Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu. Awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kipekee kuishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri zinazofanyika chini ya mama yetu Samia yenye matumaini makubwa ya kumtua ndoo mama kichwani. Kwa kweli ninasema hivi nilikuwa najaribu kuangalia bajeti zilizopita kwa kweli inaweza ikawa ni bajeti ya kwanza ile bajeti tuliyopitisha mwaka jana ambayo imeweza kutekelezwa kwa asilimia kubwa asilimia 95 ukijaribu kuangalia pesa ambayo ilikuwa imetengwa bilioni 778 lakini pesa ambayo tayari imeshatolewa ni bilioni 743 kwa kweli ni hatua nzuri sana.

Mheshimiwa Spika, kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Maji kwa kazi kubwa mnayoifanya. Kwa kweli mnafanyakazi kubwa lakini kikubwa ambacho niwapongeze kwa namna ambavyo mnatupa sisi ushirikiano wa Bunge tunapowaletea mahitaji ya wananchi wetu. Kwa kweli kipekee ninasema mmekuwa mkinipa ushirikiano mkubwa na leo hii ninaposema ninapongeza kwa kweli napongeza kwa dhati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu kuangalia mara nyingi wanasema Wabunge wa CCM wanapongeza lakini sasa kazi zinapofanyika lazima tupongeze. Nilikuwa najaribu kuangalia bajeti ambayo tumepitisha mwaka jana kwa Kyerwa tuna mradi mmoja wa Kaisho, Isingiro kuna bilioni 1.3 tuna mradi wa Kimuri, Chakarisa Rwanyango bilioni 2.1, tuna mradi wa Nyamiega Nyakatera ambao una bilioni 1.3 mradi wa Runyinya Chanya bilioni 4.6 mradi wa Kaisho Isingiro bilioni 1.9, mradi wa Murongo milioni 738, mradi wa Karongo milioni 734. Mradi wa kuchimba visima milioni 630.

Mheshimiwa Waziri kwa kweli ninakushukuru na miradi hii ninayoitaja tayari wakandarasi wamesha saini mkataba na wako kazini wanaendelea. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri mimi nakushukuru sana kwa jinsi ambavyo unaendelea kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapochangia pamoja na miradi hii ambayo imeletwa kwa Kyerwa bado naendelea kuomba Mheshimiwa Waziri juzi tumekutana pamoja na wewe na Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Mkurugenzi wa Maji Vijijini tumejadili juu ya mradi wa Kyerwa ambao unaenda Nyaruzumbura unaenda Nyakatuntu mpaka Kamuli.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ninausemea sana kwa sababu mradi huu mndiyo utakuja kuwa mkombozi kwa wananchi wa Kyerwa ambao utaenda kuhudumia zaidi ya wananchi karibu elfu arobaini. Lakini tunaposema mradi wa Kyerwa mpaka Kamuri mradi huu utakapokuwa umekamilika tukapeleka maji mpaka kwenye kata ya Kamuri tutaweza kusambaza maji kwenye maeneo ya kata ambazo hazijawahi kufikiwa kabisa tangu nchi hii imekuwepo Kata kama Kikukuru, Kata kama ya Businde, Kata kama ya Bugara kata nyingine zote pamoja na Kibale ambazo hazijawahi kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri kama tulivyokubaliana mradi huu ninaomba sana uanze kwa sababu ulipitishwa kwenye bajeti iliyopita na ninaamini kwenye bajeti hii umo. Niwaombe sana mradi huu ni muhimu na ndiyo utaenda kuondoa kero ambayo ipo kwa wananchi wa Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, mambo mengine Mheshimiwa Waziri ni pamoja na miradi mingine ambayo tumeleta hii miradi mingine ambayo imepitishwa kwa mfano mradi wa Isingiro Kaisho mradi huu utajengwa kwa awamu. Kwa hiyo, niombe awamu hii inapoisha Mheshimiwa Waziri tupate pesa ili tuweze kukamilisha mradi huu kwa sababu mradi huu ulikuwa wa muda mrefu na ulikuwa ni kero sana kwa wananchi wa Jimbo la Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine niombe sana Mheshimiwa Waziri miradi tayari tumeshasaini mikataba pamoja na wakandarasi niombe sana pesa ije kwa wakati ninaamini wale vijana mliowaweka kijana wangu Tungaraza pale Kyerwa anafanyakazi nzuri sana mleteeni pesa kwa upande wa usimamizi hana shida akishirikiana pamoja na Meneja wa Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ambalo niliona nichangie nchi hii Mungu ameijaalia sana tuna vyanzo vingi sana vya maji yaani watanzania kukosa maji kwa kweli ni jambo ambalo ni la ajabu lakini tuna vyanzo vingi vya maji. Lakini pia Mungu ametujaalia vipindi virefu vya mvua ukipita pale Dodoma karibu na kwa Mheshimiwa Spika ambaye amestaafu unakuta maji yamevuta mpaka barabara huwa najiuliza Serikali kwa nini hailioni hili? tukavuna haya maji kwanza pale tukitenga yale maji yanaweza kutusaidia kwa mahitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine yale maji inaweza ikawa ni kivutio hata na Dodoma na wao wakaonekana wana kama ziwa yale maji ni mengi sana lakini yanaishia kupotea kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye mipango yenu mje na mipango ya kuvuna haya maji tuwe na mabwawa makubwa wananchi wa Dodoma waachane na maji ya chumvi ukimaliza kuoga kama umesahau kujipaka mafuta utashangaa ni kama umejipaka poda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili na lenyewe uliangalie ili na watu wa Dodoma waweze kupata maji ambayo ni maji yanaitwa maji baridi maji safi ambayo hayana chumvi. Kwa hiyo, niombe sana na hili na lenyewe Serikali iliangalie.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilisemee Mheshimiwa Waziri ule mradi wetu mkubwa ambao tulikubaliana utajengwa kwa awamu huu mradi msije mkausahau mradi wa vijiji 57 tumeanza kuujenga kwa awamu lakini tuendelee kuufikiria ni namna gani tutaendelea kutenga kwenye bajeti ili wana Kyerwa ifike sehemu tuondokane na adha ya kutopata maji wakati mwingine ukifika sehemu nyingine ukiona maji wanayotumia kwa kweli hali ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nirudie tena Mheshimiwa Waziri ninakushukuru sana kwa kazi nzuri unayoifanya na wewe pamoja na Ofisi yako lakini pia ushirikiano ambao mmekuwa mkinipa ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)