasa kuwa na mgogoro ambao haumaliziki. Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete alishatoa maelekezo mgogoro huu uishe na Mheshimiwa Magufuli ametoa maelekezo mgogoro huu uishe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Lukuvi, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi pia washirikiane kuhakikisha wanamaliza mgogoro huu kabla sijaanza kuchukua hatua nyingine ambazo nitaona zinafaa kama mwakilishi wa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napenda niseme naunga mkono hoja. (Makofi)