Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia hoja ya Waziri.
Kwanza, nianze kwa kutoa pongezi kubwa sana kwa hotuba nzuri na mipango mizuri iliyotolewa katika hotuba ya leo. Vilevile napenda kumpongeza Mheshimiwa Nape Nnauye, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri sana wanayoifanya katika majukumu waliyokabidhiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikubaliane na sehemu ya mchango iliyotolewa asubuhi hii na Mheshimiwa Zitto Kabwe, kwamba kijana akipewa majukumu na akafanya vizuri basi ni fahari kwa vijana, kauli hiyo ni sahihi kabisa. Pia naamini kwamba kijana akipewa majukumu anastahili kutiwa moyo, kuungwa mkono hasa na vijana wenzake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya mchango ulivyotoka asubuhi, ni kana kwamba Mheshimiwa Nape kazi hii amepewa miaka minne iliyopita na imeshamshinda na hana ubunifu. Aina ya mchango ule unakatisha tamaa, haumpi moyo Mheshimiwa Nape kama inavyostahili. Majukumu haya Mheshimiwa Nape amekabidhiwa takribani siku 160 zilizopita, kwa hiyo, bado kuna muda mrefu wa kufanya kazi na kuonesha ubunifu, na mimi sina shaka yoyote kabisa na uwezo wake wa kufanya kazi hii vizuri. Sikubaliani kabisa na dhana kwamba katika nchi hii mtu anayechukiwa zaidi ni Mheshimiwa Nape Nnauye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilipata bahati, Mheshimiwa Nape aliniomba nimsindikize kwenye Chuo Kikuu cha Dodoma ambapo kulikuwa na shughuli ya vijana; walikuwa wengi takribani 8,000 mpaka 10,000. Alipotambulishwa, nilliyoyaona hayaendani na kauli zinazosema kwamba hapendwi hapa Watanzania. Ushuhuda wa mambo hayo siyo maneno yangu tu, hata record ya shughuli hiyo ipo wazi na ilioneshwa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kuchangia hotuba hii, lakini hasa hasa kuzungumzia hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani hasa ukurasa wa 11. Niseme tu kwamba binafsi huwa naheshimu karibu kila mtu hapa Bungeni na sijawahi kuinua mdomo wangu au kauli yangu pale mtu anapotoa mchango wake. Kwa hiyo, nategemea heshima hiyo iwe accorded kwa Waheshimiwa Wabunge wote, kwamba kila mtu anapopewa nafasi ya kuzungumza, basi angalau kwa Kiingereza wanasema; “decorum.” Kwamba angalau kuwepo na decorum ya kumheshimu mwenzako amalize anachosema na fursa inapopatikana, kama hukubaliani naye, basi unaweza kusema hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 11 wa hotuba, imejengwa dhana hapa kwamba Chama cha Mapinduzi na Serikali ya Chama cha Mapinduzi na Mheshimiwa Rais anabagua wasanii. Katika vitu ambavyo viko mbali na ukweli, hiki ni namba moja. Linalozungumziwa hapa ni kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alialika baadhi ya wasanii na kuwabagua wengine. Kwa hiyo, wenzetu wanasema hicho ni kitendo cha Serikali, cha Rais kuwabagua wasanii ili awatumie kwa ajili ya maslahi ya kisiasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati ya kuandaa hiyo shughuli inayozungumzwa na kushiriki kuiendesha. Katika shughuli ile Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwangu na kwa wenzangu kwamba angependa kutoa shukrani kwa makundi mbalimbali yaliyoshiriki kwenye kampeni ya CCM wakiwemo wasanii walioshiriki katika kampeni ya CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa uchaguzi kulikuwa na wasanii ambao walituunga mkono CCM na kuna wasanii ambao hawakutuunga mkono. Katika shughuli ile walialikwa wasanii, madereva, makundi mbalimbali; vijana wa IT pia walishiriki. Ilikuwa ni shughuli ya Mheshimiwa Rais kutoa shukrani kwa watu walioshiriki katika kampeni yake na kampeni ya CCM. Shughuli ile ya kushukuru watu imeendelea, haikuishia kwa makundi yale ambayo yalialikwa mwezi wa pili ambapo mimi nilishiriki, lakini pia viongozi wa CCM na viongozi wengine na kazi hiyo inaendelea.
Katika shughuli ile, masuala ya maslahi ya wasanii yalizungumzwa kwa mapana yake. Mheshimiwa Rais alielekeza hatua kadhaa za msingi za kuchukua na Mheshimiwa Waziri amezizungumza baadhi ya hatua hizo leo za kusaidia wasanii kujikwamua na changamoto zilizopo. Bahati nzuri sasa katika hatua zilizochukuliwa, katika utekelezaji wake zitawanufaisha wasanii wote waliotuunga mkono na ambao hawakutuunga mkono, walioshiriki shughuli ile na ambao hawakushiriki shughuli ile kwa sababu hatua zile hazibagui mtu, hazibagui wasanii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka nichangie, niweke record sahihi kwamba Mheshimiwa Rais wetu ni Rais wa watu wote na ni Rais wa wasanii wote. Serikali ya CCM ni Serikali ya watu wote, ni Serikali inayowaongoza na kuwaletea maendeleo hata wale ambao hawakutuunga mkono; kwa sababu sisi ndio tumekabidhiwa dhamana ya uongozi wa nchi na dhamana ya kuleta maendeleo ya nchi hii, na kazi hiyo tunaifanya na tutaifanya vizuri; na matokeo ya kazi hiyo yataonekana mwaka 2020 pale ambapo tutaongezeka na tutarudi kwa kishindo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalize tena kukushukuru kwa fursa hii na kwa kumpongeza sana na kumtia moyo ndugu yangu, Mheshimiwa Waziri Nape na timu yake. Sisi tunaokujua vizuri, waswahili wanasema haja ya mja kunena, muungwana ni vitendo. Si haki kuhukumiwa kwa neno moja kukosekana kwenye hotuba wakati kazi unaifanya ya kusukuma soka la nchi hii na sisi wote tunakujua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.