Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia bajeti ya mwaka 2023/2024.

Kwanza nianze kutoa pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambazo anazifanya za kimaendeleo katika nchi yetu, lakini katika kuhakiisha kwamba anaendelea kupambana bila kulala, bila kuchoka, kuhakikisha anaendelea kutatua changamoto kubwa ya ajira tuliyokuwanayo vijana wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa zaidi ya Shilingi bilioni 39.8 kwenye Kiwanda cha Mkulazi, Kiwanda cha Sukari Morogoro ambacho mpaka sasa hivi kimeshaajiri takribani zaidi ya vijana 154 wa Kitanzania wako kazini. Mpaka sasa hivi zaidi ya hekta 2,900 zimeshaweza kufanyiwa kazi. Tunatarajia ndani ya mwaka mmoja zaidi ya tani 50,000 zitaweza kuzalishwa na hivyo itakuza mnyororo wa thamani ya uchumi kwa maana ya kuanzia ndani ya nchi yetu kuondoa tatizo la sukari, lakini pia baada ya kukidhi soko la ndani tunaweza kupeleka na soko la nje na hivyo kuliongezea Taifa letu mapato.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuchukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na Wizara ya Kilimo kwa ubunifu wa skimu za umwagiliaji ambao tunaamini utaenda kutatua tatizo kubwa sana; kwanza la ajira; na pili, utaenda kukuza uchumi wa nchi yetu kwa sababu ni kilimo ambacho kitakuwa ni cha muda wote na kitaendeleza mnyororo wa thamani. Naishukuru sana Wizara ya Kilimo, lakini niiombe sasa, kwa jitihada hizo ambazo imeanza kuzifanya, basi ni vyema wakashirikiana na watu wa JKT kwa maana ya kuwatumia vijana walioko makambini kwa mfano, kambi yetu ya Makutupora, kwenye kilimo cha alizeti; Kambi ya Chita kwa maana ya kilimo cha mpunga na maeneo mengine kadha wa kadha. Kwa sababu tayari tuna nguvukazi ya Taifa hili ambayo ipo na yenye maadili makubwa na inaendelea kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaweza tukawasaidia vijana hawa kupitia JKT ili kuendelea kuhakikisha nchi yetu ya Tanzania kupitia kilimo kama ambavyo Waziri ameweza kuweka mipango thabiti ya kilimo cha umwagiliaji, basi tunaunganisha nguvu ili kuweza kukidhi soko la ndani, lakini kuendelea kufanya mazingira rafiki kwa vijana wa Kitanzania kuona tija ya kilimo na baadaye kuweza kukopesheka ili wao wenyewe wawe ni sehemu ya mitaji na sehemu ya uzalishaji kwa maana ya wao binafsi, kwa kuwa tayari Wizara imeshaonesha wapi tunaelekea? Wapi tunakwenda? Kilimo Tanzania chenye tija kinawezekana. Hongera sana Mheshimiwa Rais, hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuendelea kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha anaendelea kuwakwamua wananchi wake na hasa kupitia kilimo, na viwanda. Mheshimiwa Rais kupitia watu wa Poland waliweza kuingia makubaliano na Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Maendeleo la NDC na kuleta matrekta ndani ya nchi yetu ya Tanzania, matrekta yaliyoletwa na Kampuni ya Ursus ambayo yaliweza kukopeshwa kwa wakulima wetu hapa nchini kwa maeneo tofauti tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe masikitoko yangu kwa niaba ya wananchi, wakulima ambao waliweza kupokea matrekta hayo. Matrekta hayo yalivyoingia ndani ya nchi yetu, kwanza wakulima ambao walikuwa na sifa hizo za kupokea walitakiwa waende kuchukua matrekta hayo kwa usafiri. Maana yake wasiyatembeze mpaka maeneo wanapofika, bali watafute fedha waende wakachukue matrekta hayo.

Mheshimiwa Spika, wananchi walikopa, waliuza vitu vyao, wakasafiri wakaenda kubeba matrekta hayo na kuyapeleka site. Wananchi wamefika na matrekta hayo, na kwenye mkataba walikubaliana miaka miwili wataendelea kupewa huduma ya vipuri, lakini matrekta hayo yamefika kwa wakulima, na ndani ya nchi hakuna vipuri. Mkataba umekiukwa kwa sababu hawakuletewa vipuri hivyo ndani ya nchi yetu. Nini ambacho kimetokea?

Mheshimiwa Spika, kilichotokea ni umasikini mkubwa kwa wakulima wetu ambao walikopa fedha zao, badala ya kuwekeza kwenye msimu ambao siku zote wamezoea kulima kwa kawaida, walijiwekeza wakaenda kuchukua matrekta hayo. Matrekta yamefika shambani, hayana vifaa, yameharibika. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Asia Halamga, kuna Taarifa ya kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam Hamis Mwagao.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa msemaji wa taarifa hii ya haya matrekta ya Ursus. Matrekta haya yakiingia shambani linakatika vipande viwili. Hatujui aliyekwenda kuyanunua haya matrekta. Kwa hiyo, tunaomba iundwe Tume ya Bunge kwenda kuchunguza mradi huu wa haya matrekta kutia watu umasikini. Watanzania wakulima masikini wamekwenda kufilisika. Ahsante sana. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

SPIKA: Nachelea kumuuliza mchangiaji kwa sababu imetajwa hapo kampuni mahususi na tusije tukaingia kwenye mgogoro wa kibiashara hapo. Hoja ya Mheshimiwa Asia Halamga sikuiingilia kwa sababu inahusu vipuri vya hayo matrekta ambayo yametajwa jina, lakini sasa ule udhaifu wa hayo matrekta anaouonesha Mheshimiwa Tabasam, nisingependa Bunge lijielekeze huko kwa sababu, sina taarifa. Tusije tukaingia kwenye mgogoro wa kibiashara kwamba, mtu anaharibiwa biashara yake.

Kwa muktadha huo, Mheshimiwa Tabasam, hilo eneo la kuonesha udhaifu wa hayo matrekta kwa sababu ya hoja hiyo ya kibiashara isije ikatuletea changamoto hapa, maana mimi sina hiyo taarifa, inaondolewa kwenye Taarifa Rasmi za Bunge.

Mheshimiwa Asia Halamga, malizia mchango wako.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba tu sasa kwa sababu watu hawana ufafanuzi mzuri juu ya matrekta haya, niendelee tu kuchangia kwa kusema kwamba matrekta haya wakulima wetu, kwanza wakati wanakwenda kuyachukua walitakiwa waingize fedha kwenye akaunti ya mtu binafsi ambaye alikuwa anasimamia. Wananchi wakaingiza fedha kwenye akaunti hiyo ya mtu binafsi, lakini matrekta nje ya mkataba ule ambao wamekubaliana kwamba walete vipuri na vipuri havikuja, wananchi sasa hivi wameanza kukamatwa.

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi, wananchi walianza kuitwa na watu wa TAKUKURU na walikuwa wanafanya bargaining. Baada ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kupitia Ripoti ya CAG ambapo alipoongelea masuala ya TAKUKURU kutokuingilia masuala haya ya fine na kadhalika, wakaweza kusimama, lakini watu hawa NDC wakaamua kutumia watu wa Majembe Auction. Watu wa Majembe Auction wanakwenda kuwakamata wakulima na bahati mbaya sana wakiwapigia simu wanaanza ku-bargain nao kwamba umelipa lini?

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wakulima wamepewa akaunti nyingine ambayo wanatakiwa walipie sasa rasmi hiyo fedha, lakini fedha ya mwanzo ambayo wameitoa na kuweza kupata matrekta kipindi cha mwanzo, fedha ile haitambuliki.

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, wananchi hawa wamekosa jukwaa, kwanza la shirika lenyewe kwa sababu wametafuta nafasi mra kwa mara waweze kuongea nao kwa sababu tayari wako nje na mkataba, hawajapata nafasi ya kukaa nao. Haitoshi, wananchi hawa ambao ni wakulima wameshakuja mara kadhaa Dodoma bila mafanikio ya kukutana na viongozi wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi hawa wameandika barua hii hapa na ilikwenda kwa Wizara ya Viwanda na Biashara, wananchi hawa hawajaweza kupata majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi natokea Wilaya ya Hanang. Ukifika Wilaya ya Hanang unakutana na wamama ambao wamekimbiwa na waume zao kwa sababu wanaenda kukamatwa na Majembe Auction kule chini. Wamama hawa wameshindwa kuwapeleka watoto shule…

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Nani amesimama kuhusu taarifa?

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, niko huku.

SPIKA: Aah, Mheshimiwa Flatei.

T A A R I F A

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe Taarifa mzungumzaji. Pamoja na kutokuwa na vipuri ndani ya nchi, wanaenda kuchukua vipuri hivyo nje ya nchi. Pia Jimbo la Mbulu Vijijini kuna tatizo kama hilo hilo na taarifa hii ni ya kweli.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Huyo alikuwa anachangia, lakini muda wako umekwisha Mheshimiwa Asia Halamga; nakupa dakika moja umalizie hoja yako.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, nakuomba dada yangu uniongezee muda hata wa dakika mbili niweze kumalizia.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya kumalizia na kwa sababu ya tija katika Taifa letu dhidi ya makampuni ambayo yanaweza kuleta vifaa ndani ya nchi yetu na kwenda kuwatia watu wetu umaskini na ambaye anapata doa siyo mtu wa nje, anayepata doa ni Serikali ya Tanzania wakati Mheshimiwa Rais ameamua kuwasaidia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pendekezo langu la kwanza ninaiomba Serikali kwanza ikubali kukaa na hawa wakulima ili iweze kujua changamoto zao ni zipi ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili; ninaiomba Serikali iweze kuangalia kampuni hii kama ina tija au kama haina tija kwa sababu zoezi lenyewe lina tija kwa wakulima, ninaomba iwezekane kampuni ibadiliswe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia; suala la ushoga. Niombe, wasanii wetu ndani ya Nchi yetu ya Tanzania na kupitia BASATA. BASATA wimbo ukiingia doa kidogo la kama tusi au maadili hapohapo wanafungia wimbo, watoto wa kike wakivaa vimina hapohapo wanafungiwa wimbo.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna tija gani ya watoto wetu wa kiume kuvaa mawigi, maziwa au makalio ili kuonesha sanaa? Kwani hakuna njia nyingine ya wasanii wa kiume wa Tanzania kuweza kupeleka ujumbe bila kuvaa mavazi ya kike? Wanavaa mawigi, wanapaka poda, wanapaka wanja; wanafundisha nini wakati wao ni kioo cha jamii kwa watoto ambao wanachipukia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)