Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii jioni ya leo na mimi niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maji nikianza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nikianza kwa maneno Matakatifu ya Mwenyezi Mungu kutoka katika Kitabu cha Quran sura ya 21 Aya ya 30 inasema na ninanukuu, “Wajaalna minalma kula shain hayi” tafsiri yake ni kuwa, tumejaaliwa kutokana na hayo maji kuwa ndiyo chanzo cha uhai wa kila kitu hapa ulimwenguni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa spirit hiyo Mheshimiwa Waziri na timu yake watambue kabisa wao wamepewa dhamana na jukumu la kusababisha uhai wa kila kitu hapa ulimwenguni katika ardhi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nitumie fursa hii kwa upekee kabisa kwa dhati kabisa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Aweso, amekuwa ni Waziri kijana wa mfano wake katika kazi na kwa kweli anaishi kwa yale ambayo anayanena hapa Bungeni kila siku anapopata nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, hivi karibuni tuliona sakata na ameishi katika msemo wake wa “ukinizingua tutazinguana” kule Handeni ameshafanya vitu vyake majuzi mwezi uliopita. Baada ya watumishi wasio na dhamira njema na Mkandarasi asiye na dhamira njema aliyetaka kudhulumu kodi ya Watanzania kwa kulipwa zaidi ya Shilingi Milioni 600, bila kazi yenye tija Mheshimiwa Aweso amefukuza watumishi hao amewasimamisha Mkandarasi amemuweka pembeni uchunguzi unaendelea. Hivyo ndivyo tunavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, spirit ya Mheshimiwa Samia Rais wetu ya hapa kazi iendelee na kweli kazi inaendelea ndiyo namna hiyo, huko ndiko kumsaidia kwa ukweli Mheshimiwa Rais hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kana kwamba haitoshi timu nzima ya Wizara hii ya Maji wasaidizi wako wakiwemo Naibu Waziri Dada yangu Engineer Maryprisca ni Dada na Mama makini katika kazi. Katibu Mkuu rafiki yangu Engineer Sanga makini katika kazi, Naibu Katibu Mkuu makini katika kazi na Watendaji wote kwa ujumla wa Wizara hii kwa kweli wanakusaidia ipasavyo. Ni matarajio na matumaini makubwa kwa Watanzania ambao kwa muda mrefu tumekuwa na shida ya maji katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa spirit hiyo hiyo niendelee kupongeza Wizara yako lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais na nimshukuru Mheshimiwa Rais, kupitia mpango wa mapambano ya COVID na ustawi na maendeleo Jimbo langu la Kilwa Kusini tulipata Shilingi Milioni 473 kwa ajili ya kuendeleza na kustawisha miundombinu ya maji Kilwa Masoko. Kwa maana hiyo, ninayo furaha kukuambia kwamba kwa fedha hizi Shilingi Milioni 473 tunakwenda kutatua changamoto ya maji kwa asilimia zaidi ya 90 Masoko Mjini, Dodoma One, Nangurukuru, Mpara, Nangurukuru Ndogo, Mnazimmoja, Ngome, Utabiri, Mihina na maeneo mengine ya mjini Kilwa Masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa spirit yako ya “ukinizingua tutazinguana” naomba nikupe taarifa kwamba fedha hizi Shilingi Milioni 473 bado zimekaliwa huko kwenye Wizara yako hazijafika bado. Mkandarasi amefanyakazi kwa asilimia 80 hajalipwa chochote sasa swali langu ni nani anayekuzingua huko Mheshimiwa Waziri? Naomba usimamie hili ili wananchi wa Mji wa Kilwa Masoko waweze kunufaika na neema ya fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nipongeze kwa fedha ambazo Serikali yetu inakopa Serikali ya India kwa ajili ya maji katika Miji 28 na Miji yangu miwili ya Kilwa Kivinje na Kilwa Masoko ni sehemu ya kunufaika na mradi huu. Hapa ndio sehemu pakee ambapo Mheshimiwa Waziri utakuja kuweka alama ambayo kwa miaka sita ilikuwa inashindikana na wengine walikuwa wanabeza. Naomba nikupe taarifa katika maeneo ambayo walikuwa wanabeza na walikuwa hawaamini katika mradi huu ni pamoja na Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri kabisa amesema kwamba mikataba itasainiwa kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha. Maana yake ni kwamba kabla ya tarehe 30 Juni niombe na niungane na wengine kwamba mikataba hii ikasainiwe site huko ili wananchi wakashuhudie na inapowezekana basi tuma timu ya wataalam wako katika Wizara waende wakasimamie mikataba hii na sisi kwa niaba ya wananchi tutakwenda kuisimamia mikataba hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuishauri Wizara hii ni kujengea uwezo RUWASA, tunafahamu kwamba kwa mfano, mimi binafsi Meneja wangu wa RUWASA Engineer Mabula pale Kilwa anafanyakazi vizuri, anajituma sana kijana wa watu, lakini kinachopungua kwake ni mambo matatu tu na inawezekana hili ikawa na wengine pia. Jambo la kwanza bado anakaimu kama ilivyokuwa kwa wengine, jambo la pili ana timu ndogo ya watendaji wanaomsaidia kazi, lakini jambo la tatu vitendea kazi ikiwemo magari hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba utakapokuja kuhitimisha hapa kesho utoe majawabu ya changamoto hizi tatu za upungufu wa watumishi, Mameneja wanaokaimu pamoja na vitendea kazi ikiwemo na magari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo nilitaka nichangie katika bajeti ya Wizara ya maji ni kuhusiana na ahadi ambayo ilitolewa na aliyekuwa Waziri wa Maji wakati ule, katika Kata ya Limalyao, ilikuwa ni mwaka 2009 wakati Waziri wa Maji akiwa Mheshimiwa Prof. Mwandosya. Kata ya Limalyao Mheshimiwa Waziri ndio kata pekee katika Jimbo la Kilwa Kusini ambayo haina uhakika wa maji hata tone. Na Mheshimiwa Waziri Mwandosya wakati ule aliahidi kuchimba bwawa la kuweza kutosheleza kata nzima. Naomba nikumbushe tena ahadi hii iwe katika maandiko na kumbukumbu za Wizara na iwekwe katika mpango wa utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niendelee kupongeza Wizara. Wewe binafsi Mheshimiwa Waziri umekuwa ni mwenye kutembea nchi nzima. Naibu wako Mheshimiwa Engineer Maryprisca amekuwa ni mwenye kutembea nchi nzima. Kwangu Kilwa Naibu Waziri amefika pale Nangurukuru akasikiliza changamoto za maji za wana- Kilwa pale na tulimpa changamoto ya Kilwa Singino ambako kulikuwa na shida ndogo sana, naomba nitoe taarifa tu kwamba, naishukuru Serikali kupitia Wizara ya Maji kwamba, changamoto ile ya tatizo la maji Singino imekwisha Mheshimiwa Waziri, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nitakuwa mchoyo wa shukrani bila kushukuru wadau wengine wa maendeleo. Pale Kilwa sisi tumepata mdau wa maendeleo katika eneo hili la maji ambaye ni Green World Foundation Jimbo la Kilwa Kusini peke yake ametuchimbia tukishirikiana na viongozi Madiwani na Wenyeviti wangu wa Vijiji, Wenyeviti wangu wa vitongoji tumeshirikiananaye vizuri tumepata visima 83 ambavyo vinakwenda kutatua tatizo au kupunguza changamoto yam aji katika Kata ya Kivinje, Kata ya Masoko pamoja na Kata ya Kikole. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nikumbushie ahadi ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri aliahidi hapa Bungeni nikiwa nimeuliza swali la nyongeza mwaka jana kuhusiana na ombi langu mahususi la kupatiwa kisima cha maji katika Kijiji cha Nainokwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe taarifa kwamba, ahadi ile bado haijatekelezwa, nimekuwa nikifuatilia mpaka kwa Katibu Mkuu, lakini ananiambia Habari za mipango, leo nimeamua niizungumze hapa bungeni. Mheshimiwa Waziri anayekuzingua kutekeleza ahadi ambayo Naibu Waziri aliahidi kunipa kisima cha maji kimoja NaiInokwe ni nani huko Wizarani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha huu, tarehe 30 Juni, tupatiwe maji kisima kimoja Nainokwe, ili tukatengeneze uhai na tukasababishe uhai kwa wana-Nainokwe na wana-Kilwa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)