Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na ninakushukuru wewe pia kwa kunipa nafasi.
Nami niungane na watangulizi wangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa juhudi kubwa anazozifanya kuhakikisha kwamba Tanzania wanapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Waziri na timu yake yote Katibu Mkuu, Naibu Waziri, Mkurugenzi wa RUWASA bahati njema sana watu hawa wamepata fursa ya kufika maeneo yetu ya Mkoa wa Mtwara hususani kwenye mradi wa maji ya Makonde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwe miongoni mwa watu ambao kesho watashika shilingi ya wizara hii mimi Katani kwa haya yafuatayo; tarehe 16 Septemba, 2016 Rais wa sasa akiwa Makamu wa Rais alifika Tandahimba, kwenye mpango wa bajeti ya 2015/2016 mradi wa maji wa Makonde uliwekwa na kwenye maelezo ya mpango ule ilikuwa ni kupata fedha kutoka Benki ya India ambayo leo ukisoma bajeti hii ya Wizara ya Maji inaonekana tayari Wakandarasi wanakwenda kutekeleza mradi wa maji wa Miji 24.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana kitabu cha Wizara ya Maji cha 2017/2018 mradi huu wa maji wa Makonde uliwekwa hata ukienda kutafuta taarifa zake hatukupata fedha, 2018/2019 mradi wa Makonde ukawekwa tena tukiwa tunaaminishwa kwamba mradi huu utatekelezwa itakapopatikana fedha za kutoka Exim Bank ya India.

Mwaka 2019/2020 ukawekwa tena, 2020/2021 ukawekwa tena, leo 2022/2023 ukienda ule ukurasa wa 55 mradi huu umewekwa juu unaonekana kwamba ni mradi wa Miji 28 lakini kwenye Miji 28 imegawiwa miradi ya Miji 24 ambayo inakwenda kunufaika na mkopo ule kutoka Exim Bank ya India, hii miradi minne ambayo ni mradi wa Makonde, mradi wa Songwe wanasema fedha zinatokana na mapato ya ndani, lakini ukisoma hakuna kifungu kinachoonyesha hizo fedha zimetengwa wapi, maana yake hapa nina wasiwasi sana sisi watu wa Mtwara na watu wa Lindi tuna bahati mbaya kwenye miradi yote ya maendeleo, kazi yetu ni kuwekewa mipango lakini haitekelezwi! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelia barabara hapa kila tunapokuja tunawekewa kwenye mpango kwenye utekelezaji hakuna kitu, ndiyo kinachoonekana kwenye bajeti hii ya maji ya ndugu yangu Aweso. Mheshimiwa Aweso ambaye amefika Mtwara ameona adha ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Tandahimba leo maji yananunuliwa Shilingi 1,000 mpaka Shiingi 2,000 lakini kwenye bajeti hii watu hapa ambao tayari walishakuwa na miradi ya Bilioni 300, Bilioni 400 wanaendelea kuongezewa fedha Lindi na Mtwara hakuna kinachoonekana, kwani sisi ni watu wa Msumbiji au ni Watanzania kama Watanzania wengine ambao wanapata keki ya Taifa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelikosea nini Taifa hili, tukienda kwenye barabara shida, tukija kwenye maji shida, tukija kwenye umeme shida, watu wa Lindi na Mtwara tumekosea nini Taifa hili au mipaka aliyogawa mzungu mnatufanya sisi ni watu wa Msumbiji siyo Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mama Samia alikuja mwenyewe Tandahimba alizungumza juu ya mradi huu leo mnapata fedha Bank ya Exim kutoka India mradi huu mmeutoa mnasema ni mradi wa mapato ya ndani! Tumeona barabara kilometa 50 tu zile mlisema mapato ya ndani tumejenga miaka mitano na mradi huu maana yake mnataka tujenge miaka mia tatu sasa!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kwenye jambo la maji watu wa Mtwara na Lindi tumeachwa nyuma kuliko watu wengine wowote, kila anayesimama hapa anasema mimi nimepata bilioni moja, bilioni nne, bilioni tano, bilioni 50, bilioni 300, Lindi na Mtwara hizo fedha ziko wapi Mheshimiwa Waziri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitarajia ujio wa Waziri kule, ukaona mradi wa maji Makonde umekuja na Katibu Mkuu, ameona mradi wa maji wa Makonde, amekuja Mkurugenzi wa RUWASA mmeona adha na matatizo ya watu wa Lindi na Mtwara, nilitarajia kwenye bajeti hii tungeona kuna trilioni moja inaenda Lindi na Mtwara kutatua changamoto za maji, bahati mbaya sana mnapeleka matrilioni mnatoa maji Ziwa Victoria yanakuja mpaka Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tandahimba, Newala, Nanyamba, Mtwara, Liwale tuna Mto Ruvuma hauzidi kilomita 100 watu wote hawana maji safi na salama, mtuambie Wizara mna mkakati gani, mna dhamira gani na watu wa kusini au sisi mmetuondoa kwenye Taifa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu vinasikitisha sana, kila tunaposimama hapa kuzungumza bajeti za Lindi na Mtwara ni malalamiko tu, kaeni fikirieni Mikoa ambayo ilisahaulika basi, angalau mpeleke fedha na sisi tujione kwamba na sisi keki ya Taifa hili tunagawana kwa mgawanyo ambao watu wengine wanapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wote waliochangia hapa mtu akisema anasema kwangu nilipata mradi wa maji Bilioni Nne, leo nimepewa Bilioni 10 mwingine bilioni 15 Lindi na Mtwara hatuna hiyo miradi tumekosea nini, Mheshimiwa Waziri umekuja mwenyewe kule siyo kwamba hujayaona umeyaona! Kamati, Katibu wa Chama alivyokuja na Sekretarieti yake aliagiza Katibu Mkuu aje akaja mmejionea, mnataka kutupa wakati mgumu 2025 kwa jambo la maji Lindi na Mtwara, mnataka kutupeleka kwenye wakati mgumu, Mama anaupiga mwingi Mheshimiwa Waziri unaupiga mwingi lakini hili la maji Lindi na Mtwara Mzee wangu mimi kesho nashika shilingi hapa, kama hakuna mambo yanayokwenda kuonekana kwamba Lindi na Mtwara tumeingizwa mimi ni wa kwanza kushika shilingi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuone reflection ya keki ya Taifa mnayoitaja sehemu nyingine ambazo walikuwa na miradi ya maji mnaendelea kuilundika, tuone sasa mradi wa maji wa Makonde ambao mwenyewe umefika umeona uchakavu wake, umeona shida zake, Mtendaji Mkuu wa Wizara hii Katibu Mkuu amefika ameona shida zake, mnakuja kwenye bajeti ya Wizara ya Maji mnatupa sarakasi za abunuasi, mmeandika vizuri, jambo ambalo liko kwenye mpango kwa miaka sita, Mheshimiwa Aweso mimi na wewe tukiwa hapa kila bajeti ya maji mnasema mradi huu wa Makonde tunapata fedha Exim Bank, leo mnaleta Wakandarasi mmeondoa Makonde mradi ambao ulikuwa mwanzo mnasema huu utatekelezwa kwa fedha za ndani, tunayo mifano ya fedha za ndani ndugu zangu, miradi tunayotekeleza kwa fedha za ndani tunayo mifano hatutaki turudi huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuomba Mheshimiwa Waziri umepata fursa mwenyewe ya kufika Lindi na Mtwara, tuone sasa mnapokaa kuweka vizuri bajeti yetu hii ili iende sawa, tuone mradi wa maji wa Makonde ambao unakwenda kuwasaidia watu wa Mtwara, Newala, Nanyamba, Nikitangali ipo kwenye mpango wananchi hawa wakapate maji safi na salama. Nikuombe sana sisi watu wa Kusini tumekuwa nyuma kwa muda mrefu, tunayo historia kwa sababu ya vita ya Msumbiji mkatuacha sawa, watu wamejikomboa ni wakati wetu sasa wakufikiria kwamba wenzetu walitenga maeneo yao kusaidia kusaidia ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika sasa watu wamejikomboa, hao watu wapate huduma za msingi ikiwepo maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana hili jambo mliangalie kwa uhakika wa hali ya juu sana. Ndugu zangu Bungeni hapa mnaona kila akisimama mtu wa Lindi na Mtwara ni malalamiko, kila Wizara tutakayosimama Lindi na Mtwara tunalalamika, wenzetu wanapongeza, mimi nitakupongeza kwa sababu Waziri unajua shida ya maji iliyokuwepo, lakini nitashika shilingi kama sikuona mradi wa maji wa Makonde una bajeti mahsusi inayoenda kumuondoa ndoo Mama wa Tandahimba, mama wa Newala, Mama wa Kitangali, Mama Nanyamba, Mama wa Masasi, Mama Ruangwa, japo wenzetu wa Ruangwa wana visima kidogo lakini wanahitaji maji safi na salama, hawana maji ya bomba mazuri hawa pia! Mzee hawezi kusema tu kwa sababu ndiyo mwenyewe kakalia Kiti lakini wanahitaji maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda Liwale huko balaa tupu! Nenda Liwale kwa Mheshimiwa Kuchauka ukaangalie balaa la Lindi na Mtwara, nenda Nachingwea kaangalie balaa la maji Lindi na Mtwara, Lindi na Mtwara kuna nini Serikali msichofikiria, msichotuonea huruma watu sisi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana tumeonewa sana kwenye Taifa hili, kwenye miradi ya maendeleo tumeonewa sana, ufike wakati mnapokaa kwenye bajeti sasa muangalie Mikoa ya Kusini angalau tunataka tuwe kama Kilimanjaro, tunataka tuwe kama Arusha, nenda Arusha leo kila Kijiji mabomba yanapasuka..

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Katani, umeeleweka. Nimekuongezea muda mrefu; tunakushukuru.