Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukupongeza wewe binafsi kwa kushika nafasi hiyo ya uwenyekiti na kuweza kuliongoza Bunge letu, na Mwenyezi Mungu aendelee kukuongoza na kukubariki. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kipindi cha mwaka 2023/2024. Taarifa ni nzuri, imesheheni mambo mbalimbali ya maendeleo yaliyotekelezwa na miradi mikubwa ya kimkakati. Vile vile imegusa maeneo mengi katika kuboresha sekta mbalimbali kama vile sekta za elimu, afya, barabara, kilimo na mambo mbalimbali.

Mheshimwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ana maono makubwa pamoja na kuwa na mapenzi makubwa kwa Watanzania, mpenda maendeleo, mzalendo na mwanamapinduzi wa kweli mwenye huruma ya kipekee kabisa, na hatuna mfano wa kumfananisha. Tuendelee kumtakia kila la kheri na kumuombea maisha mema ili Mwenyezi Mungu aendelee kumuongoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba nizungumzie suala la kilimo. Niipongeze Serikali kwa kuendelea kuiimarisha sekta ya kilimo. Tumeona namna mbalimbali ambavyo inaendelea kuimarisha kwa kuifanya Benki ya Kilimo kuendelea kukua na kuendelea kuwahudumia wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona namna ambavyo Serikali inaendelea kutoa ruzuku. Si hivyo tu, bado tumeendelea kuona namna ambavyo wanapata mafunzo mbalimbali ya kufanya kilimo chetu kiwe kilimo cha biashara na kuendelea kupata masoko kupitia mitandao mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo bado tuna changamoto katika eneo la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mikoa yetu ya Kusini, sisi wana Kusini zao letu kubwa ni zao la korosho, na ni zao la biashara, ni zao ambalo linatufanya wananchi tuweze kuishi na tuweze kumudu kuendesha maisha yetu. Kwa hiyo panapotokea changamoto ya kutetereka zao la korosho hata kidogo tunapata shida kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo tumeona kwamba bei ya korosho inazidi kuporomoka. Hii ni changamoto kubwa sana kwa wakulima ukizingatia kwamba zao hili unapozalisha, unapolihudumia mpaka kufikia hatua ya kupeleka sokoni pana njia ndefu na mchakato ni mrefu sana. Sasa, mkulima anategemea anapopeleka sokoni anaweza kupata bei nzuri ya kuweza kurudisha gharama ambazo ameweka katika kuhakikisha kwamba anazalisha korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Serikali ilitazame suala hili la bei ya korosho na tuhakikishe kwamba tunawatia nguvu wakulima ili waendelee kuwa na moyo wa kulisimamia zao hili la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa pembejeo Kanda ya Kusini tuna msimu wa kalenda ya upuliziaji (Sulphur) kwenye mikorosho. Sasa, kanda ya kusini hatulingani na kanda nyingine. Tunaiomba Serikali kutuletea pembejeo kuendana na kalenda yetu ya kilimo cha korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile bado tuna hoja ya usajiri wa wakulima wetu. Tunajua kwamba Serikali inaendelea kusimamia usajiri wa wakulima ili kuwabaini wakulima wa korosho waweze kupata huduma nzuri kutoka Serikalini na kuwabaini na kujua idadi ya mikorosho ambayo ipo katika maeneo ambayo tunalima korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mohamed Bashe, Waziri wa Kilimo kwa kuja na Mpango wa Jenga Kesho Ijayo Iliyo Bora. Mpango huu wa kuwashirikisha vijana kuingia katika sekta ya kilimo, kuwafanya vijana waweze kupata mafunzo na kupata mitaji ili kuingia katika uzalishaji wa shughuli za kilimo ni mpango mzuri. Si hivyo tu, pia kuwafanya vijana hawa kuwasimamia na kupata masoko ya mazao ambayo wanayalima.

Mheshimiwa Mwenyekiti huu ni mpango mzuri kwa sababu unatuongezea ajira kubwa kwa vijana kwa sababu kumekuwa na changamoto kubwa sana ya ajira nchini. kwa hiyo mpango huu ni mzuri, lakini pia utakuza uchumi wetu kupitia shughuli zakilimo kwa vijana wetu. Tumeanza vizuri ingawa zipo changamoto ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kwa kuwa mpango huu ndiyo unaanza, tuutakie kila la kheri, Mungu aubariki uende salama na vijana wetu waweze kufanikiwa. Mwaka kesho tutakapokuja basi tuhakikishe kwamba katika maeneo yetu walau tutoe uwiano wa vijana wanaotoka katika majimbo yetu. Kwa mfano mwaka huu katika jimbo langu ametoka kijana mmoja tu, lakini ukiangalia katika majimbo mengine utakuta kuna vijana sita hadi nane katika jimbo moja. Kwa hiyo mwakani tuhakikishe kwamba tunaingia katika uwiano ambao walau kidogo unafananafanana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu nishati. Tunaishukuru Serikali, kwamba inaendelea kusimamia na kuimarisha sekta ya nishati. Zipo changamoto ndogondgo ambazo zinaendelea, lakini Serikali bado inaendelea kuzisimamia kuhakikisha kwamba Watanzania tunapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna matumizi ya gesi nyumbani. Sisi pale Lindi Manispaa tulianza na mpango huu katika Kata ya Mnazi Mmoja, na Serikali imeweka miundombinu ya matumizi ya gesi nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tunatamani sasa kufanya matumizi ya gesi nyumbani na kuondokana na matumizi ya mkaa na kuni, lakini bado tuna changamoto. Changamoto iliyopo ni kwamba vifaa vya matumizi, majiko, pasi na vifaa vingine ambavyo vinatumika nyumbani vimekuwa vya gharama kubwa. Niiombe sana Serikali kuhakikisha kwamba vinapunguza kodi ili Watanzania walio wengi waweze kumudu kununua majiko ya gesi na umeme ili tuondokane na matumizi ya kuni na mkaa. Hii itaweza kutusaidia katika kuhakikisha kwamba tunatunza mazingira yetu, lakini pia itatusaidia kuona kwamba wanawake ndio watumiaji wakubwa wa majiko haya. Tuta-solve muda mwingi wa kukaa jikono na badala yake tutakwenda kufanya shuhguli mbalimbali za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaomba tuhakikishe kwamba kodi inapungua katika vifaa hivi na kuwafanya watu wengi waweze kutumia gesi nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nuzungumzie suala la Mradi wa LNG. Tunashukuru kwa hatua mbalimbali ambazo tumeenda nazo, na tunamshukuru Mheshimiwa Rais alitoa idhini ya kusaini mkataba wa awamu ya kwanza, na walituambia kwamba mkataba wa pili utasainiwa mwezi wa 12, lakini leo tunapoongea ni mwezi wa nne. Hatujui kuna changamoto gani zilizojitokeza zilizosababisha mkataba huu uwe haujasainiwa awamu ya pili. Wana Lindi na Watanzania wanatamani kusikia changamoto ni nini na awamu ya pili ya kusaini mkataba huu itakuwa ni lini ili tuelekee kwenye utekelezaji wa mradi huu wa LNG.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunayo changamoto kwa wazalishaji wa chumvi. Sisi tunaoishi ukanda wa bahari tunazalisha chumvi, lakini wazalishaji wetu wa chumvi wanapata changamoto ya masoko na bei kuporomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba tumefungua fursa za uwekezaji nchini, na tumetoa leseni kwa Mwekezaji mkubwa wa kuweka kiwanda cha chumvi nchini, kwa maana ya kwamba atusaidie kununua chumvi iliyopo ndani ya nchi yetu. Hata hivyo, matokeo yake mwekezaji yule ananunua chumvi nyingi kutoka nje na chumvi yetu ya Tanzania inaendelea kukaa. Kwa hiyo hii ni changamoto kubwa. Kama tatizo ni kwamba chuvi yetu haina ubora ule unaotakiwa ni vizuri mwekezaji akaja kutufundisha ni chumvi ya aina gani yeye anaitaka ili Watanzania waweze kuzalisha na kupata soko la chumvi. Hili ni jambo muhimu, tulisimamie na kulizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Wenyeviti wetu wa Serikali za Mitaa; wenyeviti hawa wanatufanyia kazi nzuri sana. Hata hivyo wenyeviti hawa hatuwapi nafasi yoyote ya kuwanunulia vifaa; vifaa wananunua wenyewe lakini kazi zetu wanatufanyia. Inafika wakati wenyeviti hawapati posho yao. Sasa tujue, kupata posho yao ni halali ama si halali? Na kwa nini hawapati posho zao. Tutafute namna ya kutatua changamoto hii tuliyonayo, hasa kule kwetu Lindi Manispaa, wenyeviti wana miezi 16 hawajapata posho zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo miradi ya TACTIC, na sisi Lindi Manispaa tumeingia katika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, nakupa sekunde 30 umalizie.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Mambo mengine nitaandika kwa maandishi ili Serikali iweze kutusaidia mambo kadhaa ambayo tunayahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja, ahsante sana.