Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa ruhusa nami niwe mchangiaji wa mwisho siku hii ambayo na wewe umekaa kwenye Kiti hicho kwa mara ya kwanza, kama Mwenyekiti wangu wa Kamati ya Bajeti ninakupongeza sana kwa nafasi hiyo, nina imani kubwa na wewe kwamba utafanya vizuri na tunakutakia kila la kheri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo niende moja kwa moja kwenye mchango wangu. Mosi, nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri sana anazozifanya kwenye taifa letu ikiwemo Jimbo langu la Ludewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku Mheshimiwa Rais anapokea ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali alitaja mashirika ambyo yanamkera likiwemo Shirika la NDC. Wakati ametaja Shirika hili la NDC wananchi wa Ludewa walifurahi sana na walishangilia sana na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa sababu NDC wamechukua vitalu Ludewa miaka mingi sana vya makaa ya mawe, chuma lakini hakuna ambacho kinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ninamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kumteua huyu Mkurugenzi wa sasa kwa kweli anajitihada kubwa sana, naamini akimpa muda Dkt. Nicholaus atafanya mambo yale yaende kwenye vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliambiwa na watu wa NDC kwamba mwezi Oktoba wananchi wale wa Mchuchuma na Liganga wangeweza kulipwa fidia yao ya shilingi bilioni 15. Tunawashukuru walikwenda walihakiki wananchi wote, lakini Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa alikwenda pale, Mheshimiwa Antony Mtaka nami nikiwepo akawahakikishia wananchi kwamba fidia zinalipwa mwezi Oktoba, bahati mbaya uhakiki umekamilika bado mpaka leo tunaenda Aprili ile fidia ilikuwa bado haijalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi wananchi walikusanyika vikundi vikundi na kuanza kuhangaika kutaka kutafuta Waandishi wa Habari waweze kufikisha hisia zao kwa Mheshimiwa Rais kuonesha kwamba agizo lake halijatekelezwa la kuwalipa fidia wale wananchi wa Liganga na Mchuchuma. Katika ile taharuki bahati nzuri waliponipigia simu nami nilikwenda Wizara ya Fedha kufuatilia, nikabaini kwamba kibali cha kulipa ile fidia kilishatoka. Mheshimiwa Rais alitoa kibali kilitoka mwezi ule ambapo Mkuu wa Mkoa alikwenda kutoa ile ahadi kwa wananchi, bahati mbaya tu hapa katikati kuna vitu vingine ambavyo wale Wasaidizi ambao wanaikwamisha hata NDC ionekane ni taasisi ambayo haina uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha, jana nilivyofuatilia pale Hazina nikaona kwamba ile exchequer leo ndiyo ilikuwa inatoka ili baada tu ya sikukuu wananchi wale waweze kwenda kulipwa fidia. Kwa hiyo, niliweza kuwashawishi wale wananchi kwamba waniamini na kitendo cha Mheshimiwa Waziri wa Fedha kukamilisha ile exchequer siku ya leo, naamini baada ya sikukuu hii wananchi wale watakwenda kulipwa fidia na atakuwa ametuondolea aibu mimi na Mkuu wangu wa Mkoa ambao tulikwenda kuwahakikishia wale wananchi kwamba fidia watalipwa lakini mpaka leo miezi karibia minne, mitano imepita bila kulipwa fidia. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kusimamia jambo hili tuweze kuhitimisha fidia za wananchi hawa ambazo wamezisubiri toka 2015 na tuende mbele, mpaka sasa makaa ya mawe yana soko kubwa sana duniani kwa wafanyabiashara ambao wataweza kusafirisha makaa ya mawe waweze kuongeza Pato la Taifa na uchumi wa Wilaya yetu ya Ludewa uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru pia Mkurugenzi wa NDC kwa kukubali ushauri wetu tulioutoa kwamba vile vitalu walivyovihodhi kwa muda mrefu wafanye apportionment, wavigawe katika vipande vidogovidogo, wavitangaze, waweze kukaribisha wawekezaji wengi zaidi waweze kuchimba mkaa na kuuza sasa hivi ambapo una thamani kubwa duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri ule ameufanyia kazi na wamekwenda kugawa vitalu vile, tunawaomba sana katika kugawa vile vitalu wasiangalie tu matajiri wengine wa maeneo ya nje ya Mkoa wa Njombe, waangalie pia wale wachimbaji wadogo ambao wako maeneo yale ili nao waweze kushiriki kwenye uchumi. Waangalie Halmashauri iweze kushiriki uchumi huu na wawekezaji wengine wa ndani ya Mkoa. Namna hii itawezesha wananchi wale waweze katika kushiriki katika uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ikiwezekana hawa wachimbaji wanavyokwenda haya maeneo mengine ya sasa, waweze kuwaruhusu wananchi wale wakilipwa fidia waweze kununua hisa kwenye haya makampuni ili nao waweze kupata manufaa yatakayodumu vizazi na vizazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na uwekezaji huu wa Liganga na Mchuchuma kuna ile reli inayotoka Mtwara mpaka Mbamba Bay na tawi lake Mchuchuma na Liganga. Kuna wawekezaji ambao wanataka kujenga kwa mfumo wa PPP. Niliwasiliana na Ndugu Kafulila, Mkurugenzi wa PPP anaendelea nao kuwasikiliza. Kwa hiyo, ninaomba sana ikionekana wanao uwezo wa kujenga ile reli waweze kupewa nafasi hiyo ili waijenge na iweze kubadilisha kabisa uchumi wa ukanda huu wa Kusini miaka na miaka na kuongeza Pato la Taifa. Itatupunguzia hata kwenda kutegemea mikopo ambayo mingine ina masharti yasiyo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli hii ikikamilika inaweza kuchangamsha hata shughuli zingine za kiuchumi. Sambamba na hili nilikuwa nazungumza na Waziri wa Ujenzi. Changamoto kubwa ya makaa ya mawe kule yaliko mpaka kwenye Bandari ya Mtwara, kuna changamoto kubwa ya logistics, usafirishaji kuyatoa pale mpaka kufikisha bandarini. Kwa hiyo, ni muhimu sana reli hii ikajengwa ili iweze kusafirisha malighafi za chuma na makaa ya mawe mpaka bandarini na kwenda mpaka kwenye masoko ya Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili kutoka pale Ludewa kuna daraja moja ambalo lipo Kata ya Ibumi linaunganisha Wilaya ya Mbinga na Wilaya ya Ludewa. Daraja hili likijengwa itakuwa ni njia nzuri na ya mkato ya kuweza kupeleka makaa ya mawe bandarini Mtwara kuliko wakizunguka kilometa nyingi gharama za usafiri zitakuwa zimeongezeka sana. Kwa hiyo, naomba sana daraja hili liweze kujengwa ili lirahisishe usafirishaji wa makaa ya mawe vilevile shughuli za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili lina ekari ambazo Halmashauri wamezitenga 3,500 ambazo zinafaa sana kwa kilimo cha umwagiliaji, kwa hiyo daraja hili likijengwa litarahisisha sana hata ajira kwa vijana katika sekta ya kilimo, mfumo ambao Waziri wa Kilimo ameuanzisha wa BBT ni mfumo mzuri sana ambao utapunguza kero ya ajira. Tutafute sasa mfuko maalum ambao utaweza kuwakopesha vijana fedha wale wanaotoka JKT na wale wanaomaliza vyuo vikuu hasa vya kilimo na vyuo vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasoma ripoti ya Mkaguzi inaonesha kwamba kuna Halmashauri 106 zilikuwa na Idara na Vitengo ambavyo vinaongozwa na watumishi 747 wasio na sifa. Wabunge wengine wamezungumzia hapa kwamba kuna tatizo kubwa sana la ajira, ninaamini Wabunge wengi wana vijana na wazazi wao kutoka kule Majimboni wanatutumia message kila siku na kutupigia simu. Kwa hiyo, naomba vilevile hizi nafasi za ajira ambazo zinaonekana zina matatizo ziweze kufanyiwa uchambuzi na kutangazwa. Kule wazazi wamesomesha vijana wao wako kijijini hawana shughuli. Kwa hiyo, maeneo kama haya ya miradi ya kilimo cha umwagiliaji wakipewa mikopo vijana wale wanaomaliza Chuo Kikuu cha Sokoine (SUA) wanaweza wakatengeneza ajira na wakalisha hata nchi hii kwa kutumia haya maeneo ambayo yanafaa kwa kilimo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingineā€¦

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha naomba umalizie.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia. Kwa hiyo, baada ya kusema hayo machache kwa sababu nitapata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara nyingine ninashukuru sana kwa kunipa nafasi naunga mkono hoja. (Makofi)