Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri Mkuu Mheshiliwa Kassim Majaliwa Majaliwa kwa hotuba nzuri kutoka katika ofisi yake. Pia niwapongeze Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako pamoja na Naibu Mawaziri wao. Waziri Mkuu pamoja na wasaidizi wake hawa wanaupiga mwingi.

Mheshimiwa Spika, mimi mchango wangu utajikita kwenye Kiwanda cha Tanzania Biotech Products Limited (TBPL) cha Kibaha mkoani Pwani kilicho chini ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC). Kiwanda hiki kimeshaanza uzalishaji wa viuatilifu vya kuangamiza mbu na wadudu wa mazao na vilevile kina uwezo wa kuzalisha mbolea.

Mheshimwa Spika, bidhaa za kiwanda hiki ni za kibaiolojia. Kiwanda hiki kimejengwa kutokana na mahusiano mazuri ya kidiplomasia baina ya Tanzania na Cuba. Ni kiwanda bora na cha mfano Barani Afrika.

Mheshimiwa Spika, kiwanda hiki cha viuadudu kilianza uzalishaji rasmi mwaka 2017 ambapo uwezo wa uzalishaji wa kiwanda ni lita milioni sita kwa mwaka na kinatumia malighafi inayopatikana ndani ya nchi kwa asilimia 98. Pamoja na uwezo wa kiwanda hiki, pamekuwa na changamoto kubwa ya soko la bidhaa kutoka kiwandani, hali iliyopelekea watumishi wa kiwanda kutokulipwa stahiki zao kutokana na ukosefu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, lengo la ujenzi wa kiwanda hiki lilikuwa ni kuchangia kutokomeza malaria nchini na Afrika kwa ujumla kwa kuzalisha viuatilifu visivyo vya kemikali. Lengo la pili ni kuzalisha viuatilifu na mbolea zisizo na kemikali. Mbolea hizi zitaendeleza kilimo hai ambacho kina soko kubwa duniani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na uwepo wa kiwanda hiki bora na cha kisasa, pamekuwepo na matumizi mabaya ya rasilimali hii kutokana na ukosefu wa soko la bidhaa zinazozalishwa. Mpango wa awali ulizitaka Halmashauri zote nchini kununua bidhaa hizo ili kuangamiza mbu waenezao malaria kwa pamoja kama nchi. Cha kusikitisha ni kwamba Halmashauri nyingi nchini hazijashiriki kununua dawa katika kiwanda hiki.

Mheshimiwa Spika, utokomezaji wa malaria hapa nchini utafanikiwa tu ikiwa nchi yetu itaanzisha programu maalum ya kununua na kutumia dawa hizi kwa wakati mmoja katika maeneo yote hapa nchini Tanzania. Huko Zanzibar matumizi sahihi ya dawa kutoka katika kiwanda hiki kumepunguza ugonjwa wa malaria kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, hapa Tanzania kilimo ndio uti wa mgongo wa uchumi wa watu wengi kwani asilimia kubwa ya wakazi hujishughulisha na shughuli za kilimo. Lakini kilimo hukabiliwa na changamoto kubwa ya wadudu wa mazao na uchakavu wa ardhi. Pamoja na changamoto hizi, Tanzania inakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa mbolea na viuatilifu na hata zile zilizopo kutokidhi mahitaji ya soko. Uwepo wa kiwanda hiki unaweza kuwa mkombozi wa wakulima wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa kiwanda hiki, ninaishauri Serikali kufanya yafuatayo; kwanza Wizara ya Afya ihusike kikamilifu na ichukue jukumu la hukakikisha kuwa dawa kutoka kiwandani zinanunuliwa na kusambazwa nchi nzima.

Pili, ikiwezekana, Bohari ya Madawa (MSD) ihusishwe kununua dawa ya viuadudu vya mazalia ya mbu kutoka Kiwanda cha Biotech kilichopo Kibaha ili kuzuia malaria badala ya ilivyozoeleka kupoteza mamilioni ya fedha kununua madawa kutoka nje kwa ajili ya kutibu ugonjwa wa malaria.

Mheshimiwa Spika tatu, kwa kuwa kiwanda hiki kinamilikiwa na Serikali kwa asilimia mia moja chini ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC), ninashauri Serikali itenge fedha na kuwalipa wafanyakazi wanaodai stahiki zao.

Nne, Serikali ijikite kikamilifu kwenye uzalishaji wa mbolea na viuatilifu hai ili vitumike kikamilifu kwenye sekta ya kilimo kwani kuna changamoto kubwa nchini ya bidhaa hizi.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.