Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia hoja iliyoko Mezani. Katika mijadala ambayo imeendelea kwa siku kadhaa humu ndani, tumekuwa tukijadili sana kuhusiana na makosa dhidi ya maadili. Michango mingi imekuwa ikionyesha kwamba kana kwamba hatuna sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kulijulisha rasmi Bunge lako Tukufu pamoja na Watanzania wote kwamba sheria hizi tunazo toka mwaka 1934. Tulizifanyia mabadiliko mwaka 1959, lakini tukafanya mabadiliko makubwa zaidi mwaka 1998 kupitia Sheria za Makosa ya Kujamiiana. Kwa hiyo, sheria hizi zipo na ni kali. Sasa changamoto imekuwa ni kwenye utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe taarifa pia kuwa tarehe 5 Aprili, 2023 Tume ya Kurekebisha Sheria kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini na wadau wengine mbalimbali ilifanya kongamano la tathmini ya utekelezaji wa sheria hizi za makosa dhidi ya maadili. Mchakato huo bado unaendelea. Sisi Serikali bado tunaendelea kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali kujua ni kwa nini utekelezaji wa sheria umekuwa na changamoto.

Mheshimiwa Spika, kama ulivyoelekeza leo, tutakuja na matokeo ya tathmini hiyo na ikibidi kufanya marekebisho ya sheria hiyo, tutafanya marekebisho. La msingi ni kwamba sheria zipo, hatuhitaji kutunga sheria nyingine, sana sana ikibidi tuweze kufanya marekebisho ya sheria hizo.

Mheshimiwa Spika, kwa maana ya muda, ninaomba niishie hapo, lakini muhimu zaidi naunga mkono hoja iliyowekwa Mezani na Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)