Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu. Niungane na Wabunge wenzangu kuwapongeza Wizara ya Maji ikiongozwa na Mheshimiwa Aweso, Injini Prisca Mahundi lakini shukrani za kipekee pia ziende kwa Watendaji wa Wizara ya Maji wakiongozwa na Injinia Sanga. Lakini niwashukuru sana kwa ushirikiano wao mkubwa walionipa wakati wa kutekeleza miradi ya maji katika Jimbo la Meatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri inayofanya, fedha nyingi sana zimekusanywa na zimepelekwa. Yapo mabadiliko makubwa ya fedha ukilinganisha na mwaka jana. Mfuko wa Maji wa Taifa umeendelea kukusanya vizuri fedha zake na kuzipeleka kama ilivyo katika Wizara ya Maji. Mwaka jana zilipelekwa kwa asilimia 97 lakini kwa mwaka huu toka mwezi wa tatu asilimia 94 zimeshapelekwa kwa zaidi ya shilingi bilioni 160.8 zimepelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia upelekaji wa fedha katika Mfuko Mkuu wa Serikali umechangizwa haswa na tozo tuliyoipitisha mwaka jana. Kwa sababu mwaka jana ni asilimia 43 tu ya fedha za Mfuko Mkuu wa Serikali zilipelekwa Wizara ya Maji. Lakini mwaka huu mpaka Machi zimepelekwa asilimia 94 kama nilivyoeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba wananchi tuendelee kuunga tozo hii iliyowekwa katika mafuta, inatusaidia kupata maji. Nanyi ni mashahidi mnaona kila Mbunge anavyonyanyuka anapongeza katika Jimbo lake kwa fedha zilizopelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimejikita katika mapato yaliyotokana na ruzuku ya Serikali Kuu. Nijielekeze katika Jimbo la Meatu. Jimbo hili lina ukame mkubwa, lakini kazi kubwa sana imefanyika ndani ya mwaka mmoja. Ndani ya mwaka mmoja miradi imetelekezwa ya Shilingi bilioni tatu. RUWASA imetekelezwa miradi ya bilioni 1.5, huku Mamlaka ya Maji Mji wa Mwanuzi Shilingi bilioni 1.6 zilipelekwa kutekeleza miradi ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mwanuzi ambayo inatekelezwa na Mamlaka ya Maji, Vijiji vyote saba ndani ya Kata ya Mwanuzi Makao Makuu ya Wilaya ya Meatu zinaenda kupata maji kwa mara moja. Historia inaenda kuandikwa, haijawahi kutokea. Kata hiyo imekuwa na adha kubwa ya upatikanaji wa maji. Sisi wote ni mashahidi, ilifikia mahali tukaanza kuletewa maji kwa kutumia maboza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa RUWASA miradi iliyotekelezwa ni Mwabuzo Shilingi milioni 267; Malwilo Shilingi milioni 100; Isembanda Kabondo Shilingi milioni 586; Itongolyangamba Shilingi milioni 100 na Kata ya Mwamanimba fedha zilizotokana na mapambano ya UVIKO Shilingi milioni 452 zimepelekwa katika Kata ya Mwamanimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Mwamanimba ilipewa kipaumbele kwa sababu ni kata iliyokuwa imeathirika na mabadiliko ya tabia nchi. Kama tutakumbuka, miaka ya nyuma shule moja pale iliwahi kuwa ya mwisho kitaifa, kwa sababu muda mwingi watoto walienda kufanya kazi zilizotakiwa kufanywa na mama zao, wakati huo mama zao walienda kutafuta maji zaidi ya umbali wa kilomita saba wakichukuwa masaa mengi kwa ajili ya ufuatiliaji wa maji. Kwa hiyo, kupatikana kwa mradi huu utakuwa ni ukombozi katika Kata ya Mwamanimba. Wanawake wenzangu watajikita sasa katika kufanya majukumu ya kujiongezea kipato katika maisha yao kwa sababu maji yatakuwa yamepatikana yaliyokuwa yanachukuwa muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya kwa kuidhinisha fedha mbalimbali katika miradi mbalimbali ya Jimbo la Meatu. Naomba nitofautiane na kauli iliyotolewa jana kwamba mradi wa Mwanuzi ulipokamilika tayari kumekuwa na mgao wa maji. Mheshimiwa Waziri ni shahidi, ule mradi una muda wa miezi miwili. Hata kwenda kuuzindua, ndio tunategemea kwenda kuuzindua na Mheshimiwa Waziri. Matumizi yake, hata 0.001 ya 100, bado hatujaanza kuyatumia. Tumekuwa tukiufuatilia ule mradi toka hatua ya usanifu mimi pamoja na viongozi wa kimkoa, viongozi wa kiwilaya. Tulifuatilia, kile chanzo kina maji mengi sana sana. Ilikuwa ni ndoto ya wana- mwanuzi zaidi ya miaka 20 kukipata kile chanzo kukitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya awamu ya sita chanzo kile kimeweza kutekelezwa. Kinachochangiza kuwe na mgao katika Mji wa Mwanuzi ni kukatikakatika kwa umeme. Naomba niweke kumbukumbu sahihi. Siyo kwa sababu chanzo hakina maji, ni kukatikakatika kwa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme unapokuwepo wananchi wote wanapata maji kwa wakati mmoja na wenyewe ni mashahidi. Umeme unapokatika zaidi ya siku tatu, lazima tugawane kidogo kidogo ili tusimalize kabisa. Kwa hiyo, naomba niwatoe wasiwasi wananchi wenzangu wa Jimbo la Meatu, maji yapo ya kutosha. Nami kama Mbunge, kazi yangu sasa itakuwa ni kuiomba Serikali ikamilishe ujenzi wa kituo cha kupozea umeme katika Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo kile kitakapokamilika zile dharura ndogo ndogo zinazosababishwa na kukosekana kwa kituo cha kupoozea umeme zitapunguza ile kasi ya kukatikakatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite katika mradi wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi. Mradi huu umekuwa wa muda mrefu sana. Mwaka 2021 wakati nachingia nilimwomba Mheshimiwa Waziri kama hawa wafadhili wameshindwa kutuchangia fedha, basi Serikali ifanye kwa mapato yake yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri, aliichukua hoja yangu akaifanyia kazi kwa kukaa na yule mfadhili na alikubali kutoa fedha. Naye mara nyingi amekuwa akinishuhudia, sasa mradi utaanza kutekelezwa. Naomba sasa kazi ya utekelezaji wa mradi basi ianze kwa speed, kwa kuwa mradi huo ulifungwa mkataba mwezi Mei, 2019 kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Benki ya KFW ya Mfuko wa Mabadiliko ya Tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee namshukuru Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia, mfuko huu ulitafutiwa fedha na Ofisi ya Makamu wa Rais, yeye akiwa Makamu wa Rais. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa namna anavyopambana na athari ya mabadiliko ya tabianchi. Ndiyo maana alipambana kuhakikisha mradi huu tunaupata. Mradi huu ulikuwa unatekelezwa kwa phase ya kwanza toka Busega, Bariadi mpaka Itilima mpaka mwaka 2026.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi toka Bunge la Kumi na Moja nilikuwa nikiomba mradi huu utekelezwe hadi Wilaya ya Meatu ambayo imeathirika kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya tabianchi ili kuleta dhana nzima ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Namshukuru Mheshimiwa Rais, kwa sasa mradi huu Meatu inaenda kuingia katika awamu ya kwanza. Mheshimiwa Rais anaifahamu Wilaya ya Meatu ilivyo, alikuja zaidi ya mara tatu katika Wilaya ya Meatu. Mara ya kwanza alikuja kuomba kura, mara ya pili alikuja kushukuru na mara ya tatu alikuja kuzindua Bwawa wa Mwanjoro. Maeneo yote anayajua jinsi yalivyoathirika na ukame ndiyo maana ameridhia Wilaya ya Meatu iingie katika awamu ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wananchi wa Meatu tutaendelea kukuombea Mheshimiwa Rais, Mwenyezi Mungu akupe afya, Mwenyezi Mungu akupe nguvu uweze kuendelea kutekeleza majukumu yako. Nami nikiri kabisa katika awamu ya sita utekelezaji wa miradi ya maji umeongezeka kwa kasi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba ambayo niliyokuwa nayasemea. Naomba katika utekelezaji huu wa mradi wa mabadiliko ya tabianchi iwepo component ya maji ambayo hayajatibiwa ili yaweze kusaidia mifugo yetu, ili yaweze kusaidia kilimo cha umwagiliaji. Mkoa wa Simiyu na Wilaya ya Meatu ina athari kubwa. Kwa mwaka huu Jimbo la Meatu wananchi walilima hawakuotesha kwa sababu ya ukame mrefu. Mifugo ya wananchi ilikufa sana kwa sababu ya ukame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutapata maji yasiyotibiwa yatasaidia kupunguza gharama. Kwa mwaka huu upo uwezekano mkubwa hata mchicha tunaenda kuununuliwa Mwanza, upo uwezekano mkubwa hata nyanya tunaenda kuzinunulia Mwanza kwa ajili ya ukame mkubwa. Endapo mradi huu utatekelezwa kwa njia ya umwagiliaji, changamoto hizi ndogo ndogo tutaweza kukabiliana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)