Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hotuba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Niungane na wenzangu waliotangulia, kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa hatua iliyochukua siku ya jana katika mikopo ya asilimia 10 ya kuhakikisha wanabadili utaratibu, namna ya utoaji wa hiyo mikopo. Ukweli ni kwamba sasa Mfuko huu ulikuwa unakwenda kufa, kwa nini ulikuwa unakwenda kufa? Ni kutokana na utaratibu ambao ulikuwa unatumika katika suala zima la utoaji wa mikopo. Jambo la pili, mikopo hii ilikuwa haiwafikii walengwa na badala yake ilikuwa inawanufaisha watu chache kwa ajili ya maslahi yao binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu ukweli sisi sote tunajua utaratibu wa mikopo hii inavyotolewa kwenye halmashauri zetu, lakini ukisoma Ripoti ya CAG ya mwaka huu 2022/2023, ni masikitiko makubwa sana kuona kwamba bilioni 88 zimepotea na hazijulikani ziliko na hata vikundu vilivyopewa mikopo hii ya bilioni 88 havijulikani vilipo. Hili ni jambo la aibu kwa watu waliopewa dhamana ya kusimamia mikopo hii ili iweze kuwafikia welangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kauli ya Serikali naomba nishauri mambo machache: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza tunaomba waliohusika katika suala zima la utoaji wa mikopo hiyo ambayo haijulikani ilipo wachukuliwe hatua ili liwe fundisho huko mbele tuendako, mambo yako wazi kabisa. Ukisoma katika Ripoti ya CAG, ukienda katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, vikundi 34 vimepewa mikopo zaidi ya milioni 600 na pointi lakini vikundi hivyo havijulikani, havijulikani kwa maendeleo hawavijui kabisa. Hili ni jambo la ajabu, kikundi ili kipewe mkopo kwanza jambo la kwanza ni lazima Afisa Maendeleo wa eneo husika akajiridhishe kwamba kikundi kipo na kina mradi kinaouendesha ndipo kikundi kinapata sifa ya kukopa mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tunaliona kwenye halmashauri zetu, ili kikundi kipewe mkopo ni lazima kiwe na mdhamini mwenye mali zisizohamishika. Kikundi hiki ndipo kinapewa mkopo, sasa hivi vikundi vilipewaje mkopo wakati Maafisa Maendeleo wa maeneo husika hawavijui na wala hawavitambui kwenye maeneo yao. Utaona hiki ni kitu cha ajabu sana. Tuna watu wachache ambao wanakwamisha juhudi za Serikali, hawa wanatakiwa kuchukuliwa hatua ili huko mbele tuendako hayo mambo yasijirudie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, naomba nizungumzie kwenye Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Sisi sote tutakuwa ni mashahidi na hata Waziri inawezekana anajua, ndani ya miezi sita wananchi wa Mji wa Tunduma wamekuwa wakikutana na adha kubwa ya stendi na hili liko wazi na hili limekuwa ni janga ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Stendi ilikojengwa hatukatai kujengwa stendi ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma na hilo ni hitaji la kila mmoja kuona maendeleo yanafanyika kwenye eneo lake na hili jambo sisi Wabunge tunashukuru, lakini changamoto ambayo wananchi wamekuwa wakikutana nayo ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Tunduma wamekuwa wakikutana na adha na mateso makubwa sana ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Stendi iko ndani ya Kata ya Mpemba, Kata ya Mpemba ni Kata ambayo iko mwanzoni unapoingia ndani ya Mji wa Tunduma, Kata ya Mpemba imepakana na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi lakini kushoto imepakana na Halmashauri ya Wilaya ya Ileje. Kutoka katika Kata ya Mpemba kwenda kufika ndani ya Mji wa Tunduma Mjini ni kilomita 12, mwananchi anatoka Wilaya ya Mbeya amepanda gari analipia nauli Sh.4,000, lakini akishashushwa ndani ya Stendi ya Mpemba kutoka pale kuja kufika Mjini anatumia zaidi ya nauli aliyotumia kutoka Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi wananchi wamekuwa wakikutana na changamoto kwa sababu jambo la kwanza daladala hazitoshelezi za kuwatoa katika eneo la Mpemba kwenda kuwafikisha Tunduma Mjini hazitoshi. Jambo la pili, wananchi mpaka wamekuwa wakifikia hatua ya kuibiwa, wamekuwa wakikutana na changamoto nyingi wengine wametembea kwa mguu umbali mrefu kiasi kwamba wamekutana na changamoto mbalimbali ambazo zinahatarisha usalama wa maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri, alichukue hili aende akapitie Halmashauri ya Mji wa Tunduma aone namna wananchi wanavyokutana na changamoto kubwa ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma na najua kwa nafasi yake ana uwezo wa kushauri kwa sababu kama Baraza tumeshauri lakini mawazo yetu kama Baraza hayajafanyiwa kazi. Badala yake watu wachache ambao wanaona jambo hili linaweza kufaa ama kwa maslahi yao, wanalichukua jambo hili kana kwamba sasa imekuwa ni siasa, lakini siasa hii inawaumiza wananchi wa Mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hivi tusisubiri wananchi wa Mji wa Tunduma waje waandamane kwa sababu tumeona migomo ya waendesha daladala imefanyika, migomo ya waendesha mabasi yaendayo mikoani imefanyika. Sasa tusisubiri migomo ya wananchi wa kawaida ndipo tuje Mji wa Tunduma kwa ajili ya kutatua changamoto hii. Niombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu ni eneo lake alichukue jambo hili, aone ni namna gani anaweza kutusaidia kukabiliana na changamoto hii ambayo imekuwa ni mateso na changamoto kubwa kwa wananchi wa Mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeki, jambo la tatu naomba nizungumzie suala zima la elimu. Sisi sote tunajua na wananchi wetu wanajua kwamba elimu ya sasa ni elimu bila ada, lakini changamoto ambayo wananchi wamekuwa wakiikuta ni afadhali ya ada. Tuseme ukweli kabisa, changamoto ambayo wananchi wamekuwa wakikutana nayo ni afadhali ya kulipa ada, lakini si changamoto hii ambayo wananchi wanakutana nayo sasa, ni afadhali Serikali ikawa wazi na ikasema ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hela hizi ambazo zinatolewa kwa ajili ya kusapoti elimu ya bila ada hazipelekwi ipasavyo mashuleni. Badala yake Walimu na wanafunzi wamekuwa wakikutana na mazingira magumu sana huko mashuleni kwa sababu bajeti yao haitekelezwi ipasavyo na badala yake ile bajeti inapelekwa kidogo jambo ambalo linashindwa kukidhi mahitaji ya wanafunzi na Walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la vitabu vya kufundisha na kufundishia. Ukisoma katika Ripoti ya CAG iliyotolewa Februari, mwaka huu 2023 inasema wazi kabisa, kulikuwa na bajeti ambayo ilikuwa imetengwa katika Mradi wa Fungu 4393. Mradi huu ulikuwa umetengewa kiasi cha bilioni 22.850 kwa ajili ya ununuzi wa vitabu vya wanafunzi milioni 2.25, lakini badala yake mpaka kufikia Februari mwaka huu 2023 hakuna hata shilingi mia ambayo imetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vitabu vya wanafunzi, ni nini tunafanya kwa wanafunzi wetu? Tumewaweka Walimu katika mazingira magumu, lakini tumewaweka wanafunzi katika mazingira magumu ya kujifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenda miundombinu na madawati hali ni mbaya, mtoto anakalia jiwe kutoka darasa la kwanza mpaka darasa la saba halafu mnategemea akiwa Dokta akutibu vizuri?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. STELLA S. FIYAO: …Haiwezekani! Hatuwezi kufika kwa utaratibu wa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)