Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa ambazo anazifanya za kuleta fedha za maendeleo kwenye maeneo yote ya nchi yetu. Miongoni mwa walionufaika ni sehemu ya Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Tanganyika tumepata fedha nyingi za maendeleo, kwenye sekta ya elimu, maji, miundombinu na kwenye afya tumeletewa fedha nyingi za maendeleo ambazo zinaonesha kabisa jitihada za Serikali zilizofanywa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, ninawapongeza Watendaji wa Serikali wakisimamiwa na Mawaziri kwa jitihada zao ambazo wamezifanya kusimamia miradi ile ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie mradi wa bandari. Serikali imewekeza mradi mkubwa wa bandari eneo la Kalema ambao una thamani ya Shilingi Bilioni 48. Mradi huu ni mradi mkubwa na una manufaa kwa nchi yetu, kitu ambacho tunaiombe Serikali ni kuhakikisha sasa mradi huu ili uweze kufanya kazi ni lazima Serikali ijenge barabara yenye kilometa 110 kutoka Kagwira kwenda Karema ili ile bandari iweze kufanya kazi kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa DRC Congo wanaitumia fursa hii ya kupatikana kwa bandari ili waweze kuleta mizigo ipitie Bandari ya Karema na hatimaye kufika kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Ninaiomba Serikali iharakishe mchakato wa ujenzi wa barabara hiyo ili iweze kusaidia shughuli za kiuchumi kwenye maeneo hayo, vilevile kuifanya Bandari ya Dar es Salaam kuondoa msongamano uliopo pale eneo la Tunduma pindi utakapokuwa umekamilika mradi huu wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo tunaishukuru Serikali ni miradi ya umeme wa REA ambao mimi kwenye Jimbo langu tuna vijiji 26, kwa bahati nzuri Serikali ilitoa fedha na ikapata Mkandarasi lakini kumekuwa na changamoto kubwa sana Mkandarasi aliyepewa dhamana ya kupeleka umeme vijijini kwa Mkoa wa Katavi ameshindwa kutekeleza mradi ule kwa wakati. Ninaiomba Serikali Wakandarasi wanapopewa kazi wasimamiwe vizuri ili waweze kukamilisha miradi ambayo wameiweka kwa ajili ya kuwafikia wananchi.

Mheshimiwa Spika, ninavyo vijiji 26 ambavyo alipewa huyu mkandarasi lakini mpaka sasa bado hajakamilisha na kila mwaka wanamwongezea muda ili aweze kukamlisha. Ninaomba kwenye eneo hilo Serikali ilifanyie kazi ili mradi huu uweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto kubwa sana mkandarasi aliyepewa dhamana ya kupeleka umeme vijijini kwa Mkoa wa Katavi ameshindwa kutekeleza mradi ule kwa wakati. Niombe Serikali wakandarasi wanapopewa kazi wasimamiwe vizuri ili waweze kukamilisha miradi ambayo wameiweka kwa ajili ya kuwafikia wananchi. Nina vijiji 26 ambavyo alipewa huyu mkandarasi lakini mpaka sasa bado hajakamilisha na kila mwaka wanamwongezea muda ili aweze kukamilisha. Ninaomba kwenye eneo hilo Serikali ilifanyie kazi ili mradi huu uweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ni miradi ya maji. Tunaishukuru Serikali Halmashauri yangu imepata Shilingi Bilioni 8.9 kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali na Serikali imejitahidi kupeleka miradi, iko iliyokamilika na mingine bado ambayo haijakamilika ukiwemo mradi wa eneo la Mishamo wenye thamani ya shilingi bilioni1.3. Shida kubwa ambayo ipo katika eneo hilo ni Mkandarasi aliyepewa hana uwezo wa kwenda kufanya kazi na asilimia kubwa anatafuta fedha apewe fedha kabla hajafanya kazi wala kwenda kwenye eneo la site.

Mheshimiwa Spika, ninaomba Serikali iweze kutoa Mkandarasi mwingine kuliko yule ambaye walimpa na hana uwezo. Mkandarasi huyo anaitwa Hamwa, kazi anayoifanya ni kwenda kufanya lobbying na kutisha watendaji wa Serikali waidhinishe kumpa fedha wakati uwezo wa kufanya kazi haupo.

Mheshimiwa Spika, ipo miradi mingine ya maji katika Vijiji vya Kapalamsenga wenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.3 inaenda vizuri lakini tunaomba Mkandarasi aliyepewa kazi hiyo aweze kuisimamia ikamilike kwa wakati. Kubwa zaidi ambalo tunalihitaji wananchi wa Wilaya ya Tanganyika na Mkoa wa Katavi kwa ujumla kwenye mradi wa maji tuliishauri Serikali kuhakikisha mradi ambao unaweza ukabeba matumaini ya wananchi wa Wilaya ya Tanganyika na Mkoa wa Katavi ni mradi ule mkubwa wa maji kuyatoa Ziwa Tanganyika kuyapeleka Makao Makuu ya Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Spika, najua jitihada za Serikali zimefanywa hatua za awali, tunaomba kwenye bajeti hii waangalie umuhimu wa kuanza ujenzi wa mradi huu mkubwa wa maji ambao utatatua kero ya maji Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ambayo tulikuwa tunaishauri Serikali ni ujenzi wa meli wa Ziwa Tanganyika. Tumejenga Bandari lakini bado vitendeakazi havipo. Ili bandari zilizopo Mkoa wa Kigoma, Katavi na Mkoa wa Rukwa ziweze kufanya kazi tunahitaji kuwa na meli. Meli ambazo zitafanya kazi kwenye Ziwa Tanganyika na ni kitendo cha aibu kwamba katikati ya nchi zilizozunguka Ziwa Tanganyika eneo la nchi yetu tu ndiyo ambayo haina vyombo vya usafiri. Niombe Serikali iweze kufanya mchakato wa haraka ule ambao wameuanzisha wa kuanza kujenga meli kwenye Ziwa Tanganyika tupate meli za mizigo na abiria kwa ajili ya kuwasaidia wananchi. Bila kufanya hivi hata uwekezaji tuliouwekeza kule utakuwa ni sawa na hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili ni muhimu kiuchumi na wenzetu nchi za Burundi, Congo wanaitumia kama fursa na sisi hii fursa tuitumie ambayo itatusaidia sisi na kwa nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ya mchango wangu ni kwenye eneo la kilimo. Tunaishukuru Serikali ilileta mbolea zenye ruzuku ya Serikali kwenye eneo hili. Tunaipongeza sana, lipo jambo ambalo tulikuwa tunaomba na kuishauri Serikali iweze kulifanyia mchakato kwa kiwango kikubwa. Mbolea za ruzuku za Serikali zilizotolewa zimebagua baadhi ya maeneo hawakupewa kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wetu. Wakulima ambao wanatoka Mikoa inayozalisha zao la tumbaku hawajanufaika na ruzuku iliyotolewa na Serikali. Ninaomba kwenye mchakato huu na wao waangaliwe kwa sababu na wao ni sehemu ambayo wananufaika na wana mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, mfuko mmoja unauzwa kati ya shilingi 170,000 na hawa wakulima faida yao inakuwa ndogo sana kwa sababu gharama ya uzalishaji inakuwa kubwa sana. Ninaomba Serikali ilichukue hili na ilifanyie kazi ili iwasaidie wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili kwenye eneo la kilimo juu ya mbolea hizo, tunaomba utaratibu ambao ulifanyika mwaka huu mwakani ufanyiwe maboresho kwa kiwango kikubwa ili iwafikie walaji waliowengi kuliko ilivyokuwa sasa walionufaika ni wachache na pengine unawanufaisha watu wengine ambao ni wafanyabiashara middleman ambao wanatumia hizo huduma zilizotolewa na Serikali kuliko wale walengwa ambao ni wakulima halisi.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuishukuru Serikali kwenye miradi ya afya. Tumeletewa miradi mingi ya afya kwenye Mkoa wa Katavi lakini tatizo kubwa tulilonalo ni watumishi ambao wanahitaji kutoa huduma za afya. Kwenye zahanati, vituo vya afya, hospitali ya Wilaya bado uhitaji mkubwa wa watumishi ni mkubwa kwenye maeneo haya. Mimi binafsi tu kwenye Wilaya yangu nina vituo vya afya ambavyo vimejengwa zaidi ya vitano lakini watumishi tulionao ni wachache, tuna hospitali ya Wilaya ambayo inahitaji huduma kutolewa kwa wananchi, bahati mbaya sana hata vitendeakazi havipo! Kwa hiyo, tunaomba uwekezaji uliowekezwa na Serikali kwenye eneo hili ni vizuri sasa na ni muhimu wakatoa fedha kwa ajili ya kutoa ajira kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)