Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee ninaomba kuungana na Watanzania wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kutimiza miaka miwili wa kuongoza nchi yetu akiwa Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tumeshuhudia mafanikio makubwa katika kuimarisha miundombinu hususan barabara, reli, viwanja vya ndege, bandari, huduma za kiuchumi na kijamii kama vile ujenzi wa madarasa, hospitali, zahanati na vituo vya afya, huduma za maji, utawala bora, pamoja na kuhamasisha uwekezaji na utalii. Na pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Philip Isidor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri iliyotukuka ya kumsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mawaziri, na Naibu Mawaziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka. Tathmini zinathibitisha mafanikio yao mazuri ya utekelezaji na usimamizi wa Mpango wa Kwanza na wa Pili kupelekea Taifa letu la Tanzania kufanya vizuri mno kuinua uchumi katika kipindi hiki kigumu. Ukuaji wa uchumi wa Tanzania kwa mwaka 2022 umepungua hadi kufikia wastani wa asilimia 4.7 kutoka ukuaji wa asilimia 4.9 mwaka 2021 na kuongezeka hadi kufikia asilimia 5.3 mwaka 2023.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi na Naibu Spika na pia uongozi wote wa Bunge kwa uongozi mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri iliojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Taifa letu katika ya ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2022 mpaka Machi, 2023 Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kimkakati kwa mafanikio mkubwa sana na utekelezaji huu unaonekana mpaka kwenye ngazi ya Halmashauri zetu. Mafanikio makubwa yamejikita kwenye uboreshaji wa miundombinu ya barabara, reli, bandari, mtandao wa mawasiliano na uboreshaji wa usafiri wa anga. Naipongeza Serikali kwa hatua nzuri za utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR na ujenzi wa Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere (megawati 2,115). Miradi hii miwili ya SGR na umeme ni nguzo imara ya kiushindani katika uchumi wetu na nchi za Maziwa Makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo, uchumi wa dunia umekumbwa kwa kiasi kikubwa na athari za UVIKO- 19 na hivi sasa kuathirika zaidi na vita ya Urusi na Ukraine. Hivi karibuni kumekuwepo na taarifa katika nchi jirani za changamoto za ukwasi, uhaba na upandaji wa bei kwenye bidhaa za petroli, ujenzi, vyakula, nishati na hata pembejeo za kilimo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na athari za UVIKO-19 na vita ya Urusi na Ukraine, Serikali inatakiwa kuendelea kuchukua hatua za kibajeti kukabiliana hasa na mfumuko wa bei na kuporomoka kwa thamani ya shilingi dhidi ya dola ya Marekani na sarafu kuu zingine. Kwa kuzingatia kuyumba kwa uchumi wa dunia, bajeti hii ijielekeze kuchukua hatua za kuchochea uzalishaji wa ndani ili kupunguza balance of payment – BOP, kuimarisha Pato la Taifa kupitia sekta za kilimo, madini, utalii na uchukuzi. Hatua hizi ziende sambamba na kuimarisha mazingira ya uwekezaji hasa kwenye sekta ya kilimo na madini.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali iendelee kusimamia sera ya fedha na bajeti ikiwemo kuimarisha mifumo na kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za Serikali. Kutokana na mfumuko wa bei kwenye bidhaa za petroli na mtikisiko wa thamani ya shilingi, kutapelekea mahitaji zaidi ya fedha za kigeni na hivyo msukumo uwepo kwenye kuongeza uzalishaji wa madini na mazao ya kilimo. Hatua hizi ni muhimu kuhakikisha utulivu wa thamani ya shilingi na pia kuimarisha uhimilivu wa deni la Taifa hasa kwenye kigezo cha ulipaji wa deni la nje kwa kulinganisha na uuzaji wa bidhaa nje (mapato ya fedha za kigeni).

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za vita ya Urusi na Ukraine, bado kuna fursa kubwa kwa Tanzania hasa kwenye uzalishaji wa ziada wa nafaka kuziba pengo la nafaka kutoka Urusi na Ukraine kwenda nchi kadhaa za Afrika na mabara mengine. Serikali iimarishe upatikanaji wa pembejeo bora kwa bei nafuu na kuimarisha upatikanaji wa masoko ya uhakika. Kutokana na ruzuku kwenye mbolea na jitihada walizofanya Wizara ya Kilimo kuwapatia vitendea kazi Maafisa Ugani, ichochee kuongeza tija na uzalishaji wa mazao ya kilimo kutoka uzalishaji wa sasa wa kilo 1,000 za mahindi kwa eka mpaka kilo 4,000 kwa eka ya mahindi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na msukumo kwenye kilimo, madini na utalii, Serikali inatakiwa kuwekeza hasa kwenye miundombinu ya usafirishaji ikiwemo barabara, reli, bandari na usafiri wa anga hasa kwa mizigo. Katika Halmashauri zetu tumekuwa tunakabiliwa na changamoto hasa kwenye miundombinu ya barabara. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, barabara zinazohudumiwa na TARURA kwa asilimia zaidi ya 80 zipo kwenye hali mbaya sana kwa kukosa matengenezo ya mara kwa mara. Maeneo mengi ya vijijini barabara hazipitiki kutokana na ufinyu wa bajeti ukilinganisha na mtandao wa barabara zinazohudumiwa na TARURA. Naomba Serikali ichukue hatua za haraka kunusuru hali hii ili wananchi waweze angalau kusafirisha mazao yao.

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuidhisha ujenzi wa barabara ya njia nne kuanzia Nsalaga (Uyole) mpaka Uwanja wa Ndege wa Songwe. Kipande hiki cha barabara ambacho ni sehemu ya barabara kuu ya TANZAM, ni muhimu sana kwa kuinua uchumi wa Tanzania na hata kupunguza ajali za mara kwa mara zinazotokea katika mteremko wa Mlima Iwambi kuelekea Mji wa Mbalizi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa usafirishaji wa mazao yetu kwa soko la ndani na nje ikiwemo fursa za biashara ukanda wa SADC na uzalishaji mkubwa kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, napendekeza muendelezo wa uboreshaji wa barabara za TANZAM kipande cha Igawa - Tunduma; barabara ya bypass ya Uyole - Songwe; barabara ya Mbalizi – Shigamba – Isongole kutokana na uzalishaji wa mazao ya kilimo; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongolosi kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na madini; na pia barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea kwa kasi ile ile na pia napongeza jitihada za kuendelea kutafuta vyanzo vya fedha vya masharti nafuu kugharamia ujenzi huo. Pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa, Serikali imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na huduma katika bandari zetu hususan bandari ya Dar es Salaam ili kukabiliana na ushindani mkubwa wa bandari zingine za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika. Bandari ya Dar es Salaam inakumbana na ushindani mkubwa toka bandari za Mombasa (Kenya), Beira (Msumbiji), Nacala (Msumbiji), Durban (Afrika Kusini), Lobito (Angola) na Walvis Bay (Namibia). Maboresho ya bandari zetu iendane na kuondoa changamoto zingine ambazo zinasababisha gharama kubwa za usafirishaji kwa bandari zetu na kusababisha kupoteza biashara ya usafirishaji kwa bandari shindani. Ufanisi wa bandari unategemea pia maboresho ya barabara, reli ya kati (TRL), Reli ya TAZARA, utendaji wenye tija wa wadau wote wa bandari na hata watumishi ili kupunguza gharama za usafirishaji kwa wateja wa bandari zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa taarifa zilizopo, karibu asilimia 72 ya mzigo wote wa nchi za nje unasafirishwa kwa kupitia Dar es Salaam Corridor ambapo DR Congo ni asilimia 36, Zambia asilimia 31 na Malawi asilimia tano. Pamoja na fursa za kijografia ya bandari zetu, mzigo unaopita sasa kwenye bandari ya Dar es Salaam ni asilimia 50 tu ya biashara yote ambayo kwa sasa inashikiliwa na bandari shindani. Kwa ajili ya kunusuru biashara hii inayopotea kwa bandari shindani, Serikali ichukue hatua za haraka kuboresha huduma za TAZARA ikiwa ni pamoja ya maboresho ya miundombinu ya reli, ununuzi wa vichwa vya reli, mabehewa na vitendea kazi vingine.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali kwa haraka ishughulikie maboresho ya mkataba wa TAZARA na kisha kutafuta fedha ya masharti nafuu angalau kiasi cha shilingi bilioni 300. Katika kipindi hiki cha ushindani mkubwa na hata mfumuko wa bei wa mafuta ya petroli, mbolea na bidhaa mbalimbali, usafirishaji wa reli ni mojawapo ya suluhisho kubwa kupunguzo mzigo wa bei kubwa kwa wateja wa bandari zetu na hata wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maboresha ya reli ya TAZARA, napendekeza kuendelea na ujenzi wa bandari kavu Mbeya ambayo ina fursa kubwa katika kipindi hiki katika kuwezesha kupunguza gharama za kusafirisha kwa wateja wa bandari na hata kupunguza bei za mafuta ya petroli, pembejeo na mazao ya kilimo. Bandari kavu ya Mbeya ni njia panda kwa wateja wa nchi za Malawi, Zambia, DRC Lubumbashi na hata kwa Zimbabwe na Msumbiji.

Mheshimiwa Spika, reli ya TAZARA ambayo ni tegemeo kusafirisha mizigo kwa mikoa ya Pwani, Morogoro, mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini na pia mizigo ya nchi za nje ikiwemo, Zambia, Malawi, na DRC Congo, miundombinu inaendelea kuchakaa kutokana na kukosa matengenezo ya mara kwa mara. Serikali ichukue hatua za haraka kuinusuru reli ya TAZARA hata ikibidi kurekebisha mikataba ya umiliki na uongozi ili mradi iendeshwe kwa tija. Kuna kuchukua hatua za makusudi kwa kutumia zaidi TAZARA kusafirisha mizigo ambayo imeelemea hata uwezo wa barabara zetu. Usafirishaji wa mizigo kwa kutumia TAZARA ilenge kupunguza gharama za mafuta ya petroli, pembejeo kwa wakulima na wakati huo kupunguza gharama za kusafirisha mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuboresha TAZARA, napendekeza kukamilisha taratibu za ujenzi wa bandari kavu ya Mbeya ambapo Mamlaka ya Bandari kwa kipindi kirefu wamewahakikishia wananchi kulipa fidia ya eneo lao wanalolichukua.

Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuvutia wawekezaji na kuongeza pato la fedha za kigeni, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya Niobium ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja na reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa kimataifa. Kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapo kwetu.

Mheshimiwa Spika, Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya Niobium ambayo yanapatikana milima ya Panda Hill, Songwe Wilaya ya Mbeya na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) ni makubwa duniani na hapa kwetu pia. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini, Serikali inaweza kutengeneza fursa nyingi na kupitia Mradi wa Niobium na Kiwanda cha Ferroniobium, ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakuwepo ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000. Mradi utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (US$ 220 million) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka shilingi bilioni 50 (US$ 22 million), uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (Modern Manufacturing Plant and Smelter). Pamoja na kuingiza teknolojia hii adimu na ujuzi (skills transfer) pia itakuwa itachangia huduma za kijamii (Corporate Social Investment in Community) na chanzo cha fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.