Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ya Maji. Kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kumpa hongeza sana kwa kazi kubwa anayoifanya ya kutatua mambo mbalimbali changamoto mbalimbali za wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais tumeona juzi imekuja changamoto ya mafuta Mheshimiwa Rais amewajibu wananchi wake kwa kuweka ruzuku ya bilioni 100 ili kuwapunguzia kasi ya bei ya mafuta wananchi wa Tanzania waweze kupata huduma hiyo kwa gharama nafuu. Hilo siyo jambo dogo Mheshimiwa Rais wetu anafanya kazi kubwa sana anahangaika huku na huku kuhakikisha watanzania wanapata huduma zote muhimu kwa gharama nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo naomba sasa nirudi kwenye Wizara yetu ya Maji nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha wanakwenda kumtua mama ndoo kichwani na kuhakikisha sasa wananchi wa Tanzania wanakwenda kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, nikipongeze Chama cha Mapinduzi pia katika Ilani yake ya CCM sura ya kwanza kipengele cha kwanza ukurasa wa tatu Ilani inasema Serikali itaongeza idadi ya wananchi wanaopata huduma ya upatikanaji wa maji safi na salama vijijini kutoka asilimia 47 mpaka kufikia zaidi ya asilimia 70 katika kipindi hiki kinachokuja. Hili ni jambo kubwa ninapoanza kutaka kuzungumza katika Wizara hii ya Maji ninaona jinsi gani mipango ya bajeti inavyokwenda sasa kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa vitendo. Nakipongeza Chama chetu cha Mapinduzi kwa kuisimamia vizuri Serikali na hata katika bajeti hii sasa tunakwenda kufanya hiyo kazi kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti hii nitazungumzia masuala ya ujenzi wa bwawa la Kidunda. Mkoa wa Dar es Salaam unategemea kupata maji safi na salama katika chanzo kikuu cha Bonde la Ruvu. Lakini katika kipindi hapa nyuma tumeona ilitokea ukame Mkoa wa Dar es Salaam tukawa tunapata maji kwa mgao. Lakini katika bajeti hii inaelekeza sasa inakwenda kutengeneza bwawa la Kidunda, naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuamua hilo na niombe hili bwawa la Kidunda sasa litengenezeke ndiyo mwarobaini pekee wa upatikanaji maji fulltime katika Mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemuona Mheshimiwa Waziri wakati ule wa ukame alikuwa anaingia kwenye mabonde anaingia huku na huku tunaumia Mheshimiwa Waziri utaliwa na mamba suluhisho ni kujenga bwawa la Kidunda. Kwa nini nasema bwawa la Kidunda Mkoa wa Dar es Salaam wenye watu takriban kwa mujibu wa sensa 2012, 5,465,420 wanategemea maji kwa asilimia kubwa kutoka kwenye mto Ruvu.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Ilala ina takriban watu 1,534,489 hao wanategemea maji kutoka mto Ruvu, Wilaya ya Kinondoni yenye takriban watu 1,164,174 inategemea maji kutoka huko kwenye hilo bonde la Ruvu. Ubungo yenye takriban watu 1,058,597 wanategemea kupata maji huko ya mto Ruvu. Lakini pia Temeke nayo yenye watu takriban 1,510,000 wanategemea kupata maji kutoka mto Ruvu lakini kama haitoshi kupitia DAWASA hiyo hiyo Kibaha mjini na vijijini Chalinze yenye watu takriban watu 233,000 wanategemea kupata maji kutoka chanzo cha Ruvu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe Kisarawe, Bagamoyo hao wote kupitia DAWASA tunategemea maji ya mto Ruvu suluhisho la tatizo la maji yapatikane saa zote iendane na idadi ya watu. Dar es Salaam chanzo cha Ruvu kimeanza toka sasa toka Uhuru sasa ni karibu miaka 60 hakijapatikana chanzo mbadala zaidi ya visima vya Kimbiji na Mpera lakini mradi huu bado haujakamilika. Sasa Serikali iende ikaandike historia mpya kwa kuweka hifadhi ya maji katika Bonde la Mto Kidunda.

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo kutokana na mabadiliko ya tabia nchi kumekuwa na mafuriko mengi yanatokea maji mengi yanapotea kwa mpito yanatoka kwenye mto Ruvu yanaingia baharini lakini baada ya hizo mvua kupita ukame unarudi suluhisho lake ni maji ya Kidunda lakini maji haya hayataisaidia mkoa wa Dar es Salaam yatasaidia Mkoa wa Pwani, Mkoa wa Morogoro hilo bwawa la Kidunda litasaidia katika Mkoa wote wa Morogoro katika kuchachua uchumi, uvuvi na kilimo lakini na sisi wa Dar es Salaam tunapata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mji wa Dar es Salaam unakua kwa kasi enzi hizo inawekwa hiki chanzo cha Ruvu kuwa chanzo pekee ile Kariakoo haikuwa hivyo leo Kariakoo magorofa yote yale yanatumia maji yanayotoka mto Ruvu. Sasa niombe Serikali hili bwawa la Kidunda tena nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuliweka katika mpango hili bwawa. Tumekuwa muda mrefu linaingia toka mimi nimeingia hapa Bungeni linaingizwa kwenye bajeti linatoka linaingizwa linatoka hivi lini linatekelezwa. Sasa nimuombe Mheshimiwa wangu Rais atengeneze historia mpya katika Tanzania kwa kuamua sasa kulijenga hili bwawa la Kidunda.

SPIKA: Mheshimiwa Mariam Kisangi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kalogeresi.

T A A R I F A

MHE. INNOCENT E. KALOGERESI: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa mchangiaji ni ukweli usiofichika suluhi la Dar es Salaam ni bwawa la Kidunda ambalo linajengwa katika Wilaya ya Morogoro Vijijini Jimbo la Morogoro Kusini ambapo natoka na sisi wana Morogoro Kusini tumejipanga kuhakikisha kwamba vikwazo vyote ambavyo vitakwamisha ujenzi wa bwawa hili vitaondoka Jumatatu nitakuwa na Mkurugenzi wa DAWASA kule kuhakikisha kwamba mambo yanakwenda vizuri.

SPIKA: Mheshimiwa Mariam Kisangi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo naipokea kwa mikono miwili na naomba sana Wizara ilisimamie hilo tuweze kupata maji wote mikoa yote hiyo ineemeke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nije kwenye mchango wangu wa pili kuhusu chanzo cha maji cha Visima vya Kimbiji na Mpera niipongeze sana Serikali mradi huu umekuwa ukisuasua kwa muda mrefu angalau sasa umeanza kuleta matumaini tunaona kwamba katika kata kama za Mjimwema, Kibada kumeanza mpango wa kusambaza mabomba. Lakini changamoto kubwa ambayo wasiwasi umewaingia wananchi wa maeneo hayo ni kuangalia jinsi ya gharama za maji.

Mheshimiwa Spika, kama ulivyoongea Mheshimiwa Waziri tunakuomba kama ulivyosema kitu chema kinaigwa. Hebu tuendane na vile wanavyofanya wenzetu wa umeme vijijini tuangalie mipango mahsusi ambayo itamwezesha mwananchi kuwekewa maji na walau kulipa kwa kiasi kidogo aendelee kufanya matumizi ninasema hivyo kwa sababu watu wameanza kuogopa hata kukwepa kuletewa hayo maji.

Mheshimiwa Spika, lakini pia niombe sasa huu mradi wa visima vya Kimbiji na Mpera sasa uwawezeshe wananchi angalau wa Wilaya ya Kigamboni wote waweze kupata maji safi na salama. Maji haya yaende kwenye Kata yenyewe ya Kisarawe II, yaende mpaka Mwasonga, yaende Tunduisongani, yaende Pembamnazi, yaende Kimbiji lakini pia maji hayo…

SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa Mariam.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa utendaji wake mahiri ahsante sana. (Makofi)