Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu ambayo ina page 95, imegusa maeneo mengi.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza napenda nianze kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa mambo anayonipa ushirikiano kwenye Jimbo langu la Mbogwe na ikumbukwe tu tarehe 8 Aprili, nimefanya Mkutano pale Kata ya Ilolangulu Kijiji cha Nyashinge, nimepokea malalamiko mengi ya wananchi yanayoishutumu Serikali. Hata hivyo, nimpongeze Rais maana amekuwa ni Rais wa mfano katika Jimbo la Mbogwe. Mbogwe ilikuwa haijawahi kutengenezewa lami, lakini kwa awamu yake tumepokea lami kilomita tano. Mheshimiwa Rais ametu-balance hata kwenye upande wa maji japokuwa kuna maeneo mengine bado hayajaguswa, nizidi kumwombea kwa Mwenyezi Mungu Mama yangu aendelee kuwa na moyo wa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametupatia miradi ya umeme pamoja na mambo mengi luluki. Wananchi wangu walikuwa na njaa ya kufa mtu, niishukuru Wizara ya Kilimo nilikuwa nikilia wananisaidia, Mheshimiwa Bashe Mungu amlinde sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya shukurani hizo, sasa uniruhusu kidogo nijaribu kuingia kwenye ilani yetu ambayo ni mkataba wetu na wananchi waliotuchagua.

Mheshimiwa Spika, neno la Mungu linasema “watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa”. Hapo nipo kwenye maandiko kwanza bado sijaingia kwenye ilani. Ukisoma ukurasa wa 52, unaelezea bayana kwamba wananchi tuliwaahidi nini? Wizara ya Ardhi tulipanga kwamba tutatenga hekari milioni sita kwa ajili wananchi kuchungia ng’ombe pamoja na kilimo. Leo naweza nikasema kwamba haya maswali yanaulizwa sana na wananchi. Ni wapi ambapo tumetenga hasa eneo langu la Mbogwe? Kwa vile Mawaziri wapo sasa wawe makini ili waweze kunijibu huko mwishoni na uzuri Waziri wa Maliasili anakuja kuingia ajipange sasa kuja kunijibu kama anavyonifahamu kaka yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mbogwe wanapata tabu kwenye mapori. Sheria zinasema mita mia tano, ukisogea mita mia tano ng’ombe wanataifishwa, lakini hapa tuliwaahidi wananchi kwamba tutawatengenezea maeneo na wanifundishe sasa kwa vile hili suala liko kiilani halafu mpaka sasa hivi bado hawajatenga maeneo wananitakia nini mimi Mbogwe?

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nigusie kidogo sheria zetu ambazo tumezipitisha hapa Bungeni, zimekuwa zikileta mkanganyiko mwingi kwa wananchi. Lazima Serikali tuishauri vizuri. Ukiangalia Sheria za Madini zinasema mtu anaweza akaomba kwenye mtandao akapatiwa leseni hata kama kuna nyumba. Suala hili kwa vile yananitokea na ninayaishi, yameleta mkanganyiko mkubwa sana kwa wananchi wa Mbogwe. Ukiangalia Kata ya Kanegele migogoro ni mingi Bukandwe pamoja na Masumbwe, wananchi wamekuwa wakilia sana. Mbaya zaidi hawa wawekezaji pale wanapozipokea hizi leseni hawasomi Sheria zinasemaje. Wanaingia na Mapolisi, wanafukuza watu, hawalipi fidia, wanajali masilahi yao, matokeo yake hii nchi inakuwa kama vile imepoteza mwelekeo.

Mheshimiwa Spika, tukikumbuka enzi za Mwalimu Nyerere aliishi vizuri na watu, aliwasikiliza wanyonge. Tunatambua sera yetu ni kukaribisha wawekezaji, lazima tufikirie hawa wawekezaji wanaoingia ni wazuri kwetu au ndio watatutoa madarakani? Tatizo hili hata Chunya, Mbeya lipo, maeneo yote yaliyozungukwa na migodi yanasumbua watu sana. Nikuombe wewe ni bosi wetu hapa Bungeni, utoe maelekezo ikiwezekana kuanzia kwenye Kamati zetu ili tuziangalie upya. Hii sheria inakinzana sana na wananchi wanyonge wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine niongezee hapohapo na Mawaziri, tuna Baraza la Mawaziri 24 lazima tuangalie vizuri, hawa Mawaziri wanamsaidia kweli Mama hawa?

Lazima tuwaangalie hawa Mawaziri 24, wanamsaidia Mama au wanaendesha V8 halafu wanakalia kusema Mama anaupiga mwingi? Wananchi wa kawaida waliumia sana juzi wakati Mama anakabidhiwa ripoti ya CAG, kauli aliyoitumia ni lugha ya Kiingereza, alisema stupid! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais ni mtu mkubwa sana kufikia kusema neno pumbavu na mtupishe wakati kuna watu wake wanaomsaidia, ina maana wao hawaoni matatizo haya, hata kama matatizo haya yanafanywa na wataalam. Kwa nini Mawaziri wasichukue hatua mapema? Mwishowe hili suala mbona linatugharimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaombe Mawaziri, sina bifu na ninyi na wala sijaja kutafuta ugomvi hapa, hebu kila mmoja ajitathmini kwenye nafasi yake anamsaidiaje Mama hasa anapoenda Ikulu kukaa naye? Nikiangalia Wizara zipo 24 mpaka na Naibu Mawaziri hawa watu wanatumia kodi za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuingiza suala la maridhiano kwamba vyama sasa tuanze mchakamchaka sasa ndiyo tutajuana sasa mwaka 2025 ni nani Mwanamme na Mwanamke ni nani? Maandamano yameruhusiwa itafika sehemu tuchoke kuwashauri hapa Waheshimiwa Mawaziri hamchukui hatua, kitakachofuatia sisi ni kuandamana na wananchi kuja kwenye familia zenu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, siwezi nikakubali kukalisha wananchi fedha zimeliwa na watu wanajulikana!

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, taarifa!

TAARIFA

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba mwaka 2025 au 2030 tutakutana watu wenye sifa na siyo habari ya mwanamke na mwanaume, kusema kwamba nani atakuwa mwanaume na mwanamke ni kudhalilisha wanawake ambao wanafanya kazi nzuri na njema, saa nyingine kuliko hata wanaume. Haya ni masuala ya ushindani wa vigezo siyo masuala ya ‘ME’ na ‘KE’, afute hiyo aliyoisema.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri kwa sababu umemtaka afute hiyo kauli yake. Kwanza hatupiti kwenye Kanuni ya Taarifa kama unataka mtu afute kauli. Pia mimi nilikuwa nafuatilia mchango wake anaelekea wapi kwa sababu niliyekaa hapa mbele ni mwanamke na aliyekuwa anamsifia pia ni Rais ambaye ni mwanamke. Kwa hiyo, nilikuwa naangalia hoja yake. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, nilikuwa naisikiliza hoja yake niielewe halafu ndiyo nijue yale maneno yake yametumika isivyo ama yako sawasawa. Kwa hiyo, kwa kuwa umeomba kuhusu kufuta wacha nimruhusu aendelee na hoja yake kama kutakuwa na hiyo sababu baada ya kueleweka hoja yake, kwa sababu anaendelea kuzungumza tutajua kama anatakiwa kufuta au hapana. Endelea Mheshimiwa Maganga. (Makofi)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakushukuru kwa kunipa nafasi nilindie na muda wangu ili kusudi niweze niweze kuwasilisha mchango wangu vizuri na sikuwa na maana mbaya kwamba nani mwanaume na mwanamke atajulikana maana yake ni nani mchapakazi ambaye anastahili kuaminiwa na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tumlinde Rais wetu kwa wivu na nguvu zote, tumekuwa na Naibu Mawaziri tukiwapigia hata simu Wabunge hawapokei, tunawandikia meseji ili washughulikie matatizo ya wananchi hawatujibu. Tunatambua Wizara zipo 24 ambapo mimi Mbunge kwa nafasi yangu ni kuchukua changamoto na kuipeleka mahala husika, ndiyo maana nasema hizi Wizara ziangaliwe upya, mpaka nafika sehemu mbali sana mimi kufikiria hivi! Hivi hawa kwanza waliteuliwaje yaani mpaka nachanganyikiwa nashindwa kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia Wizara ya Afya madawa hakuna kwenye vituo vya afya, kilio kila mahala, pale Masumbwe nina kituo kikubwa sana akina Mama wengi wanahangaika. Naishukuru Serikali ilileta vifaatiba lakini mpaka leo havijaanza kufanya kazi, Mawaziri wapo hawahawa wanabadilishwa mara yupo Ustawi wa Jamii mara Maendeleo ya Jamii lakini hawafanyi kazi kiukweli, lazima tushauriane vizuri, najua ni chungu itawauma lakini ukweli lazima tuuseme. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la mikataba. Kwenye suala la mikataba najua kuna Waziri wa Mikataba hapo kuwa makini uje unijibu. Ile Halmashauri ya Mbogwe imeanza kujengwa toka mwaka 2016, Halmashauri ya Mbogwe mpaka leo ni mwaka wa Saba bado haijaisha, Mkandarasi alishakula fedha, Halmashauri tulishaazimia kwamba tupewe hata Mkandarasi mwingine, mpaka sasa hivi Milioni 700 zipo zimekaa tu kwenye account, mikataba haieleweki! Nakuomba utusaidie Mbogwe tuko busy kwanza tulishacheleweshwa zamani mno, ndiyo tumepata kafursa ka huyu Mama anatusaidia na anatusikiliza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, vilevile kingine, ninyi Mawaziri ni marafiki zangu lakini inakuja suala la wananchi mimi sina urafiki. Upande wa Jeshi la Polisi Mbogwe ni Mji mkubwa Askari hawajulikani wanalala wapi? Gari la zimamoto hakuna, nyumba zimejengwa nzuri nyingine zinaungua, kila siku ninauliza maswali humu mnashughulikia mtaleta, hakuna kuona kitu kinatekelezeka. Naomba Waziri kwa vile hii hotuba ya Waziri Mkuu imegusa vitu vyote na wewe ujipange unanisaidiaje Mbogwe ili kusudi niendelee kuwa Mbunge mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla hatujaanza mikutano mwaka kesho niwaombe sana Mawaziri wengi nimewataja, kuna Waziri wa Biashara, kuna Waziri sijui wa Mifugo, kuna Waziri wa Kilimo mbolea na zenyewe ilikuwa shughuli, tulikuwa tunamaliza mikutano kisera vilevile kuna Waziri wa Habari na Mawasiliano mitandao ina-scratch kila wakati lakini inaonekana kwenye maeneo mengine, Waziri wa Nishati na wewe umeme unakatikakatika kila siku majibu hayaeleweki, lazima tushauriane vizuri ili kusudi hata kama tunapongezana suala liko sawasawa, tusikalie kupongezana tu lazima tusuguane ili kusudi tuendelee kushika Serikali.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kunipa muda huo nikushukuru sana na Mungu akubariki sana. Ahsante sana. (Makofi)