Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuwa mtu wa kwanza katika kuchangia hotuba ya TAMISEMI kwa jioni ya leo ya tarehe 14 mwenzi wa nne mwaka huu wa 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza wananchi wa Buhigwe wamenituma nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri wa Tanzania kwa fedha nyingi sana ambazo amepeleka katika Wilaya ya Buhigwe. Amefungua wilaya yetu na ameendelea kufungua mkoa wetu. Amefanya nini katika Wilaya yetu ya Buhigwe? Amegusa Maisha ya wananchi ya kila siku katika yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023 tulipata shilingi 3,336,624,000,901 ambazo zilikuja kwenye ukamilishaji wa maboma ya shule za msingi, ukarabati wa shule kongwe, ujenzi wa matundu ya vyoo katika shule za msingi, ukamilishaji wa zahanati, ununuzi wa vifaa tiba kwenye hospitali, vituo vya afya na zahanati. Wananchi wa Buhigwe wanasema ahsante sana. Wanatoa shukrani za dhati kwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki pamoja na Manaibu wake Mawaziri akiwepo Mheshimiwa Festo pamoja na Mheshimiwa Ndejembi kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi ya pekee kwa kuwashukuru kwa utaratibu mzuri ambao mwaka huu tumeuona. Walituita wakiwa na kikosi kazi cha TAMISEMI, tukakaa nao sisi kama Wabunge wa kila mkoa na wakatupa nafasi ya kutoa vipaumbele vyetu na changamoto. Katika nafasi hiyo, kuna methali Waswahili wanasema, “kiu isiyoweza kuishia kwenye mto, hiyo ni kifo.” Basi tuliweza kutoa changamoto zetu, tukatoa vipaumbele vyetu na tumeona kwa uhakika waliyapeleka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ameyajibu kwa matendo. Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa afya, tumeona kazi kubwa sana kwa wilaya ambayo ni changa. Tumepata vituo vitatu vya afya. Kituo cha Kajana, tulipata shilingi milioni 500, Mayaya shilingi milioni 500 na Lusaba shilingi milioni 500. Tunategemea mwezi wa Saba vitaanza kutoa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo tumepata fedha za kumalizia maboma ya zahanati katika vijiji sita, tulipata shilingi milioni 300. Wananchi wa Buhigwe pamoja na viongozi wote wa vyama vyote na wa madhehebu yote wamenituma nije nitoe shukrani kwa Mheshimiwa Rais pamoja na wasaidizi wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye TARURA, katika miaka hii miwili ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ametusaidia pakubwa. Japokuwa mahitaji yetu ni makubwa, lakini tulipata shilingi bilioni 5.9 ambazo zimeweza kutujengea kilometa tano za lami Makao Makuu ya Wilaya na tukajengewa kilometa 1.2 ya lami na kilometa moja. Mpaka sasa hivi tunao mradi mwingine ambao tumeupata, na tumepatiwa fedha. Mradi huo unatoka katika Kata ya Muyama kupitia Kasumo kwenda Kasulu kilometa 12, ambazo zitagharimu fedha ya Kitanzania shilingi bilioni 15.6, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utawala bora, Mheshimiwa Rais ametusaidia parefu na pakubwa sana. Kwa miaka mingi tulikuwa hatuna Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, alitoa fedha na mwaka 2022 tarehe 16 Mwezi wa Kumi yeye mwenyewe amekuja kuizindua. Sambamba na hilo, ujenzi wa Mahakama ya Wilaya umeshakamilika na huduma zinaendelea kutolewa. Ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo katika Kata ya Buhigwe umeanza kujengwa. Tunamshukuru sana, tunampongeza sana na Mungu ambariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani, bado tunazo changamoto nyingi. Moja, tunao upungufu mkubwa kwenye kada ya watumishi wa afya. Mahitaji yetu kwenye afya ni wafanyakazi 819, waliopo ni 210 pungufu ni 609. Tuna upungufu wa asilimia 75. Tunaomba ajira mpya mtupe kipaumbele mlete watumishi. Kwenye upande wa elimu, mahitaji ni walimu 1,487; waliopo ni 692, pungufu ni 794, sawa na asilimia 55. Kwenye ajira hizi mpya tunaomba Serikali ituangalie kwa jicho la huruma na kwa upendo mkubwa mwaelekeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi maalumu kwa vijana wanaojitolea wa tasnia ya elimu. Kuna vijana wengi ambao wamejitolea baada ya kumaliza vyuo vyao, wapo kwenye shule zetu za kata, wapo kwenye shule zetu za Serikali, hao ndio wahimili, ndio wazalishaji, na wameshatoa mchango mkubwa. Naomba sana, katika hizi ajira mpya ambazo zimetolewa kwa moyo wa dhati na kwa huruma ya Mungu, hawa wapewe kipaumbele. Wapewe kipaumbele katika ajira hizi zilizotangazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili, pamoja na kwamba tumepata vituo vya afya, bado tuna kata ambazo zina idadi kubwa ya watu, na uzuri watu wa kule Buhigwe wameshajipanga kwa ajili ya kuchangia kwenye shughuli za maendeleo. Kata ya Muhinda na Kata ya Mubanga wameshachagua sehemu ambayo wakipata fedha ya kujenga kituo cha afya ambacho kitasaidia wananchi zaidi ya 45, wameshaanza na mchakato wa kufyatua tofali. Tunaomba kituo cha afya kijengwe katikati ya Kata ya Muhinda na Mubanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine ni kituo cha afya tena ambacho kitasaidia tena kata mbili na ni mpakani mwa Burundi kabisa kuna watu wengi, zaidi ya 44,000, nayo ni Kata ya Mkatanga na Kata ya Kibwigwa. Kituo hicho kije kijengwe katikati ya Kata ya Kibwigwa na Mkatanga, nao wameshachagua sehemu yao ambayo inaitwa Muharuro hapo ni center nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo marefu, nakushukuru sana, naishukuru Serikali, najua imesikia na itatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)